Danieli 6 - Swahili Congo Revised Bible 2002

1Naye mufalme Dario, wa inchi ya Wamedi, akatwaa utawala akiwa na umri wa miaka makumi sita na miwili.

Shauri baya za kumwangamiza Danieli

2Mufalme Dario aliamua kuweka wakubwa mia moja na makumi mbili kwa kusimamia mambo ya ufalme.

3Aliweka vilevile wakubwa watatu, Danieli akiwa mumoja kati yao, wawasimamie wale wakubwa wengine katika uongozi kusudi mufalme asipatwe na hasara.

4Danieli akaonekana kuwa bora kuliko wale wasimamizi wengine na wakubwa wote kwa maana alikuwa na roho njema. Hivyo mufalme akakusudia kumupa uongozi wa ufalme wote.

5Wale wakubwa pamoja na maliwali wakatafuta kisingizio cha kumushitaki Danieli juu ya mambo ya ufalme, lakini hawakuweza kupata sababu ya kumushitaki, wala kosa lolote, maana Danieli alikuwa mwaminifu. Hakupatikana na kosa, wala ubaya wowote.

6Halafu wakapatana hivi: Hatutapata kisingizio chochote cha kumushitaki Danieli isipokuwa kama kisingizio hicho kitakuwa kinaelekea Sheria ya Mungu wake.

7Basi, hao wakubwa na maliwali wote pamoja, wakamwendea mufalme na kumwambia: Uishi milele ee mufalme Dario!

8Sisi wakubwa uliotuweka, wasimamizi, maliwali, washauri na wakubwa wa majimbo, wote tumepatana kwamba inafaa, ee mufalme, utoe amri na kuhakikisha kwamba inafuatwa kikamilifu. Amuru kwamba kwa muda wa siku makumi tatu kusikuwe mutu yeyote atakayeruhusiwa kuomba kitu chochote kwa mungu yeyote au kwa mutu yeyote, isipokuwa kutoka kwako wewe, ewe mufalme. Mutu yeyote atakayevunja sheria hii atupwe katika pango la simba.

9Hivyo, ee mufalme Dario, utoe amri hiyo na kuitia sahihi yako kusudi isibadilishwe. Nayo itakuwa sheria ya Wamedi na Wapersi, sheria ambayo haitavunjika.

10Hivyo, mufalme Dario akatia sahihi kwenye sheria hiyo.

11Danieli alipojua kwamba ile sheria imetiwa sahihi, alirudi kwa nyumba yake kwenye gorofi katika chumba chake kilichokuwa na madirisha yaliyofunguka kuelekea Yerusalema. Humo, Danieli, kama ilivyokuwa kawaida yake, alipiga magoti mara tatu kila siku kwa kuomba na kumushukuru Mungu wake.

12Watu wale waliofanya mupango mubaya juu ya Danieli waliingia ndani, wakamukuta Danieli akiomba na kumusihi Mungu wake.

13Basi, walikwenda kwa mufalme na kumushitaki Danieli kwa kutumia ile sheria, wakisema: Mufalme Dario, haukutia sahihi kwenye sheria kwamba kwa muda wa siku makumi tatu hakuna mutu yeyote atakayeruhusiwa kuomba kitu chochote, kwa mungu yeyote, au kwa mutu yeyote isipokuwa kutoka kwako wewe, ee mufalme, na kwamba yeyote atakayevunja sheria hii atatumbukizwa katika pango la simba? Mufalme akaitikia: Hivi ndivyo inavyokuwa kulingana na sheria ya Wamedi na Wapersi ambayo haiwezi kuvunjika.

14Wakamwambia mufalme: Yule Danieli anayekuwa mumoja wa wafungwa kutoka inchi ya Yuda hakuheshimu wewe mufalme wala amri uliyotia sahihi. Anafanya maombi yake mara tatu kila siku.

15Mufalme aliposikia maneno hayo, alisikitika sana. Akafanya nguvu yake yote kwa kutafuta njia ya kumwokoa Danieli. Aliendelea kujaribu mpaka jua likatua.

16Wale watu kwa pamoja wakamwendea mufalme Dario na kumwambia: Ee mufalme, ujue kwamba hakuna sheria wala amri yoyote ya Wamedi na Wapersi inayoweza kubadilishwa kisha kuwekwa na mufalme.

Danieli katika pango la simba

17Halafu mufalme Dario akatoa amri, naye Danieli akaletwa na kutupwa katika pango la simba. Mufalme akamwambia Danieli: Mungu wako ambaye unamutumikia siku zote akuokoe.

18Jiwe likaletwa na kuwekwa kwenye mulango wa lile pango. Mufalme akapiga muhuri wake mwenyewe na ule wa wakubwa wake, kusudi uamuzi uliotolewa juu ya Danieli usibadilishwe.

19Kisha mufalme akarudi katika nyumba yake ya kifalme ambamo alikesha akifunga kula chakula wala hakupenda kufarijiwa na kitu chochote na hata usiku ule hakupata usingizi.

20Ilipokuwa asubui mapema, mufalme Dario aliamuka, akaenda kwa haraka kwenye pango la simba.

21Alipofika karibu akamwita Danieli kwa sauti ya huzuni: Danieli, mutumishi wa Mungu Mwenye Uzima, Mungu wako unayemutumikia siku zote ameweza kukuokoa na simba hawa?

22Danieli akamujibu mufalme: Uishi milele, ee mufalme!

23Mungu wangu alileta malaika wake kwa kufunga vinywa vya simba hawa, nao hawakunizuru. Alifanya hivyo kwa sababu alijua mimi sina kosa lolote mbele yake na wala sijafanya jambo lolote baya mbele yako.

24Kwa hiyo mufalme akafurahi sana; akaamuru kwamba wamwondoe Danieli toka ndani ya pango. Basi wakamwondoa, naye hakuonekana na alama hata kidogo ya kidonda, kwa sababu alimutegemea Mungu wake.

25Mufalme akaamuru wale watu waliomuchongea Danieli wakamatwe, nao wakatupwa ndani ya lile pango la simba pamoja na wake wao na watoto wao. Nao, hata mbele hawajagusa chini, simba waliwashambulia na kuivunjavunja mifupa yao.

26Halafu mufalme Dario akawaandikia watu wa makabila yote, mataifa yote, na luga zote katika dunia:

Ninawatakia amani kwa wingi.

27Ninatoa amri katika ufalme wangu kwamba watu wote wanapaswa kumwogopa na kumuheshimu Mungu wa Danieli.

Yeye ni Mungu Mwenye Uzima, anayeishi milele;

ufalme wake hauwezi kuangamizwa hata kidogo,

utawala wake hauna mwisho.

28Yeye anakomboa na kuokoa,

anafanya miujiza na maajabu mbinguni na katika dunia,

maana amemwokoa Danieli toka nguvu za simba.

29Basi, Danieli akastawi wakati wa utawala wa mufalme Dario na wa mufalme Kiro wa inchi ya Persia.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help