Matendo ya Mitume 21 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Paulo anakwenda Yerusalema

1Tulipokwisha kuagana nao, tukasafiri ndani ya chombo na kwenda mara moja mpaka kwenye kisanga cha Kosi. Kesho yake tukafika katika muji Rodo, na kutoka kule tukafika katika muji Patara.

2Kule tukakuta chombo kilichokuwa kikienda katika inchi ya Foinikia; tukaingia ndani yake na kusafiri.

3Tulipoanza kuona kisanga cha Kipuro, tukikiacha kwa upande wa kusini na kuelekea katika jimbo la Suria. Tukaezeka kwenye kivuko cha Tiro, kwa maana ni pale chombo kilipaswa kupakuliwa mizigo.

4Kule tukakuta wanafunzi na tukakaa pamoja nao muda wa juma moja. Nao wakiogozwa na Roho Mutakatifu wakamwambia Paulo asiende Yerusalema.

5Lakini muda ule ulipotimia tukaondoka na kuendelea na safari yetu. Waamini wote pamoja na wanawake na watoto wao wakatusindikiza mpaka mbali na hata kufika kwenye kivuko cha muji. Kule sisi wote tukapiga magoti na kuomba.

6Kisha kuagana, tukaingia ndani ya chombo, nao wakarudi kwao.

7Kutoka Tiro tukaendelea hata tukafika Tolemai. Na pale tukamaliza safari yetu ya bahari. Kule tulisalimia wandugu zetu waamini na kukaa nao muda wa siku moja.

8Kesho yake tukaondoka na kufika katika muji Kaisaria. Kule tukaenda kupanga katika nyumba ya muhubiri Filipo, aliyekuwa mumoja kati ya wale watu saba waliochaguliwa Yerusalema.

9Yeye alikuwa na wabinti wane waliokuwa hawajaolewa waliokuwa na zawadi ya kutabiri.

10Nasi tulipokuwa tumekwisha kukaa kule siku nyingi, nabii mumoja, aliyeitwa Agabo, akafika kutoka Yudea.

11Akatufikia, akatwaa mukaba wa Paulo, akajifunga miguu na mikono yake mwenyewe na kusema: “Roho Mutakatifu anasema: ‘Wayuda watamufunga mutu mwenye mukaba huu namna hii kule Yerusalema na kumutoa kwa watu wa mataifa mengine.’ ”

12Basi tuliposikia maneno hayo, sisi pamoja na watu wa Kaisaria tukamusihi Paulo asiende Yerusalema.

13Lakini Paulo akajibu: “Kwa sababu gani munalia na kunivunja moyo? Mimi niko tayari, si kwa kufungwa tu kule Yerusalema, lakini hata kufa vilevile kwa ajili ya jina la Bwana Yesu.”

14Tulipoona kwamba amekataa shauri letu, tukanyamaza na kusema: “Mapenzi ya Bwana yafanyike.”

15Nyuma ya siku zile tulizokaa kule tukafunga mizigo yetu na kwenda Yerusalema.

16Wanafunzi wamoja toka muji Kaisaria wakatusindikiza na kutufikisha kwa Munasoni, mutu wa Kipuro, aliyegeuka mwamini tangu siku nyingi, kusudi tupate kupanga kwake.

Paulo anamutembelea Yakobo

17Tulipofika Yerusalema, wandugu waamini wakatupokea kwa furaha.

18Kesho yake tukaenda pamoja na Paulo kwa Yakobo, na wazee wote wa kanisa walikuwa kule vilevile.

19Kisha kuwasalimu, Paulo akaanza kuwaelezea neno kwa neno mambo yote, Mungu aliyofanya kati ya mataifa mengine kwa njia ya kazi yake.

20Nao waliposikia maneno hayo, wakamusifu Mungu. Na kisha wakamwambia Paulo: “Ndugu, unaona namna maelfu ya Wayuda walivyoamini; nao wote wanajitolea sana kwa kushika Sheria.

21Lakini wamesikia habari juu yako kwamba unawafundisha Wayuda wote wanaokaa katika inchi za mataifa wasishike Sheria ya Musa. Umewakataza wasiwatahiri watoto wao wala kufuata desturi zetu za kiyuda.

22Hakika watu wale watasikia kwamba umekwisha kufika. Basi tufanye nini?

