1Zaburi ya Daudi.
Usihangaike kwa sababu ya waovu;
usiwaonee wivu wanaotenda mabaya.
2Maana hao watatoweka mara moja kama nyasi;
watanyauka kama majani.
3Umutumainie Yawe na kutenda mazuri,
upate kuishi katika inchi na kuwa salama.
4Uitafute furaha yako kwa Yawe,
naye atakujalia unayotamani katika moyo.
5Umutolee Yawe maisha yako,
umutumainie yeye, naye atakufanyia kitu.
6Ataifanya haki yako iangae
kama mwangaza wa jua muchana kati.
7Tulia mbele ya Yawe, umungojee kwa uvumilivu;
usihangaike juu ya wale wanaofanikiwa,
ndio watu wanaojaliwa katika mipango yao mibaya.
8Usiwake hasira wala kuwa na kasirani;
usihangaike, maana hiyo inazidisha ubaya.
9Watu wanaotenda mabaya wataangamizwa,
lakini wanaomutumainia Yawe watarizi inchi.
10Bado kidogo, mwovu atatoweka;
utamutafuta pale alipokuwa, wala hautamwona.
11Lakini wapole watarizi inchi,
hao wataifurahia amani kamili.
12Mwovu anamufanyia mutu wa haki shauri baya,
na kumusagia meno kwa chuki.
13Lakini Yawe anamuchekelea mwovu,
kwa maana anajua mwisho wake ni karibu.
14Waovu wanachomoa panga na kuvuta pinde zao,
wapate kuwaua wamasikini na wakosefu;
wawachinje watu wenye mwenendo sawa.
15Lakini panga zao wenyewe zitawapenya mioyo,
na pinde zao zitavunjwavunjwa.
16Afazali mali kidogo ya mutu wa haki
kuliko utajiri mwingi wa watu waovu.
17Maana nguvu za waovu zitavunjwa,
lakini Yawe atawaimarisha watu wa haki.
18Yawe anatunza maisha ya watu wakamilifu,
na urizi wao utadumu milele.
19Hawatafezeheka nyakati mbaya zikiwafikia;
siku za njaa watakuwa na chakula tele.
20Lakini waovu wataangamia,
waadui za Yawe watanyauka kama maua katika jangwa;
kweli watatoweka kama moshi.
21Mutu mwovu anakopesha bila kurudisha;
lakini mutu wa haki anatoa kwa moyo safi.
22Waliobarikiwa na Yawe watarizi inchi,
lakini waliolaaniwa naye wataongolewa.
23Yawe anaongoza mutu katika njia yake,
anamulinda yule anayemupendeza.
24Hata akianguka, hatabaki chini,
kwa sababu Yawe anamuimarisha.
25Nilikuwa kijana na sasa mimi ni muzee;
hata kidogo sijaona mutu wa haki ameachwa na Mungu,
au watoto wake wakiombaomba chakula.
26Siku zote yeye anakopesha kwa moyo safi,
na watoto wake ni wenye baraka.
27Achana na uovu, utende mazuri,
nawe utaishi katika inchi siku zote;
28maana Yawe anapenda haki,
wala hawaachi waaminifu wake.
Anawalinda hata milele;
lakini wazao wa waovu wataangamizwa.
29Watu wa haki watarizi inchi,
nao wataishi humo milele.
30Mutu wa haki anasema maneno ya hekima,
kwa ulimi wake anasema kufuatana na sheria ya Mungu.
31Sheria ya Mungu wake ni ndani ya moyo wake,
naye hapiti pembeni katika mwenendo wake.
32Mutu mwovu anamuvizia mutu wa haki,
na kujaribu kumwua;
33lakini Yawe hatamutoa mutu wa haki katika makucha yake,
wala kumwachilia aazibiwe anaposhitakiwa.
34Umutumainie Yawe na kushika njia yake,
naye atakuinua uirizi inchi,
na kuwaona waovu wakiongolewa.
35Nilimwona mwovu aliyejivuna sana,
akinyanyua shingo juu kama mierezi ya Lebanoni!
36Kisha nikapita pale, naye hakukuwa tena;
nikamutafuta, lakini hakuonekana tena.
37Muangalie mutu mukamilifu, mutu wa usawa;
mutu anayependa amani anajaliwa wazao.
38Lakini wakosaji wote wataangamizwa;
na wazao wao wataongolewa.
39Yawe anawaokoa watu wa haki,
na kuwalinda wakati wa taabu.
40Yawe anawasaidia na kuwaokoa;
anawaopoa kutoka makucha ya waovu na kuwaokoa,
maana wanakimbilia kwake.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.