1Nyuma ya kifo cha Yoshua, Waisraeli walimwuliza Yawe: “Ni kabila gani litakwenda kupigana kwanza na Wakanana?”
2Yawe akawajibu: “Kabila la Yuda litakwenda kupigana nao kwanza, maana nimeitia inchi hiyo katika mikono yao.”
3Watu wa kabila la Yuda wakawaambia wandugu zao, watu wa kabila la Simeoni: “Mushirikiane nasi tunapokwenda kuitwaa inchi hiyo ambayo tumepewa. Nasi, vilevile tutashirikiana nanyi kwenda kuitwaa inchi mutakayopewa.” Hivyo kabila la Simeoni likakubali kushirikiana nao.
4Basi watu wa kabila la Yuda wakaenda kufanya mashambulio, naye Yawe akawatia Wakanana na Waperizi katika mikono yao, wakawaua watu elfu kumi katika vita kule Bezeki.
5Katika muji ule wakamukuta mufalme Adoni-Bezeki, wakapigana naye na kuwashinda Wakanana na Waperizi.
6Adoni-Bezeki akakimbia, lakini walimufuatilia, wakamukamata, wakamukata vidole gumba vya mikono na miguu.
7Adoni-Bezeki akasema: “Wafalme makumi saba waliokatwa vidole gumba vya mikono na miguu waliokota makombo chini ya meza yangu. Sasa Mungu amenilipa kama nilivyotenda.” Wakamupeleka Yerusalema, akakufia kule.
8Watu wa kabila la Yuda waliushambulia Yerusalema na kuuteka. Waliwaua wakaaji wake kwa mapanga na kuuteketeza muji kwa moto.
9Kisha, watu wa kabila la Yuda wakakwenda kupigana na Wakanana walioishi kwenye inchi ya milima, Negebu na kwenye inchi ya bonde.
10Waliwashambulia vilevile Wakanana walioishi katika muji wa Hebroni ambao zamani uliitwa Kiriati-Arba, wakashinda makabila ya Sesai, Ahimani na Talmayi.
11Kutoka kule watu wa kabila la Yuda walikwenda kuushambulia muji wa Debiri; ambao zamani uliitwa Kiriati-Seferi.
12Kalebu akatangaza: “Mutu yeyote atakayeshinda na kuuteka muji wa Kiriati-Seferi, nitamupa binti yangu Akisa kuwa muke wake.”
13Basi, Otinieli mwana wa Kenazi na mudogo wa Kalebu, akauteka, naye Kalebu akamutoa binti yake Akisa aolewe na Otinieli.
14Akisa alipofika kwa Otinieli, akamwambia Otinieli amwombe baba yake Kalebu shamba. Akisa alikuwa amepanda juu ya punda na aliposhuka chini baba yake akamwuliza: “Ungependa nikupe nini?”
15Akamujibu: “Unipe zawadi! Ninaomba unipe chemichemi za maji maana kule upande wa kusini ni jangwa.” Kalebu akamupa chemichemi za upande wa juu na za chini.
16Wazao wa Keni ambaye alikuwa baba mukwe wa Musa, walifuatana na watu wa kabila la Yuda kutokea Muji wa Miti ya Ngazi, ni kusema muji wa Yeriko, mpaka jangwa la Yuda karibu na Aradi, wakafanya makao yao kule pamoja na watu wa Yuda.
17Watu wa kabila la Yuda walishirikiana na wandugu zao, watu wa kabila la Simeoni, wakawashinda Wakanana waliokaa Sefati. Wakaangamiza kabisa muji ule na kugeuza jina lake kuwa Horma, ni kusema “Maangamizo”.
18Watu wa kabila la Yuda vilevile waliteka miji ya Gaza na eneo lake, Askeloni na eneo lake, na Ekuroni na eneo lake.
19Yawe alikuwa pamoja na watu wa kabila la Yuda, nao wakaiteka inchi ya milima. Lakini hawakuweza kuwashinda wenyeji wa inchi ya bonde kwa sababu magari yao ya vita yalikuwa ya chuma.
20Muji wa Hebroni ukapewa kwa Kalebu kufuatana na maagizo ya Musa. Kalebu akazifukuza kutoka kule ukoo tatu za Anaki.
21Lakini watu wa kabila la Benjamina hawakuwafukuza Wayebusi waliokaa katika Yerusalema; ndiyo maana Wayebusi wanakaa pamoja na watu wa kabila la Benjamina katika Yerusalema mpaka leo.
22Watu wa makabila ya Yosefu waliushambulia muji wa Beteli, naye Yawe alikuwa pamoja nao.
23Kwanza walikuwa wamewatuma wapelelezi kwenda kuupeleleza muji wa Beteli. Muji ule zamani uliitwa Luzi.
24Wapelelezi hao walimwona mutu mumoja akitoka katika muji, wakamwambia: “Tafazali, utuonyeshe njia inayoingia katika muji, nasi tutakutendea mema.”
25Akawaonyesha njia ya kuingia katika muji. Basi, wakaingia na kuangamiza kila mutu aliyekuwa mule. Lakini wakamwacha salama mutu yule na jamaa yake.
26Mutu yule akahamia katika inchi ya Wahiti, kule akajenga muji ambao aliuita Luzi, na muji huo unaitwa hivyo mpaka leo.
27Watu wa kabila la Manase hawakuwafukuza wakaaji wa miji ya Beti-Seani na vijiji vyake, Tanaki na vijiji vyake, Dori na vijiji vyake, Ibileamu na vijiji vyake, na Megido pamoja na vijiji vyake. Wakanana waliendelea kukaa kule.
28Hata Waisraeli walipokuwa na nguvu hawakuwafukuza Wakanana lakini waliwapa kazi za kulazimishwa.
29Watu wa kabila la Efuraimu hawakuwafukuza Wakanana walioishi kule Gezeri, na hawa waliishi kule pamoja na watu wa Efuraimu.
30Watu wa kabila la Zebuluni hawakuwafukuza wakaaji wa muji wa Kitironi, wala wale wa muji wa Nahalali, waliendelea kukaa pamoja nao wakiwatumikisha kazi za kulazimishwa.
31Watu wa kabila la Aseri hawakuwafukuza wakaaji wa miji ya Ako, Sidona, Alabu, Akizibu, Helba, Afika na Rehobu.
32Watu wa kabila la Aseri walikaa pamoja na Wakanana wenyeji wa inchi hiyo maana hawakuwafukuza.
33Watu wa kabila la Nafutali hawakuwafukuza wakaaji wa muji wa Beti-Semesi au wakaaji wa Beti-Anati, lakini walikaa pamoja nao. Hata hivyo wenyeji wa miji hiyo walitumikishwa kazi za kulazimishwa.
34Waamori waliwafukuzia watu wa kabila la Dani kwenye milima. Hawakuwaruhusu kuja kuishi katika inchi ya bonde.
35Waamori waliendelea kuishi katika miji iliyokuwa katika kilima cha Heresi, Ayaloni na Salabimu. Lakini watu wa makabila ya Manase na Efuraimu waliwatawala Waamori na kuwatumikisha kazi za kulazimishwa.
36Mupaka wa Waamori ulikuwa upande wa kaskazini ya Sela, kupitia njia inayopanda kwenda Akarabimu.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.