1Daudi akajengea nyumba katika muji wa Daudi. Tena akatengenezea Sanduku la Agano nafasi, akalipigia hema.
2Kisha akasema: “Hakuna mutu mwingine yeyote atakayebeba Sanduku la Agano isipokuwa Walawi, maana Yawe aliwachagua wao kwa kulibeba na kumutumikia kwa milele.”
3Basi, akawakusanya Waisraeli wote wakuje Yerusalema, kwa kuleta Sanduku la Agano la Yawe pahali alipolitayarishia.
4-10Hao ndio Walawi, wazao wa Haruni, ambao Daudi aliowaita kufuatana na ukoo zao:
Ukoo wa Kohati: Urieli na wandugu zake mia moja na makumi mbili chini ya usimamizi wake;
Ukoo wa Merari: Asaya na wandugu zake mia mbili na makumi mbili chini ya usimamizi wake;
Ukoo wa Gersoni: Yoeli na wandugu zake mia moja na makumi tatu chini ya usimamizi wake;
Ukoo ya Elisafani: Semaya na wandugu zake mia mbili chini ya usimamizi wake;
Ukoo wa Hebroni: Elieli na wandugu zake makumi munane chini ya usimamizi wake;
Ukoo wa Uzieli: Aminadabu na wandugu zake mia moja kumi na wawili, chini ya usimamizi wake.
11Daudi akawaita makuhani wawili, Zadoki na Abiatari, na Walawi sita, Urieli, Asaya, Yoeli, Semaya, Elieli na Aminadabu;
12akawaambia: “Ninyi ni viongozi wa ukoo za Walawi. Mujitakase pamoja na wandugu zenu, mupate kuleta Sanduku la Agano la Yawe, Mungu wa Israeli, mpaka pahali ambapo nimelitayarishia.
13Kwa sababu hamukulibeba safari ya kwanza, Yawe, Mungu wetu, akatuazibu maana hatukulitunza kama vile alivyoagiza.”
14Basi, makuhani na Walawi wakajitakasa kusudi wapate kuleta Sanduku la Agano la Yawe, Mungu wa Israeli.
15Walawi wakalibeba juu ya mabega yao wakitumia miti yake ya kuibebea kama Musa alivyoamuru, kulingana na neno la Yawe.
16Daudi aliwaamuru vilevile wakubwa wa Walawi wachague kati ya wandugu zao waimbaji wakuwe wanaimba na kupiga ala za muziki kwa nguvu, kwa kutoa sauti za furaha. Walipiga vinanda, vinubi na matoazi.
17Hivyo wakachagua watu hawa katika ukoo za waimbaji: Hemani mwana wa Yoeli, ndugu yake Asafu aliyekuwa mwana wa Berekia na wana wa Merari, ndugu zao, na Etani mwana wa Kusaya.
18Kisha wakawachagua Walawi hawa wakuwe wasaidizi wao kwa kushika nafasi ya pili: Zekaria, Yazieli, Semiramoti, Yehieli, Uni, Eliabu, Benaya, Maseya, Matitia, Elifelehu na Mikineya na walinzi wa mulango: Obedi-Edomu na Yeieli.
19Hemani, Asafu na Etani wakachaguliwa kupiga matoazi ya shaba.
20Zekaria, Azieli, Semiramoti, Yehieli, Uni, Eliabu, Maseya na Benaya, walikuwa wapiga vinubi vya sauti ya juu.
21Matitia, Elifelehu, Mikineya, Obedi-Edomu, Yeieli na Azazia waliongoza wakiwa na vinubi vya sauti ya chini.
22Naye Kenania kwa sababu ya ujuzi wa muziki aliokuwa nao, aliwekwa kuwa kiongozi wa wote.
23Berekia na Elekana walikuwa walinzi wa Sanduku la Agano.
24Sebania, Yosafati, Netaneli, Amasai, Zekaria, Benaya na Eliezeri, waliokuwa makuhani, waliwekwa kwa kupiga baragumu mbele ya Sanduku la Agano. Obedi-Edomu na Yehiya waliwekwa vilevile kuwa walinzi wa sanduku.
Sanduku la Agano linapelekwa Yerusalema(2 Sam 6.12-22)25Basi, Daudi, wazee wa Waisraeli na majemadari wa maelfu, wakaenda kutwaa Sanduku la Agano la Yawe kutoka katika nyumba ya Obedi-Edomu kwa shangwe.
26Wakamutolea Mungu sadaka: ngombe dume saba na kondoo dume saba kwa sababu aliwasaidia wale Walawi waliolibeba Sanduku la Agano la Yawe.
27Daudi alikuwa akivaa kanzu ya kitani safi, hata vilevile na Walawi wote waliobeba sanduku, waimbaji na Kenania kiongozi wa waimbaji. Zaidi ya kanzu ile, Daudi alikuwa akivaa kizibao cha kitani.
28Hivyo, Waisraeli wote wakakusanyika pamoja kwa shangwe kwa kubeba Sanduku la Agano la Yawe mpaka Yerusalema. Wakalisindikiza kwa mulio wa baragumu, ngunga, matoazi, na sauti kubwa za vinanda na vinubi.
29Sanduku la Agano la Yawe lilipokuwa likiingia katika muji wa Daudi, Mikali, binti wa Saulo, akachungulia kwenye dirisha, akamwona mufalme Daudi akicheza na kushangilia, basi akamuzarau ndani ya moyo wake.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.