1Yawe anasema hivi:
Nitavumisha upepo wa kuangamiza juu ya Babeli
na juu ya wakaaji wa Kaldea.
2Nitawapeleka wapepetaji katika inchi ya Babeli,
nao watamupepeta;
watamaliza kila kitu katika inchi yake
watakapofika kuishambulia toka kila upande
wakati wa maangamizi yake.
3Usiwape nafasi wapiga mushale wa Babeli;
usiwaache wavute upinde,
wala kuvaa nguo zao za vita.
Usiwahurumie vijana wake;
uangamize kabisa jeshi lake.
4Wataanguka na kuuawa katika inchi ya Wakaldea,
wataumizwa katika barabara zake.
5Lakini Israeli na Yuda hawakuachiliwa
na Mungu wao, Yawe wa majeshi,
ingawa inchi yao imejaa makosa
mbele ya Mutakatifu wa Israeli.
6Mukimbie kutoka Babeli,
kila mutu apate kuyaokoa maisha yake!
Musiangamizwe katika azabu yake,
maana huu ndio wakati wa Mungu wa kulipiza kisasi,
anaiazibu Babeli kama inavyostahili.
7Babeli ilikuwa kikombe cha zahabu
katika mukono wa Yawe,
ambacho kiliilewesha dunia nzima.
Mataifa yalikunywa divai yake;
kwa hiyo, yakapata wazimu.
8Kwa rafla Babeli imeanguka na kuvunjikavunjika;
muomboleze kwa ajili yake!
Mulete dawa kwa kutuliza maumivu yake;
labda utaweza kupona.
9Tulijaribu kuuponyesha Babeli,
lakini hauwezi kupona.
Muuache, tujiendee,
kila mumoja katika inchi yake.
Hukumu yake ni kubwa sana
inafika mpaka katika mawingu.
10Yawe amehakikisha kwamba hatuna kosa.
Tuende Sayuni tutangaze
matendo ya Yawe, Mungu wetu.
11Yawe amezichochea roho za wafalme wa Wamedi, kwa maana amekusudia kuiangamiza Babeli. Kweli, hicho ndicho kisasi cha Yawe; analipiza kisasi kwa ajili ya hekalu lake.
Munoe mishale yenu!
Mutwae ngao!
12Mupandishe bendera ya vita
kwa kushambulia kuta za Babeli.
Muimarishe walinzi,
muweke walinzi,
mutayarishe mashambulizi.
Yawe amepanga na kutimiza
mambo aliyosema juu ya wakaaji wa Babeli.
13Inchi hiyo imejaa mito na akiba tele,
lakini mwisho wake umefika,
uzi wa uzima wake umekatwa.
14Yawe wa majeshi ameapa kwa nafsi yake:
Hakika nitakujaza na watu kama vile nzige,
nao watapiga vigelegele vya ushindi juu yako.
15Yawe ndiye aliyeumba dunia kwa nguvu zake,
aliyeuimarisha ulimwengu kwa hekima yake,
na kwa akili yake akazitandaza mbingu.
16Anapotoa sauti yake maji yanajikusanya mbinguni,
anafanya ukungu upande kutoka mipaka ya dunia.
Anafanya umeme upige wakati wa mvua,
anavumisha upepo kutoka gala zake.
17Kila mutu ni mupumbafu bila maarifa,
kila mufua vyuma anapatishwa haya na miungu yake;
maana sanamu zake ni udanganyifu mutupu,
wala hazina pumzi ndani yake.
18Hazina maana, ni udanganyifu mutupu;
wakati watakapoazibiwa, nazo zitaangamia.
19Mungu anayekuwa hazina ya Yakobo si kama hizo,
maana yeye ndiye aliyeviumba vitu vyote,
na Israeli ni kabila linalokuwa mali yake;
Yawe wa majeshi, ndilo jina lake.
Mwisho wa Babeli20Yawe anasema hivi:
Wewe Babeli ni nyundo na silaha yangu ya vita;
ninakutumia kwa kuyavunjavunja mataifa,
ninakutumia kwa kuangamiza falme.
21Ninakutumia kwa kuponda farasi na waaskari wapanda-farasi,
magari ya kukokotwa na watembezaji wake.
22Ninakutumia kwa kuwaponda wanaume na wanawake,
wazee na vijana,
vijana wanaume na wabinti.
23Ninakutumia kwa kuponda wachungaji na makundi yao,
walimaji na nyama wao wanaotumia kwa kulima,
wakubwa na maliwali.
