1Wafilistini walikusanya makundi yao yote ya waaskari kule Afeki, na Waisraeli walipiga kambi kwenye chemichemi ya bonde la Yezereheli.
2Wakubwa watano wa Wafilistini walipokuwa wakipita na makundi yao ya waaskari ya mamia na maelfu, Daudi naye akiwa na watu wake pamoja na Akisi walikuwa wanafuata upande wa nyuma wa kundi lile.
3Wakubwa wa waaskari wa Wafilistini waliuliza: “Waebrania hawa wanafanya nini hapa?”
Akisi akawajibu wale wakubwa wa Wafilistini: “Huyu ni Daudi, mutumishi wa Saulo mufalme wa Israeli; naye amekuwa nami kwa miaka fulani. Na tangu alipokimbilia kwangu, sijamupata na kosa lolote.”
4Lakini wakubwa wa Wafilistini walimukasirikia sana Akisi, wakamwambia: “Umurudishe aende pahali ulipomupa akae. Asiende hata kidogo pamoja nasi kwa vita, kama sivyo wakati wa vita atageuka na kuwa adui yetu. Hauoni kwamba mutu huyu atapata njia nzuri ya kupatana na bwana wake halafu kuwa adui yetu katika vita?
5Huyu ni Daudi yuleyule ambaye wanawake waliimba habari zake walipokuwa wakicheza:
‘Saulo ameua maelfu,
lakini Daudi ameua maelfu kumi.’ ”
6Akisi akamwita Daudi na kumwambia: “Kama vile Yawe anavyoishi, umekuwa mutu wa usawa. Ingekuwa jambo zuri kwangu tuende wote katika vita, kwa maana sijaona jambo baya lolote kwako tangu siku ile ulipokuja kwangu mpaka leo hii. Hata hivyo, wakubwa hawajapendezwa nawe.
7Hivyo sasa, urudi kwa nyumba. Kwenda kwa amani kusudi usiwachukize wakubwa wa Wafilistini.”
8Daudi akamwambia Akisi: “Lakini nimefanya nini? Kama unavyosema kwamba haujaniona na kosa lolote tangu siku ile nilipoanza kukutumikia mpaka leo, kwa nini nisiende kupigana na waadui za bwana wangu mufalme?”
9Akisi akamwambia: “Ninajua kwamba hauna lawama mbele yangu kama malaika wa Mungu. Hata hivyo, wakubwa wa Wafilistini wamesema: ‘Asiende hata kidogo pamoja nasi katika vita’.
10Sasa, wewe pamoja na watumishi wa bwana wako Saulo waliokuja pamoja nawe, kesho asubui mapema, muamuke na kuondoka mara tu kunapopambazuka.”
11Kwa hiyo, kesho yake asubui, Daudi pamoja na watu wake waliondoka kurudi katika inchi ya Wafilistini. Lakini hao Wafilistini wakaenda Yezereheli.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.