23Kwa hiyo, ufanye kama hivi tunavyotaka kukuambia. Hapa tuko na watu wane waliofanya kiapo mbele ya Mungu.

24Kwenda ujiunge na watu wale katika ibada ya utakaso, nawe uwalipie malipo yanayoamuriwa kusudi wapate kunyolewa. Hivi watu wote watajua kwamba habari zile walizoambiwa juu yako zilikuwa za uongo mutupu. Na zaidi ya hii watajua kwamba unafuata Sheria ya Musa katika maisha yako.

25Lakini kwa ngambo ya watu wa mataifa mengine walioamini, tumekwisha kuwaandikia juu ya mambo tuliyoamua. Tumewaamuru kwamba wasikule vyakula vilivyotolewa kwa kutambikia sanamu; wasikule damu wala nyamafu; na waepuke uasherati.”

26Halafu kesho yake Paulo akaenda na wale watu wane, na akajitakasa pamoja nao. Kisha akaingia ndani ya hekalu na kutangaza wakati siku za utakaso zitakapotimia, na sadaka itakayotolewa kama malipo kwa ajili ya kila mumoja wao.

Kufungwa kwa Paulo

27Zile siku saba zilipokaribia kutimia, Wayuda wamoja waliotoka katika jimbo la Azia wakamwona Paulo ndani ya hekalu. Wao wakashawishi watu wote waliokusanyika, wakamukamata

28wakilalamika: “Ninyi wanainchi Waisraeli, mutusaidie! Huyu ndiye mutu yule anayefundisha kwa watu wote, nafasi zote maneno ya kuzarau taifa letu, Sheria ya Musa, na hekalu hili. Na zaidi ya hii, amewaingiza watu wa mataifa mengine katika hekalu na hivi amechafua Pahali hapa Patakatifu!”

29(Walisema hivi kwa sababu walikuwa wamemwona Paulo katika muji pamoja na Mwefeso mumoja aliyeitwa Trofimo, nao walizani kwamba Paulo alikuwa amemwingiza katika hekalu.)

30Muji wote ukajaa fujo na watu wakakusanyika pale mbiombio. Wakamukamata Paulo na kumukokotea mpaka inje ya hekalu, na mara moja wakafunga milango yake.

31Walipotafuta kumwua Paulo, habari ikamufikia mwongozi wa kundi la waaskari kwamba muji wote wa Yerusalema umejaa fujo.

32Mara moja akatwaa waaskari pamoja na wakubwa wao na kwenda nao haraka pale watu walipokusanyika. Nao walipomwona huyo mwongozi pamoja na waaskari wake wakaacha kumupiga Paulo.

33Halafu huyo mwongozi akamujongelea Paulo, akamukamata na kuamuru afungwe na minyororo miwili. Kisha akauliza: “Mutu huyu ni nani? Naye amefanya nini?”

34Wamoja katika makutano walikuwa wakilalamika na kusema hivi, na wengine hivi. Basi kwa kuwa yule kiongozi hakuweza kupata jibu kamili kwa sababu ya makelele, akaamuru kwamba wamupeleke Paulo ndani ya upango wa waaskari.

35Paulo alipofika kwenye ngazi, waaskari walilazimishwa kumubeba kwa sababu makutano yalitomboka sana.

36Maana wote walimufuata nyuma wakilalamika: “Auawe!”

Paulo anajitetea

37Waaskari walipotaka kumwingiza Paulo katika upango, akamwuliza mukubwa wa kundi la waaskari: “Unaweza kuniruhusu kukuambia neno moja?”

Yule mukubwa wa kundi la waaskari akamwuliza: “Unajua Kigriki?

38Wewe si yule Mumisri aliyeleta fujo siku hizi na kuwaongoza wauaji elfu ine kwenda naye katika jangwa?”

39Paulo akajibu: “Mimi ni Muyuda, muzaliwa wa muji Tarso, katika jimbo la Kilikia. Ninatoka katika muji unaosifiwa sana. Tafazali uniruhusu kusema na watu hawa.”

40Yule mukubwa wa kundi la waaskari akamuruhusu. Basi Paulo akasimama juu ya ngazi, akainua mukono kwa kuwaalika watu wanyamaze. Na watu waliponyamaza kabisa, Paulo akawaambia maneno haya katika luga ya Kiebrania:

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help