Marko 10 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Mafundisho ya Yesu juu ya kuvunja ndoa(Mat 19.1-12; Lk 16.18)

1Yesu akaondoka kule, akaenda katika jimbo la Yudea na kuvuka ngambo ingine ya Yordani. Na makundi mengi ya watu wakakusanyika tena mbele yake, naye akaanza kuwafundisha, kama vile alivyozoea kufanya.

2Wafarisayo wamoja wakamufikia kwa kumupima, wakamwuliza: “Sheria yetu inamuruhusu mutu kufukuza muke wake?”

3Yesu akajibu: “Musa aliwaamuru nini?”

4Nao wakamujibu: “Musa alitoa ruhusa kwa mutu kuandika barua ya kuachana na muke wake na kisha amufukuze.”

5Yesu akawaambia: “Musa aliwaandikia amri ile kwa sababu ya ugumu wa mioyo yenu.

6Lakini wakati Mungu alipowaumba watu wa kwanza, aliwaumba mwanaume na mwanamuke.

7Kwa sababu hii, mutu atawaacha baba yake na mama yake na kuungana na muke wake,

8nao wawili watakuwa mwili mumoja. Hivi wao si wawili tena, lakini wanakuwa mumoja.

9Basi mutu asitenganishe kile Mungu alichokiunganisha.”

10Walipokuwa ndani ya nyumba, wanafunzi wakamwuliza Yesu tena juu ya neno lile.

11Yesu akawaambia: “Kila mutu anayemufukuza muke wake na kuoa mwingine, anazini na kumukosea yule muke wa kwanza.

12Vile vile, kila muke anayemwacha mume wake na kuolewa na mwingine, anazini.”

Yesu anabariki watoto wadogo(Mat 19.13-15; Lk 18.15-17)

13Watu wamoja wakamuletea Yesu watoto kusudi awawekee mikono, lakini wanafunzi wake wakawakaripia watu wale.

14Yesu alipoona vile, akakasirika na kuwaambia wanafunzi wake: “Muwaache watoto wadogo wakuje kwangu wala musiwakataze, kwa maana Ufalme wa Mungu ni wa watu wanaokuwa sawasawa na wao.

15Kweli ninawaambia ninyi: mutu yeyote asiyepokea Ufalme wa Mungu kama mutoto mudogo, hawezi kuingia ndani yake hata kidogo.”

16Kisha akawakumbatia watoto wale, akaweka mikono juu yao na kuwabariki.

Kijana mumoja tajiri(Mat 19.16-30; Lk 18.18-30)

17Yesu alipoondoka kwa kuendelea na safari yake, mutu mumoja akamufikia mbio akapiga magoti mbele yake na kumwuliza: “Mwalimu mwema, nifanye nini kusudi nipate kurizi uzima wa milele?”

18Yesu akamwuliza: “Sababu gani unaniita mwema? Hakuna mutu anayekuwa mwema, isipokuwa Mungu peke yake.

19Unajua jinsi amri zinavyosema kwamba: ‘Usiue, usizini, usiibe, usishuhudie uongo, usidanganye, uwaheshimu baba yako na mama yako.’ ”

20Yule mutu akamujibu: “Mwalimu, nimetii amri zile zote tangu ujana wangu.”

21Yesu akamwangalia kwa upendo, akamwambia: “Unakosewa na kitu kimoja tu: kwenda uuzishe vitu vyote unavyokuwa navyo, na uwape wamasikini mali zile, nawe utakuwa na akiba mbinguni. Kisha urudi, unifuate!”

22Lakini kijana yule aliposikia maneno yale, alikunja uso, na kujiendea katika huzuni, kwa sababu alikuwa tajiri sana.

23Yesu akaangalia pande zake zote na kuwaambia wanafunzi wake: “Kweli ni vigumu sana kwa watajiri kuingia katika Ufalme wa Mungu!”

24Wanafunzi wakashangaa sana kusikia maneno hayo. Lakini Yesu akawaambia tena: “Watoto wangu, ni vigumu kabisa kuingia katika Ufalme wa Mungu!

25Ni kwepesi zaidi kwa ngamia kupita katika tundu la sindano kuliko tajiri kuingia katika Ufalme wa Mungu.”

26Wanafunzi waliposikia maneno hayo wakazidi kushangaa hata wakaulizana wao kwa wao: “Ni nani basi anayeweza kuokolewa?”

27Yesu akawaangalia na kuwaambia: “Kwa mwanadamu haiwezekani, lakini kwa Mungu si vile, kwa maana mambo yote yanawezekana kwa Mungu.”

28Petro akamwambia: “Angalia sisi tumeacha vyote na kukufuata wewe!”

