1Kwa hiyo wandugu zangu wapendwa, niko na hamu sana ya kuwaona tena. Ninyi ndio munaokuwa furaha yangu na zawadi ya ushindi nitakayopokea. Ninyi wapendwa wangu, ninawaomba musimame imara katika ushirika wenu na Bwana.
2Ninakusihi wewe Ewodia na wewe Sintike, muishi katika masikilizano mbele ya Bwana.
3Na wewe vilevile mutumishi mwenzangu mwaminifu, ninakuomba uwasaidie wanawake hao, kwa maana walisumbuka sana pamoja nami katika kazi ya kutangaza Habari Njema. Kuko vilevile Klementi na wenzangu wengine wa kazi. Hao wote majina yao yameandikwa katika kitabu cha uzima.
4Mufurahi siku zote katika kuungana kwenu na Bwana. Na tena ninasema: Mufurahi!
5Muonyeshe upole wenu kwa watu wote, kwa maana Bwana yuko karibu kurudia.
6Musijisumbue juu ya neno lolote, lakini katika kila neno mutoe mahitaji yenu kwa Mungu, mukimwomba, mukimusihi na kumushukuru.
7Na amani ya Mungu inayopita ufahamu wa mutu yeyote, italinda mioyo yenu na nia zenu salama katika kuungana kwenu na Yesu Kristo.
8Kwa kumaliza, wandugu zangu, muweke mafikiri yenu juu ya mambo yote yanayokuwa ya kweli, ya heshima, ya haki, safi, ya kupendeza, nayo mambo yote yanayostahili sifa na ya utu wema.
9Mushike mambo yote muliyojifunza na kupokea toka kwangu, nayo yote muliyosikia na kuona kwangu. Naye Mungu wa amani atakuwa pamoja nanyi.
Paulo anatoa shukrani kwa Wafilipi10Nilipata furaha kubwa katika kuungana na Bwana kwa kuona munakumbuka tena kunisaidia. Sitaki kusema kwamba mulinisahau, lakini hamukupata wakati wa kuonyesha kwamba munanishugulikia.
11Na sisemi hivi kwa sababu ninakosewa na kitu, kwa maana ninajizoeza kufurahi na kile ninachokuwa nacho.
12Ninajua kuishi katika ukosefu na ninajua kuishi katika utajiri. Nimejizoeza kufurahi fasi zote na katika kila hali: ikiwa hali ya kuwa na vyakula kwa uwingi au ya njaa, ikiwa hali ya utajiri au ya ukosefu.
13Ninaweza vyote kwa njia ya Kristo anayenitia nguvu.
14Lakini, mumefanya vizuri kwa kushirikiana pamoja nami katika taabu yangu.
15Ninyi Wafilipi munajua vizuri wenyewe kwamba nilipotoka Makedonia, tangu mwanzo wa kuhubiri Habari Njema, ni ninyi tu ndilo kanisa moja lililoshirikiana nami katika mambo ya utoaji na upokeaji.
16Hata wakati wote nilipokuwa Tesalonika, mulinitumia musaada mara nyingi juu ya mahitaji yangu.
17Sitaki kusema kwamba ninatafuta tu kupokea zawadi, lakini ninataka faida iongezwe kwa upande wenu.
18Kweli nina vitu vyote vya lazima na zaidi kupita. Sasa kwa kuwa Epafrodito ameniletea zawadi zenu zote, ninatosheka. Zawadi hizi ni kama sadaka ya ubani yenye harufu nzuri, na kama sadaka ya kuteketezwa kwa moto inayokubaliwa na Mungu na kumupendeza.
19Basi, kwa njia ya Yesu Kristo, Mungu wangu atatimiza mahitaji yenu yote kufuatana na uwingi na utukufu wa utajiri wake.
20Mungu Baba yetu atukuzwe kwa milele na milele. Amina.
Salamu za mwisho21Musalimie watu wote wa Mungu wanaomwamini Yesu Kristo. Wandugu wanaokuwa pamoja nami wanawasalimia.
22Watu wote wa Mungu, na hasa zaidi wale wanaokuwa katika nyumba ya Mufalme, wanawasalimia vilevile.
23Ninawatakia ninyi wote neema kutoka kwa Bwana wetu Yesu Kristo.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.