1 Yoane 4 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Kutambua Roho wa Mungu na roho ya mupinga Kristo

1Wapendwa wangu, musimwaminie kila mutu anayesema kwamba yuko na Roho wa Mungu, lakini mumupime kwa kuhakikisha kama roho yule anatoka kwa Mungu. Kwa maana manabii wengi wa uongo wametokea katika dunia.

2Mutatambua Roho wa Mungu kwa njia hii: kila mutu anayesadiki kwamba Yesu Kristo amekuja katika hali ya kimutu yuko na Roho wa Mungu.

3Lakini mutu yeyote asiyemusadikia Yesu hana Roho anayetoka kwa Mungu. Mutu yule yuko na roho ya mupinga Kristo. Ninyi mumekwisha kusikia kwamba roho yule atakuja, na sasa amekwisha kuja katika dunia.

4Lakini ninyi, watoto wangu, muko watoto wa Mungu, nanyi mumewashinda manabii wa uongo; maana roho anayekaa ndani yenu ni mwenye uwezo kuliko yule anayekaa ndani ya watu wa dunia.

5Manabii wa uongo ni watu wa dunia, ndiyo maana wanasema mambo ya kidunia nao watu wa dunia wanawasikiliza.

6Lakini sisi ni watu wa Mungu. Mutu anayemujua Mungu anatusikiliza; yule asiyemujua Mungu hatusikilizi. Basi ni kwa njia hii tunaweza kutambua tofauti kati ya Roho wa ukweli na roho ya udanganyifu.

Mungu ni Upendo

7Wapendwa wangu, tupendane, kwa maana upendo unatoka kwa Mungu. Kila mutu anayekuwa na upendo ni mutoto wa Mungu naye anamujua Mungu.

8Mutu asiyekuwa na upendo hamujui Mungu kwa maana Mungu ni upendo.

9Hii ndiyo namna Mungu alivyoonyesha upendo wake kwetu: alimutuma Mwana wake wa pekee katika dunia kusudi kwa njia yake tupate uzima wa milele.

10Na huu ndio upendo: si kwamba sisi tulimupenda Mungu, lakini kwamba ni yeye ndiye aliyetupenda hata akatuma Mwana wake kama vile sadaka iliyotolewa kwa ajili ya usamehe wa zambi zetu.

11Wapendwa wangu, ikiwa Mungu alitupenda sisi namna ile, sisi vilevile tunapaswa kupendana.

12Hakuna hata mutu aliyekwisha kumwona Mungu wakati wowote. Tukipendana sisi kwa sisi, Mungu anaungana nasi na upendo wake unakamilika ndani yetu.

13Kwa njia hii tunatambua kwamba sisi tunakaa ndani ya Mungu, naye anakaa ndani yetu: yeye ametupatia Roho wake.

14Na sisi tumeona na kushuhudia kwamba Baba amemutuma Mwana wake kuwa Mwokozi wa dunia.

15Kila mutu anayesema kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu, Mungu anaungana naye, na mutu yule anaungana na Mungu.

16Na sisi tumejua na kuamini upendo Mungu anaokuwa nao kwetu.

Mungu ni upendo. Yule anayeishi katika upendo anaungana na Mungu, na Mungu anaungana naye.

17Hivi upendo umekamilishwa ndani yetu, kusudi tupate kuwa na tumaini kwa Siku ile ya hukumu. Kwa sababu maisha yetu katika dunia hii yanafanana na maisha ya Yesu Kristo.

18Katika upendo hakuna woga, lakini upendo kamili unaondoa woga wote. Maana yule anayekuwa na woga hakamiliki katika upendo kwa sababu woga unaonyesha hali ya kuhukumiwa.

19Sisi tuko na upendo kwa sababu Mungu ndiye aliyetupenda wa kwanza.

20Kama mutu akisema “Ninamupenda Mungu,” naye anamuchukia ndugu yake, yeye ni mwongo. Kwa maana yule asiyemupenda ndugu yake anayemwona, hawezi kumupenda Mungu asiyemwona.

21Basi hii ndiyo amri tuliyopewa na Kristo: yule anayemupenda Mungu anapaswa kumupenda ndugu yake vilevile.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help