24Nitaiazibu Babeli na wakaaji wote wa Kaldea mukiona kwa macho yenu wenyewe, kwa sababu ya uovu wote walioufanya katika Sayuni. –Ni ujumbe wa Yawe.
25Mimi ninapingana nawe, ewe mulima muharibifu,
mulima unaoharibu dunia nzima!
–Ni ujumbe wa Yawe.–
Nitanyoosha mukono wangu juu yako kwa kukuazibu,
nitakuangusha kutoka juu kwenye mawe makubwa
na kukufanya kuwa mulima uliochomwa kwa moto.
26Kwako hakutapatikana jiwe la kujenga,
hata jiwe kwa kujenga musingi!
Utakuwa kama jangwa milele.
–Ni ujumbe wa Yawe!–
27Pandisha bendera ya vita katika dunia,
piga baragumu kati ya mataifa;
uyatayarishe mataifa kwa kupigana naye;
uziite falme kwa kuishambulia;
falme za Ararati, Mini na Askenazi.
Weka jemadari juu yake;
ulete farasi kama makundi ya nzige.
28Mutayarishe mataifa kwa kupigana naye vita;
muwatayarishe wafalme wa Medi, watawala na maliwali wao,
mutayarishe inchi zote katika utawala wao.
29Inchi inatetemeka na kugaagaa kwa maumivu,
maana nia ya Yawe juu ya Babeli ni imara:
ataifanya inchi ya Babeli kuwa jangwa,
ataifanya ikuwe bila watu.
30Waaskari wa Babeli wameshindwa kupigana,
wamebaki katika makimbilio yao;
nguvu zao zimewaishia,
wamekuwa kama wanawake.
Nyumba za Babeli zimechomwa kwa moto,
milango yake ya chuma imevunjwa.
31Wakimbiaji wanakimbia
wakitoleana ujumbe mumoja kwa mwingine
kwa kumupasha mufalme wa Babeli habari
kwamba muji wake umeshambuliwa kila upande.
32Vivuko vya muto vimetekwa,
makimbilio yamechomwa kwa moto,
waaskari wamepatwa na hofu.
33Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi:
Babeli ni kama uwanja wa kupepetea ngano
wakati unapotayarishwa.
Lakini bado kidogo tu,
wakati wa mavuno utaufikia.
34Mufalme Nebukadneza wa Babeli
aliuharibu na kuuponda Yerusalema
aliuacha kama chungu kitupu;
aliumeza kama vile nyoka mukubwa.
Alijaza tumbo lake vitu vyake vizurivizuri,
akautupilia mbali kama matapiko.
35Watu wa Sayuni watasema:
Babeli ulipizwe mateso makali yaleyale
tuliyotendewa sisi pamoja na jamaa zetu!
Yerusalema itasema:
Damu yangu ikuwe juu ya wakaaji wa Kaledea.
Yawe atasaidia36Kwa hiyo Yawe anasema hivi:
Nitawatetea juu ya maneno yenu,
na kulipiza kisasi kwa ajili yenu.
Nitaikausha bahari ya Babeli
na kuvifanya visima vyake vikauke.
37Babeli itakuwa lundo la mabomoko,
itakuwa makao ya mbweha,
itakuwa machukizo na kitu cha kuzomewa;
hakuna mutu atakayekaa ndani yake.
38Wababeli watanguruma pamoja kama simba;
watalia kama wana-simba.
39Wakiwa na hamu kubwa
nitawatayarishia karamu:
nitawalewesha mpaka wapepesuke;
nao watalala usingizi wa siku zote
na hawataamuka tena.
–Ni ujumbe wa Yawe.–
40Nitawashusha chini kama kondoo wa kuchinjwa,
kama vile kondoo dume na beberu.
41Namna gani Babeli imetekwa;
muji uliosifiwa katika dunia yote umekamatwa!
Babeli umekuwa ukiwa kati ya mataifa!
42Bahari imefurika juu ya Babeli,
Babeli imefunikwa na mawimbi yaliyochafuka.
43Miji yake imekuwa ukiwa,
inchi yenye kukauka na jangwa,
inchi isiyokaliwa na mutu yeyote,
wala hakuna mwanadamu yeyote anayepita ndani yake.
44Nitamwazibu mungu Beli huko Babeli,
nitamutapikisha kile alichomeza.
Mataifa hayatamwendea tena kwa wingi.
