1Siku ileile, mufalme Ahasuero akamupatia malkia Esteri mali yote ya Hamani, adui ya Wayuda. Esteri akamujulisha mufalme kwamba Mordekayi ni ndugu yake. Basi, tangu wakati ule, Mordekayi akaruhusiwa kumwona mufalme.
2Mufalme akaivua pete yake ya muhuri aliyokuwa amemunyanganya Hamani, akamupa Mordekayi. Esteri naye akamupa Mordekayi mamlaka juu ya mali ya Hamani.
3Kisha Esteri akazungumuza tena na mufalme; akajitupa chini, kwenye miguu ya mufalme, naye akilia, akamusihi mufalme aukomeshe mupango mubaya ambao Hamani, wa uzao wa Agagi, alikuwa amepanga juu ya Wayuda.
4Mufalme akamunyooshea Esteri fimbo yake ya zahabu, naye Esteri akasimama na kusema:
5“Ikikupendeza, ewe mufalme, na kama nimepata kukubaliwa mbele yako, ukiona ni vizuri nami nikikupendeza, tafazali, toa tangazo la kuvunja mipango ambayo Hamani alikuwa ameamuru itimizwe. Mipango hiyo ni ile ya mwana wa Hamedata, wa uzao wa Agagi, aliyopanga kwa kuwaangamiza Wayuda wote katika majimbo yote.
6Maana, ninaweza namna gani kuvumilia kuona watu wangu wanaangamizwa na wandugu zangu wanauawa?”
7Mufalme Ahasuero akawaambia malkia Esteri na Mordekayi, yule Muyuda: “Muangalie! Nimemupa Esteri mali ya Hamani, naye wamekwisha kumutundika kwa sababu ya shauri lake baya juu ya Wayuda.
8Munaweza kuwaandikia Wayuda neno lolote munalopenda. Tena munaweza kuandika kwa jina langu na kutumia muhuri wa kifalme, kwa sababu tangazo ambalo limetolewa kwa jina la mufalme na kupigwa muhuri wa mufalme, haliwezi kuvunjwa.”
9Basi, katika siku ya makumi mbili na tatu ya mwezi wa tatu inayoitwa Siwani, Mordekayi akawaita waandishi wote wa mufalme, akawaagiza waandike barua kwa Wayuda na wakubwa, watawala na wakubwa wa majimbo yote mia moja makumi mbili na saba, kuanzia Uhindi mpaka Etiopia. Barua hizo zikaandikwa kwa kila jimbo katika luga yake na sawasawa na maandiko yake, vilevile na kwa Wayuda kwa maandiko yao na luga yao.
10Mordekayi alikuwa ameandika barua hizo kwa jina la mufalme Ahasuero, akazipiga muhuri kwa pete ya mufalme. Na waliozipeleka walikuwa wajumbe waliopanda juu ya farasi wenye nguvu wanaokimbia mbio.
11Kwa njia ya barua hizi mufalme akawaruhusu Wayuda katika kila muji kukusanyika kwa kuyalinda maisha yao. Walikuwa na ruhusa ya kuharibu, kuua bila huruma na kuangamiza kundi lolote la watu au jimbo, lenye kuwashambulia kwa silaha pamoja na wanawake na watoto wao, na kunyanganya mali zao.
12Jambo hili lingefanyika katika majimbo yote ya mufalme Ahasuero, katika siku ya kumi na tatu ya mwezi wa kumi na mbili, ni kusema Adari.
13Mifano ya tangazo hili ambalo lilitolewa kama sheria katika kila jimbo ilisambazwa kwa kila mutu katika kila jimbo, kusudi Wayuda wajitayarishe kulipiza kisasi siku hiyo itakapofika.
14Kwa amri ya mufalme, wajumbe waliopanda juu ya farasi wa kifalme wenye nguvu wanaokimbia mbio, wakaondoka mbio. Tangazo hili vilevile lilitolewa katika muji mukubwa Susani.
15Mordekayi alipotoka katika nyumba kwa mufalme, akiwa amevaa nguo ya kifalme ya rangi ya mayungiyungi na nyeupe, koti la kitani safi la rangi nyekundu, na taji kubwa ya zahabu, muji wa Susani ukajaa shangwe na vigelegele.
16Hapo Wayuda wakapata utukufu, heshima na furaha, wakajisikia wenye shangwe na ushindi.
17Katika kila jimbo na kila muji, popote pale tangazo hili liliposomwa, Wayuda wakafurahi na kushangilia, wakafanya sherehe na mapumziko; na watu wengine wengi wakajifanya kuwa Wayuda, maana waliwaogopa sana Wayuda.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.