Ezekieli 13 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Manabii wa uongo

1Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi:

2Wewe mwanadamu, uwakaripie manabii wa Waisraeli wanaotangaza mambo ambayo wameyafikiria wao wenyewe. Uwaambie: Musikilize neno la Yawe!

3Bwana wetu Yawe anasema hivi: Ole kwenu manabii wapumbafu munaofuata mawazo yenu wenyewe na maono yenu wenyewe!

4Manabii wenu, enyi Waisraeli ni kama mbweha wanaopitapita katika mabomoko.

5Hawakwenda kulinda sehemu zile za kuta zilizobomoka wala hawajengi kuta mupya kusudi Waisraeli waweze kujilinda wakati wa vita siku ile ambayo mimi Yawe nimeiweka.

6Maono yao ni ya uongo mutupu na wanachotabiri ni udanganyifu mutupu. Wanasema “Ni ujumbe wa Yawe” lakini Yawe hakuwatuma; kisha wanamutazamia atimize yale wanayosema.

7Basi, ninawauliza: Maono yenu si uongo mutupu na utabiri wenu udanganyifu wakati munaposema “Ni ujumbe wa Yawe”, ijapokuwa mimi sijaongea nanyi hata kidogo?

8Basi, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Kwa kuwa maneno yenu ni udanganyifu na maono yenu ni ya uongo mutupu, basi, mimi nitapingana nanyi.

–Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe!

9Nitanyoosha mukono wangu juu yenu ninyi manabii munaotoa maono ya uongo na kutabiri udanganyifu mutupu. Watu wangu watakapokutanika kwa kuamua maneno, ninyi hamutakuwa pale. Wala hamutakuwa katika kitabu cha majina ya Waisraeli na hamutaingia katika inchi ya Waisraeli; halafu mutatambua kwamba mimi ni Bwana wenu Yawe.

10Manabii hao wanawapotosha watu wangu na kuwaambia “Kuna amani”, wakati hakuna amani. Watu wangu wanajenga ukuta usiofaa, nao wanaupakaa chokaa! Ang. Yer 6.14; 8.11

11Sasa uwaambie hao manabii wanaopakaa chokaa ukuta huo kwamba kutanyesha mvua kubwa ya mawe na zoruba itavuma na ukuta huo utaanguka.

12Utakapoanguka, watu hawatawauliza hivi: Na ile chokaa mulioupakaa iko wapi?

13Kwa hiyo Bwana wetu Yawe anasema: Kwa kasirani yangu nitazusha upepo wa zoruba na mvua nyingi ya mawe, navyo vitauangusha ukuta huo.

14Nitaubomoa kabisa huo ukuta mulioupakaa chokaa, na musingi wake utakuwa wazi. Ukuta huo ukianguka, mutaangamia chini yake. Halafu mutatambua kwamba mimi ni Yawe.

15Hasira yangu yote nitaimalizia juu ya ukuta huo na juu ya hao walioupakaa chokaa. Nanyi mutaambiwa: Ukuta haupo tena, wala walioupakaa rangi hawapo;

16huo ndio mwisho wa manabii wa Waisraeli waliotabiri mema juu ya Yerusalema na kuona maono ya amani ijapokuwa hakuna amani. Ni Bwana wetu Yawe anayesema hivyo.

Juu ya manabii wa kike wa uongo

17Na sasa, ewe mwanadamu, uwaelekee wanawake wa taifa lako ambao wanatabiri mambo ambayo wameyawaza wao wenyewe. Utabiri juu yao

18na kuwaambia kwamba Bwana wetu Yawe anasema hivi: Ole kwenu ninyi wanawake munaoshona vitepe vyenye hirizi ambavyo kila mutu anavivaa kwenye maunganio ya mikono na kutengeneza vitambaa vyenye hirizi za kila kimo kwa ajili ya watu wa kila umri. Munapowinda maisha ya watu wangu munazani kwamba mutaokoa maisha yenu wenyewe?

19Mumenizaraulisha mbele ya watu wangu kusudi mupate vitanga vya shayiri na chakula kidogo. Munawaua watu wasiostahili kufa na kuwaacha wazima wanaostahili kuuawa, kwa uongo wenu munaowaambia watu wangu, nao wanawaaminia.

20Basi, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Nitashambulia hirizi zenu munazowafunga nazo watu; nitazipasuapasua toka katika mikono yenu na kuwaacha huru hao munaowawinda kama ndege.

21Nitavirarua vitambaa vyenu na kuwaokoa watu wangu toka katika mikono yenu; nao hawatakuwa tena kama nyama wa kuwindwa katika mikono yenu. Halafu mutatambua kwamba mimi ni Yawe.

22Kwa sababu mumewavunja watu wa haki moyo kwa kusema uongo, ijapokuwa mimi sikuwavunja moyo, mukawaimarisha waovu wasiache mienendo yao mibaya na kuokoa maisha yao,

23basi, ninyi hamutapata tena maono madanganyifu, wala hamutatabiri tena. Nitawaokoa watu wangu toka katika mikono yenu. Halafu mutatambua kwamba mimi ni Yawe.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help