Ukuta wa Babeli umebomoka.
45Mutoke humo, enyi watu wangu!
Kila mutu apate kuyaokoa maisha yake,
kutoka hasira kali ya Yawe.
46Musiregee wala musikuwe na hofu,
kwa sababu ya habari munazosikia katika inchi.
Mwaka huu kuna habari hii,
mwaka mwingine habari ingine;
habari ya mateso makali katika inchi,
mutawala mumoja anapigana na mutawala mwingine.
47Kwa hiyo, siku zinakuja
ambapo nitaazibu sanamu za Babeli;
inchi yake yote itapata haya,
watu wake wote watauawa humohumo.
–Ni ujumbe wa Yawe.–
48Kisha mbingu, dunia na vyote vinavyokuwa ndani yao
vitaimba kwa furaha juu ya kuanguka kwa Babeli,
wakati waangamizaji watakapofika kutoka upande wa kaskazini kuushambulia.
–Ni ujumbe wa Yawe.–
49Babeli umesababisha vifo katika dunia yote;
sasa muji wenyewe utaangamizwa kwa ajili ya mauaji ya Waisraeli.
50Ninyi mulioponyoka kifo,
muondoke sasa, wala musisitesite!
Ingawa muko katika inchi ya mbali, mumukumbuke Yawe,
muukumbuke vilevile Yerusalema.
51Ninyi munasema: Tumepatishwa haya na kutukaniwa;
haya imefunika nyuso zetu,
kwa sababu wageni wameingia
katika sehemu takatifu za nyumba ya Yawe.
52Kwa hiyo, siku zinakuja
ambapo nitaiazibu miungu ya Babeli,
na wenye kuumizwa watalalamika katika inchi yake yote.
–Ni ujumbe wa Yawe.–
53Ingawa Babeli ungepanda mpaka mbinguni,
na kuziimarisha kuta zake ndefu,
waangamizaji watakuja kutoka kwangu kwa kuuharibu.
–Ni ujumbe wa Yawe.
Maangamizi zaidi juu ya Babeli54Sikiliza! Kilio kinasikilika kutoka Babeli!
Kishindo cha maangamizi makubwa
kutoka inchi ya Wakaldea!
55Maana mimi Yawe ninaiangamiza Babeli,
na kuikomesha kelele yake kubwa.
Waadui wananguruma kama mawimbi ya maji mengi,
sauti ya kishindo chao inaongezeka.
56Kweli, mwangamizaji anashambulia Babeli;
waaskari wake wametekwa,
pinde zao zimevunjwavunjwa.
Mimi Yawe ni Mungu mwenye kuazibu,
hakika mimi nitalipiza kisasi kamili.
57Nitawalewesha wakubwa na wenye hekima wake,
watawala wake, maliwali na waaskari wake;
watalala usingizi wa milele wala hawataweza tena kuamuka.
–Ni ujumbe wa mufalme, jina lake Yawe wa majeshi!
58Yawe wa majeshi anasema hivi:
Ukuta mukubwa wa Babeli
utabomolewa mpaka chini,
na milango yake mirefu
itateketezwa kwa moto.
Watu wanafanya juhudi za bure,
mataifa yanajichokesha,
maana mwisho wao ni katika moto!
Ujumbe wa Yeremia unapelekwa Babeli59Katika mwaka wa ine wa utawala wake, mufalme Zedekia alikwenda Babeli pamoja na mukubwa wa wasimamizi wa nyumba yake anayeitwa Seraya mwana wa Neria na mujukuu wa Maseya. Wakati huo mimi Yeremia nilimutolea Seraya ujumbe.
60Nilikuwa nimeandika katika kitabu hasara yote niliyotangaza juu ya Babeli na vilevile maneno mengine juu ya Babeli.
61Nilimwambia Seraya: Utakapofika Babeli ni lazima uwasomee wote maneno haya.
62Kisha umalizie na maneno haya: Ee Yawe, wewe umesema kwamba utaharibu nafasi hii hata kusikaliwe na kiumbe chochote, mwanadamu au nyama, na kwamba inchi hii itakuwa jangwa milele.
63Utakapomaliza kusoma kitabu hiki, ufunge jiwe juu yake, kisha ukitumbukize katikati ya muto Furati, ukisema:
64Hivi ndivyo Babeli utakavyozama, wala hautainuka tena, kwa sababu ya hasara ambayo Yawe anauletea. Huu ndio mwisho wa maneno ya Yeremia.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.