Walawi 11 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Nyama wanaoruhusiwa kukuliwa na wasioruhusiwa kukuliwa(Kumb 14.3-21)

1Yawe akawaambia Musa na Haruni:

2Wawaambie Waisraeli hivi:

3Kati ya nyama wote katika dunia, mumeruhusiwa kula nyama yeyote mwenye kwato zinazogawanyika sehemu mbili na ambaye anacheua.

4Lakini musikule nyama yeyote ambaye anacheua lakini kwato zake hazigawanyiki sehemu mbili, au ambaye kwato zake zimegawanyika lakini hacheui. Musikule ngamia, maana anacheua lakini kwato zake hazigawanyiki sehemu mbili. Kwenu huyo ni muchafu.

5Musikule wibari. Yeye anacheua lakini kwato zake hazigawanyiki. Kwenu huyo ni muchafu.

6Musikule sungura. Yeye anacheua lakini kwato zake hazigawanyiki. Kwenu huyo ni muchafu.

7Musikule nguruwe. Yeye ana kwato zinazogawanyika lakini hacheui. Kwenu huyo ni muchafu.

8Kwa sababu nyama hao ni wachafu, musikule nyama yao wala musiguse mizoga yao.

9Samaki yeyote wa bahari au muto mwenye mapezi na magamba, munaweza kumukula.

10Lakini chochote kinachoishi katika bahari au ndani ya mito, ambacho hakina mapezi wala magamba, maana viumbe vyote vinavyotembea ndani ya maji na viumbe vingine vyote vinavyoishi ndani ya maji ni vichafu kwenu.

11Viumbe hivyo vitakuwa siku zote vichafu kwenu. Musikule nyama yao, wala musiguse mizoga yao maana ni chafu.

12Chochote kinachoishi ndani ya maji ambacho hakina mapezi na magamba ni kichafu kwenu.

13Ndege hawa wote ni wachafu kwenu. Kwa hiyo, musiwakule: tai, furukombe, kipungu,

14mwewe, aina zote za kozi,

15aina zote za kibombobombo,

16mbuni, kirukanjia, dudumizi, aina zote za kipanga,

17bundi, munandi, bundi kubwa,

18mumbi, mwari, muderi,

19korongo, aina zote za koikoi, hudihudi na popo.

20Wadudu wote wenye mabawa na wanaotembea kwa miguu mine, hao ni wachafu kwenu.

21Lakini, kati ya wadudu wenye mabawa na wanaotembea kwa miguu mine mirefu kwa kurukia juu ya udongo munaweza kula.

22Hao ni: kila aina ya nzige, kila aina ya senene, kila aina ya panzi na kila aina ya parare.

23Lakini wadudu wengine wote wenye mabawa na miguu mine ni wachafu kwenu.

24Kugusa nyama fulanifulani kunamufanya mutu kuwa muchafu. Yeyote atakayegusa mizoga yao atakuwa muchafu mpaka magaribi.

25Mutu akitwaa sehemu ya mizoga yake atakuwa muchafu mpaka magaribi na nguo zake zinapaswa kufuliwa.

26Mutu yeyote akigusa nyama mwenye kwato zinazogawanyika lakini hacheui, mutu yule atakuwa muchafu.

27Nyama wote wanaotembelea kwa vitanga vyao ingawa wana miguu mine, ni wachafu kwenu na yeyote atakayegusa muzoga wa nyama kama huyo atakuwa muchafu mpaka magaribi.

28Mutu yeyote anayebeba muzoga atakuwa muchafu mpaka magaribi, naye atasafisha nguo zake. Hao ni wachafu kwenu.

29Viumbe hivi ni vichafu kwenu: fuko, panya, kila aina ya mujusi,

30guruguru, kenge, mijusi, mbulu, na kigeugeu.

31Hao wote ni wachafu kwenu na yeyote atakayegusa mizoga yao, atakuwa muchafu mpaka magaribi.

32Ikiwa muzoga wa viumbe hao unaangukia kitu chochote, kikuwe ni kifaa cha mbao au nguo au ngozi au gunia au chombo chochote kinachotumiwa kwa kazi yoyote, chombo hicho kitakuwa kichafu mpaka magaribi. Kwa kukifanya kikuwe safi kinapaswa kusafishwa kwa maji.

33Ikiwa muzoga wake umeangukia chombo cha udongo, basi, kitu chochote kilicho ndani ya chombo hicho ni kichafu na chombo hicho kinapaswa kuvunjwa.

34Chakula au kinywaji chochote kilichokuwa ndani ya chombo hicho kitakuwa kichafu.

35Kila kitu ambacho sehemu ya muzoga imekiangukia, kitakuwa kichafu. Ikiwa ni furu au jiko, kinapaswa kuvunjwa. Vitakuwa vichafu navyo ni vichafu kwenu.

36Hata hivyo, kisima au chemichemi ya maji vitakuwa safi. Lakini kitu chochote kinachogusa muzoga kitakuwa kichafu.

37Ikiwa sehemu ya muzoga inaangukia mbegu za kupanda, mbegu hizo hazitakuwa chafu.

38Lakini ikiwa mbegu zimetiwa katika maji kwa kuota na sehemu yoyote ya muzoga ikaziangukia, basi, mbegu hizo ni chafu kwenu.

39Ikiwa nyama yeyote munayeruhusiwa kula, anakufa mwenyewe, yeyote atakayegusa muzoga wake, atakuwa muchafu mpaka magaribi.

40Mutu yeyote akikula nyama ya muzoga huo atafua nguo yake na atakuwa muchafu mpaka magaribi. Na yeyote atakayebeba muzoga huo, atafua nguo zake, naye atakuwa muchafu mpaka magaribi.

41Kiumbe chochote kinachotambaa katika dunia ni chukizo kwenu, musikikule.

42Chochote kinachotambaa kwa tumbo lake, chochote kinachotembea kwa miguu mine au miguu mingi, musikikule kwa maana ni chukizo.

43Hivyo musijifanye kuwa chukizo kwa kula viumbe vinavyotambaa na hivyo kujichafua navyo.

44Kwa sababu mimi ni Yawe, Mungu wenu, mujitakase na kuwa watakatifu kwa maana mimi ni mutakatifu. Wala musijichafue na kitu chochote kinachotambaa juu ya inchi. Ang. Law 19.2; 1 Pet 1.16

45Kwa sababu ni mimi Yawe niliyewatoa katika inchi ya Misri kusudi nikuwe Mungu wenu; kwa hiyo mukuwe watakatifu kwa maana mimi ni mutakatifu.

46Hiyo basi, ndiyo sheria kuelekea nyama, ndege na viumbe vyote vyenye uzima ambavyo vinaishi ndani ya maji na inchi kavu,

47kwa kutia tofauti kati ya kisichokuwa kichafu na kinachokuwa kichafu, kinachoweza kukuliwa na kisichoweza kukuliwa.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help