Kutoka 37 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Kutengeneza Sanduku la Agano(Kut 25.10-22)

1Bezaleli akatengeneza sanduku kwa mbao za mujohoro. Urefu wake ulikuwa sentimetre mia moja na kumi, upana sentimetre makumi sita na sita, na urefu kwenda juu sentimetre makumi sita na sita.

2Akalipakaa zahabu safi ndani na inje na kulifanyia ukingo wa zahabu pande zote.

3Kisha akatengeneza pete ine za zahabu za kulibebea, akazitia kwenye pembe zake, kila pembe pete moja.

4Akatengeneza miti ya mujohoro na kuipakaa zahabu.

5Miti hiyo akaipitisha katika zile pete zinazokuwa katika pande mbili za sanduku, kwa ajili ya kulibebea.

6Akatengeneza kiti cha rehema cha zahabu safi; urefu wake sentimetre mia moja na kumi na upana wake sentimetre makumi sita na sita.

7Akatengeneza vilevile makerubi wawili kwa kufua zahabu kwenye miisho ya kifuniko hicho;

8kerubi mumoja mwisho huu na mwingine mwisho mwingine. Akatengeneza makerubi wale kwenye miisho ya kifuniko hicho, wakikuwa kitu kimoja na kifuniko.

9Makerubi wale walikuwa wakielekeana, mabawa yao yakikunjuliwa na kukifunika kifuniko cha sanduku, nyuso zao zilikielekea kifuniko cha sanduku.

Meza ya mikate ya sadaka(Kut 25.23-30)

10Vilevile akatengeneza meza ya mujohoro yenye urefu wa sentimetre makumi nane na nane, upana sentimetre makumi ine na ine, na urefu kwenda juu sentimetre makumi sita na sita.

11Akapakaa zahabu safi na kuitengenezea ukingo wa zahabu.

12Akaizungushia ubao wenye upana wa milimetre makumi saba na tano, na kuifanyia ukingo wa zahabu.

13Akaitengenezea pete ine za zahabu na kuzitia katika pembe zake ine pahali miguu ilipoishia.

14Pete hizo za kushikilia ile miti ya kuibebea ziliwekwa karibu na ule muzunguko wa ubao.

15Akatengeneza miti miwili ya mujohoro ya kuibebea, akaipakaa zahabu.

16Akatengeneza vyombo vya zahabu safi vya kuweka juu ya meza: sahani zake na visahani kwa ajili ya ubani, na bilauri zake na bakuli kwa ajili ya sadaka za kinywaji.

Kinara cha taa(Kut 25.31-40)

17Akatengeneza vilevile kinara cha taa kwa zahabu safi. Tako lake na muti wa hicho kinara ulikuwa kitu kimoja pamoja na vikombe vyake, vifundo vyake na maua yake.

18Matawi sita yalitokeza kila upande wa muti wake, matawi matatu upande mumoja na matawi matatu upande mwingine.

19Katika kila tawi kulikuwa vikombe vitatu mufano wa maua ya lozi, kila kimoja na kifundo chake na ua lake.

20Na katika muti kulikuwa vikombe vine mufano wa maua ya lozi, pamoja na vifundo vyake na maua yake.

21Kulikuwa kifundo kila pahali matawi mawilimawili yalipotokea kufuatana na yale matawi sita yanayotoka kwa kile kinara.

22Vifundo hivyo na matawi vilikuwa kitu kimoja na kinara hicho na chote kilifuliwa kwa zahabu safi.

23Akatengeneza taa zake saba, koleo zake na visahani vyake kwa zahabu safi.

24Akatengeneza kinara hicho na vifaa vyake kwa kilo makumi tatu na tano za zahabu.

Mazabahu ya kufukizia ubani(Kut 30.1-5)

25Akatengeneza mazabahu ya kufukizia ubani kwa mbao za mujohoro. Mazabahu hiyo ilikuwa ya muraba, sentimetre makumi ine na tano kwa sentimetre makumi ine na tano, na urefu kwenda juu sentimetre makumi tisa. Pembe za mazabahu hiyo zilikuwa kitu kimoja na mazabahu yenyewe.

26Yote aliipakaa zahabu safi: upande wake wa juu, pande zake za ubavu na pembe zake. Vilevile akaitengenezea ukingo wa zahabu.

27Akatengeneza pete mbili za zahabu chini ya ukingo kwenye pande mbili zinazoelekeana. Pete hizo zilitumika kushikilia miti ya kuibebea.

28Akafanya miti miwili ya mujohoro na kuipakaa zahabu.

29Akatengeneza mafuta matakatifu ya kupakaa na ubani safi wenye harufu nzuri uliochanganywa vizuri kama manukato.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help