Ufunuo 22 - Swahili Congo Revised Bible 2002

1Kisha yule malaika akanionyesha muto wa maji ya uzima wenye kungaa kama kioo, uliokuwa ukitiririka toka kwenye kiti cha kifalme cha Mungu na cha Mwana-Kondoo.

2Muto ule ulitelemuka katikati ya barabara ya muji mutakatifu. Kandokando ya ule muto, kulikuwa kumeota muti wa uzima, nao unatoa matunda mara kumi na mbili kwa mwaka, maana yake mara moja kila mwezi. Majani ya muti ule yanatumiwa kama dawa ya kuponyesha mataifa.

3Hakutakuwa tena kitu chochote kinacholaaniwa na Mungu.

Kiti cha kifalme cha Mungu na cha Mwana-Kondoo kitakuwa ndani ya muji ule, na watumishi wa Mungu watamwabudu.

4Wataona uso wake na jina lake litaandikwa juu ya paji za nyuso zao.

5Hakutakuwa usiku tena, wala hawatakuwa na lazima ya mwangaza wa taa wala jua, kwa sababu Bwana wetu na Mungu wetu mwenyewe atawaangazia, nao watatawala milele na milele.

Kurudi kwa Yesu

6Kisha yule malaika akaniambia: “Maneno haya ni ya kweli na ya uhakika. Na Bwana Mungu anayewaongoza manabii kwa njia ya Roho wake ametuma malaika wake kwa kuwaonyesha watumishi wake mambo yanayopaswa kutokea kisha kidogo.”

7Yesu anasema: “Sikiliza, ninakuja upesi! Heri yule anayeshika maneno ya unabii yanayoandikwa katika kitabu hiki!”

8Ni mimi Yoane niliyesikia na kuona mambo hayo. Na wakati nilipokwisha kuyasikia na kuyaona, nilianguka mbele ya malaika aliyeyaonyesha kwangu kwa kumwabudu.

9Lakini akaniambia: “Angalia, usifanye vile! Kwa maana mimi ni mutumishi kama vile wewe, na wandugu zako manabii na watu wanaoshika maneno ya unabii yanayoandikwa katika kitabu hiki. Ni Mungu ndiye unayepaswa kumwabudu!”

10Kisha akaniambia: “Usichunge kwa siri maneno haya ya unabii wa kitabu hiki, kwa sababu wakati wa kutimia kwa mambo haya unakaribia.

11Mutu mubaya aendelee kufanya ubaya, na mutu muchafu azidi kuwa muchafu, na mutu mwema aendelee kutenda mema na mutu mutakatifu aendelee kuwa mutakatifu.”

12Yesu anasema: “Sikiliza, ninakuja upesi! Nitaleta mushahara kwa kulipa kila mumoja wenu kwa kadiri ya matendo yake.

13Mimi ni Alfa na Omega, mwanzo na mwisho.”

14Heri wale wanaosafisha kanzu zao, kwa maana watakuwa na haki ya kukula matunda ya muti wa uzima na ya kuingia katika muji ule kwa kupitia kwenye milango.

15Lakini mbali ya muji ule kuna watu wenye kuchukiza, wachawi, wazinzi, wauaji, wanaobudu sanamu na wasema uongo na wote wanaoupenda.

16“Mimi Yesu, nimemutuma malaika wangu kwa kuwashuhudia maneno haya yote katika kanisa. Mimi ni wa shina na wa uzao wa mufalme Daudi. Mimi ni nyota ya asubui.”

17Roho na Bibi arusi wanasema: “Kuja!”

Naye mwenye kusikia maneno haya aseme vilevile: “Kuja!”

Yule anayesikia kiu akuje, na yule anayetaka maji ya uzima akuje kuyapokea kwa bure.

Maneno ya mwisho

18Mimi Yoane ninatoa maonyo haya kwa kila mutu anayesikia maneno ya unabii yanayoandikwa katika kitabu hiki: kama mutu akiongeza kitu juu ya maneno haya, Mungu atamwongezea mapigo yale yanayoandikwa katika kitabu hiki.

19Na kama mutu akipunguza neno kati ya maneno ya unabii yanayoandikwa katika kitabu hiki, Mungu ataondoa fungu la matunda ya muti wa uzima alilotayarishiwa, pamoja na fungu alilotayarishiwa katika ule muji mutakatifu ambavyo vimeandikwa katika kitabu hiki.

20Mwenye kushuhudia maneno hayo anasema: “Ndiyo, ninakuja upesi!”

Amina! Kuja Ee Bwana Yesu!

21Ninawatakia ninyi wote neema kutoka kwa Bwana Yesu. Amina.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help