2 Wafalme 3 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Vita kati ya Israeli na Moabu

1Katika mwaka wa kumi na nane wa utawala wa mufalme Yosafati wa Yuda, Yoramu mwana wa Ahabu alianza kutawala inchi ya Israeli. Akatawala akiwa Samaria kwa muda wa miaka kumi na miwili.

2Yoramu alitenda maovu mbele ya Yawe, lakini yeye hakukuwa mubaya kama baba na mama yake; maana alibomoa munara wa Bali uliofanywa na baba yake.

3Hata hivyo, Yoramu aliendelea kutenda zambi ileile ya Yeroboamu mwana wa Nebati ambaye aliwasukuma watu wa Israeli watende zambi. Hakuiacha.

4Mufalme Mesha wa Moabu alikuwa mufugaji wa kondoo, na kila mwaka alilipa kodi kwa mufalme wa Israeli wana-kondoo elfu mia moja na manyoya ya kondoo wengine elfu mia moja.

5Lakini Ahabu alipokufa, mufalme wa Moabu alimwasi.

6Kwa hiyo mufalme Yoramu akaondoka Samaria, akakusanya waaskari wote wa Israeli.

7Akatuma ujumbe kwa mufalme Yosafati wa Yuda, akamwambia: “Mufalme wa Moabu ameniasi. Utashirikiana nami tupigane naye?”

Mufalme Yosafati akamujibu: “Niko tayari! Mimi na wewe ni kitu kimoja; watu wangu ni kama wako, farasi wangu ni kama wako.

8Tutashambulia kutokea upande gani?” Yoramu akajibu: “Tutashambulia kutokea jangwa la Edomu.”

9Basi, mufalme Yoramu akaondoka pamoja na mufalme wa Yuda na mufalme wa Edomu. Nyuma ya kusafiri kwa muda wa siku saba, maji yakawaishia. Hawakukuwa na maji kwa ajili ya waaskari wao wala kwa nyama wao.

10Hapo mufalme wa Israeli akasema: “Ole wetu! Yawe ametukusanya wote wafalme watatu atutie katika mikono ya mufalme wa Moabu.”

11Mufalme Yosafati akauliza: “Hakuna nabii yeyote hapa wa Yawe ambaye tunaweza kumwuliza shauri la Yawe?” Mutumishi mumoja wa mufalme Yoramu wa Israeli akajibu: “Elisha mwana wa Safati iko hapa. Yeye alikuwa mutumishi wa Elia.”

12Yosafati akasema: “Huyo ni nabii wa kweli.” Kisha wafalme hao watatu wakamwendea Elisha.

13Elisha akamwuliza mufalme wa Israeli: “Kuna maneno gani kati yako nami? Kwenda uombe shauri kwa manabii ambao baba yako na mama yako waliwaendea.” Mufalme wa Israeli akajibu: “Sivyo! Yawe ndiye aliyetuita sisi wafalme watatu kusudi atutie katika mikono ya mufalme wa Moabu.”

14Elisha akasema: “Kama vile Yawe wa majeshi, yule ambaye mimi ninamutumikia, anavyoishi, kama isingekuwa kwa heshima ninayokuwa nayo kwa rafiki yako mufalme Yosafati wa Yuda, nisingekujali hata kidogo.

15Lakini sasa uniletee mupiga kinanda.” Wakamuletea mupiga kinanda. Ikakuwa wakati alipopiga kinanda, nguvu ya Yawe ikamujaza Elisha,

16akasema: “Yawe anasema hivi: ‘Muchimbe mashimo kila pahali katika bonde.’

17Ingawa hamutaona upepo wala mvua, bonde litajaa maji, nanyi mutakunywa, ninyi pamoja na ngombe wenu na nyama wenu.

18Lakini hili si jambo gumu kwa Yawe; yeye atawapa vilevile ushindi juu ya Moabu.

19Mutashinda kila muji wenye kuta na kila muji muzuri; mutaikata miti yao yote, mutaziba chemichemi zote za maji, na kuyaharibu mashamba yao yote yenye mboleo kwa kuyajaza mawe.”

20Kesho yake asubui, wakati wa kutoa sadaka, maji yakatiririka kutoka upande wa Edomu na kujaa kila pahali katika bonde.

21Wamoabu walipopata habari kwamba hao wafalme watatu wamekuja kuwashambulia, watu wote walioweza kubeba silaha kuanzia vijana mpaka wazee, waliitwa, wakapewa silaha na kuwekwa kwenye mupaka tayari kwa vita.

22Walipoamuka asubui iliyofuata, jua lilikuwa linametameta juu ya maji hayo; walipoyaangalia yakaonekana kuwa mekundu kama damu.

23Wakasema: “Hii ni damu! Bila shaka hawa wafalme watatu wamepigana wao kwa wao na kuuana! Tuende tunyanganye vitu vyao!”

24Lakini walipofika katika kambi ya Waisraeli, watu wa Israeli waliwashambulia, nao wakakimbia mbele yao. Watu wa Israeli wakawafuatilia mpaka Moabu, wakiwaua

25na kuibomoa miji yao. Kila nafasi walipopita kwenye shamba zuri, kila mutu alilirushia jiwe mpaka kila shamba likajaa mawe; vilevile wakaziziba chemichemi zote za maji na kukata miti yote mizuri. Nyuma ya hayo, kukabaki muji mukubwa wa Kiri-Haraseti peke yake, ambao waaskari wapiga-kombeo waliuzunguka na kuuteka.

26Mufalme wa Moabu alipoona kwamba vita inamwendea vibaya, akatwaa watu wake mia saba wenye kupigana kwa mapanga, akikusudia kupenya kati ya waaskari wa waadui zake mbele ya mufalme wa Edomu, lakini hakuweza.

27Hapo akamutwaa mwana wake wa kwanza ambaye angekuwa mufalme kwa pahali pake, akamutoa kuwa sadaka ya kuteketezwa juu ya ukuta wa muji. Watu wa Israeli walipoona hayo, wakachukizwa sana. Wakauacha muji ule na kurudia katika inchi yao.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help