Muhubiri 8 - Swahili Congo Revised Bible 2002

1Nani anayekuwa kama mwenye hekima?

Nani anayejua maana ya kila kitu?

Hekima inaangarisha uso wa mutu,

inaondoa alama za upumbafu.

2Mimi ninasema hivi: tii amri ya mufalme. Kwa sababu ya kiapo chako kitakatifu, usikate tamaa.

Mutii mufalme

3Usifanye haraka kukataa mamlaka yake, wala usiendelee kutenda lisilomupendeza, maana mufalme anafanya jinsi anavyopenda.

4Amri ya mufalme ni shauri la mwisho. Nani anayesubutu kumwuliza: “Unafanya nini?”

5Anayetii amri hatapata hasara, na mwenye hekima atajua kwamba kuna wakati wa hukumu.

6Kweli, kila kitu kina wakati wake na njia yake, ingawa mwanadamu anapatwa na tatizo kubwa.

7Hajui ni kitu gani kitakachotukia nyuma, maana ni nani anayeweza kumujulisha yatakayotukia nyuma?

8Hakuna mutu anayekuwa na uwezo wa kushikilia roho yake kusudi asikufe; hakuna mutu anayekuwa na uwezo juu ya siku ya kufa. Wakati wa vita hakuna kuponyoka, na uovu hauwezi kumwokoa mwovu.

Waovu na wenye haki

9Haya yote nimeyaona katika uchunguzi wangu juu ya yote yanayotendeka hapa chini ya jua, ambako mwanadamu anatawala mwenzake na kumutesa.

10Tena, nimeona waovu wakizikwa, watu ambao walizoea kuingia na kutoka pahali patakatifu, na kusifiwa katika muji uleule walimotenda maovu yao. Hayo nayo ni bure.

11Kwa vile uovu hauazibiwi haraka, mioyo ya wanadamu inakusudia kutenda mabaya.

12Wenye zambi wanatenda maovu mara mia. Hata hivyo, wanaendelea kuishi. Lakini, mimi ninajua kwamba itakuwa heri kwa wanaomwogopa Mungu, kwa sababu ya woga wao.

13Lakini hakuna furaha kwa waovu. Wao watapita kama kivuli, maisha yao hayatakuwa marefu kwa sababu hawamwogopi Mungu.

14Kuna jambo moja la bure nililotambua hapa katika dunia: mara kwa mara watu wema wanatendewa jinsi waovu wanavyostahili kutendewa, nao waovu wanatendewa jinsi watu wema wanavyostahili kutendewa. Ninasema kwamba hayo nayo ni bure.

15Basi, mimi ninasifu furaha, kwa maana hapa chini ya jua hakuna kitu kinachokuwa kizuri zaidi kuliko kula na kunywa na kujifurahisha. Haya ndiyo mutu anayoweza kufanya anapotoa jasho katika muda wa maisha yake aliyojaliwa na Mungu chini ya jua.

16Kila mara nilipojitoa kwa kujua hekima na kuona yanayotendeka hapa katika dunia, nilitambua kwamba mutu anaweza kukaa macho muchana na usiku,

17lakini hataelewa kazi ya Mungu inayofanyika chini ya jua. Mutu anaweza kutoa jasho sana lakini hataelewa. Wenye hekima wanaweza kujidai kwamba wanajua, lakini, kwa kweli, hawajui.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help