29Yesu akajibu: “Kweli ninawaambia: kama mutu akiacha nyumba yake, ndugu, dada, mama, baba, watoto wake au mashamba yake kwa ajili yangu na kwa ajili ya Habari Njema,

30atapokea mara mia zaidi katika wakati wa sasa. Atapokea nyumba, ndugu, dada, mama, watoto na mashamba pamoja na mateso. Na katika wakati utakaokuja atapokea uzima wa milele.

31Lakini wengi wanaokuwa wa kwanza watakuwa wa mwisho, na wengi wanaokuwa wa mwisho watakuwa wa kwanza.”

Yesu anajulisha mara ya tatu habari za kufa na kufufuka kwake(Mat 20.17-19; Lk 18.31-34)

32Yesu na wanafunzi wake walipokuwa katika njia, wakipanda kwenda Yerusalema, yeye akatangulia mbele yao. Wanafunzi walishikwa na hofu, nao watu waliowafuata waliogopa. Yesu akawatwaa tena wanafunzi wake kumi na wawili, na kuanza kusemezana nao juu ya mambo yatakayomupata.

33Akawaambia: “Tunapanda kwenda Yerusalema na kule Mwana wa Mutu atatolewa kwa wakubwa wa makuhani na kwa walimu wa Sheria. Nao watamuhukumu auawe na kumutoa katika mikono ya watu wa mataifa mengine.

34Nao watamuchekelea, watamutemea mate, watamupiga fimbo na kumwua. Lakini kwa siku ya tatu kisha kufa kwake, atafufuka.”

Yakobo na Yoane wanaomba ukubwa(Mat 20.20-28)

35Kisha wana wawili wa Zebedayo, Yakobo na Yoane, wakamufikia Yesu na kumwambia: “Mwalimu, tunataka utufanyie jambo tutakalokuomba.”

36Yesu akawauliza: “Munataka niwafanyie nini?”

37Nao wakamujibu: “Utakapokuwa katika utukufu wako, uturuhusu kuikaa pamoja nawe, mumoja kwa upande wako wa kuume na mwingine kwa upande wako wa kushoto.”

38Lakini Yesu akawaambia: “Hamujui kitu munachoomba. Munaweza kunywa kikombe cha mateso nitakachokunywa? Au munaweza kubatizwa kwa namna ya ubatizo nitakaoupata?”

39Nao wakamujibu: “Tunaweza.”

Yesu akaongeza kuwaambia: “Hakika mutakunywa kikombe nitakachokunywa, na kubatizwa kama vile nitakavyobatizwa.

40Lakini kuikalisha mutu kwa upande wangu wa kuume au wa kushoto si kazi yangu. Ni Mungu peke yake atakayeweka watu aliowatayarisha kwenye nafasi zile.”

41Wanafunzi wengine kumi waliposikia maneno yale, wakachukizwa na Yakobo na Yoane.

42Yesu akawaita wote na kuwaambia: “Munajua kwamba wale wanaohesabiwa kuwa watawala wa mataifa wanayatawala kwa kinguvu, na wakubwa yao wanayagandamiza.

43Lakini isikuwe hivi katikati yenu. Anayetaka kuwa mukubwa kati yenu, sherti akuwe mutumishi wenu.

44Naye anayetaka kuwa wa kwanza, sherti akuwe mutumwa wa wote.

45Kwa maana hata Mwana wa Mutu hakuja kutumikiwa, lakini kutumika na kutoa maisha yake kusudi awakomboe watu wengi.”

Yesu ananyesha kipofu Bartimayo(Mat 20.29-34; Lk 18.35-43)

46Wakafika Yeriko. Na wakati Yesu alipokuwa akitoka kule pamoja na wanafunzi wake na kundi kubwa la watu, mutu mumoja kipofu aliyeitwa Bartimayo mwana wa Timayo, alikuwa akiikaa pembeni ya njia akiombaomba.

47Naye aliposikia kwamba Yesu wa Nazareti anapita katika njia ile, akalalamika, akisema: “Yesu Mwana wa Daudi, unisikilie huruma!”

48Watu wengi walimukaripia na kumwambia anyamaze, lakini alizidi kulalamika akisema: “Yesu Mwana wa Daudi, unisikilie huruma!”

49Yesu akasimama na kusema: “Mumwite.”

Basi wakamwita yule kipofu na kumwambia: “Ujipe moyo! Simama, anakuita.”

50Bartimayo akatupa koti yake, akaruka upesi na kumwendea Yesu.

51Yesu akamwuliza: “Unataka nikufanyie nini?”

Yule kipofu akamujibu: “Mwalimu, ninataka nipate kuona.”

52Yesu akamwambia: “Ujiendee, imani yako imekuponyesha.”

Na pale pale akapata kuona, na kumufuata Yesu katika njia.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help