Isaya 65 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Mungu anawaazibu waasi

1Yawe anasema;

Nilikuwa tayari kujionyesha

kwao wasiouliza habari zangu.

Nilikuwa tayari kuwapokea

wale wasionitafuta.

Nililiambia taifa ambalo halikuomba kwa jina langu:

Niko hapa! Niko hapa!

2Muchana kutwa niliwanyooshea mikono watu waasi,

watu ambao wanafuata njia zisizokuwa nzuri,

watu ambao wanafuata mawazo yao wenyewe.

3Ni watu ambao wananichokoza waziwazi siku zote;

wanatambikia miungu yao katika bustani,

na kuifukizia ubani juu ya matofali.

4Wanaikaa katika makaburi na kupitisha usiku ndani ya mashimo.

Wanakula nyama ya nguruwe

na kuweka muchuzi wa nyama wachafu ndani ya sahani zao.

5Wanawaambia wale wanaokutana nao hivi:

Muikae mbali nami;

musinikaribie kwa sababu mimi ni mutakatifu!

Watu hao wananikasirikisha sana,

hasira yangu ni kama moto usiozimika.

6Mujue kwamba mambo hayo yameandikwa mbele yangu,

sitanyamaza lakini nitawalipiza;

nitawalipa sawa inavyostahili.

7Nitawalipiza maovu yao

wayalipe vilevile maovu ya babu zao.

–Ni Yawe anayesema hivyo.–

Wao waliifukizia ubani miungu yao kwenye milima,

wakanitukana mimi kule juu ya vilima.

Nitawalipa sawa inavyostahili,

watayalipa matendo yao ya zamani.

8Yawe anasema hivi:

Mutu akikuta kishada cha mizabibu mizuri,

watu wanasema: Tusikiharibu; kina baraka.

Ndivyo nitakavyofanya kwa ajili ya watumishi wangu;

sitawaangamiza wote.

9Nitawajalia watu wa Yakobo,

na Yuda nitamujalia watakaorizi milima yangu;

wachaguliwa wangu watairizi,

watumishi wangu watakaa kule.

10Bonde la Saroni litakuwa nafasi ya kukulishia nyama,

bonde la Akori litakuwa mapumziko ya ngombe

kwa ajili ya watu wangu walionitafuta.

11Lakini nitafanya nini na ninyi

munaoniacha mimi Yawe,

musioujali Sayuni, mulima wangu mutakatifu,

munaotolea miungu chakula na divai

kusudi iwapatie bahati zuri.

12Nimewapangia kifo kwa upanga,

ninyi wote mutanaswa kwa kuchinjwa!

Maana, nilipowaita, hamukuniitikia;

niliposema, hamukunisikiliza.

Mulitenda maovu mbele yangu,

mukachagua yale nisiyoyapenda.

13Basi, mimi Yawe ninasema:

Watumishi wangu watakula,

lakini ninyi mutasikia njaa;

watumishi wangu watakunywa,

lakini ninyi mutasikia kiu;

watumishi wangu watafurahi,

lakini ninyi mutafezeheka.

14Watumishi wangu wataimba kwa furaha ndani ya moyo,

lakini ninyi mutalia kwa uchungu ndani ya moyo

na kupiga kelele kwa uchungu mukubwa ndani ya roho.

15Wale niliowachagua nitawapa jina jipya.

Lakini ninyi jina lenu watalitumia kwa kulaani;

watasema: Bwana wetu Yawe awaue.

16Basi, mwenye kujitakia baraka katika inchi,

atajitakia baraka kwa Mungu wa kweli.

Mwenye kuapa katika inchi hii,

ataapa kwa Mungu wa kweli.

Maana taabu za zamani zimepita

zimetoweka kabisa mbele yangu.

17Sasa, ninaumba mbingu mupya na dunia mupya.

Mambo ya zamani hayatakumbukwa tena.

18Mufurahi na kushangilia milele,

kwa ajili ya vitu hivi ninavyoumba.

Yerusalema nitaifanya muji wa shangwe,

na watu wake watu wenye furaha.

19Nami nitaufurahia Yerusalema,

nitawafurahia watu wangu.

Sauti ya kilio haitasikilika tena,

kilio cha taabu hakitakuwa tena.

20Hakutakuwa tena vifo vya watoto wachanga,

wazee nao hawatakufa mbele ya wakati wao.

Mutu wa miaka mia moja akikufa, amekufa akiwa kijana;

na akikufa mbele ya miaka mia moja, ni kusema amelaaniwa.

21Watu watajenga nyumba na kuishi humo;

watalima mizabibu na kula matunda yake.

22Hawatajenga nyumba na watu wengine wakae ndani yake,

wala kulima chakula kikuliwe na watu wengine.

Maana watu wangu niliowachagua

wataishi maisha marefu kama miti;

wachaguliwa wangu watafurahia matunda ya jasho lao.

23Kazi zao hazitakuwa bure,

wala hawatazaa watoto watakaopatwa na musiba;

maana watakuwa waliobarikiwa na Yawe,

wamebarikiwa wao pamoja na wazao wao.

24Hata mbele hawajaniita, mimi nitawaitikia;

mbele hawajamaliza kusema, nitakuwa nimewajibu.

25Imbwa wa pori na kondoo watakula pamoja,

simba watakula majani kama ngombe,

lakini chakula cha nyoka kitakuwa mavumbi.

Katika mulima wangu wote mutakatifu,

hakuna atakayeumiza au kuharibu kitu.

–Ni Yawe anayesema hivyo.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help