Yeremia 10 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Ibada ya sanamu na ya kweli

1Enyi Waisraeli musikilize neno Yawe analowaambia.

2Yawe anasema hivi:

Musiige mwenendo wa mataifa mengine,

wala musishangazwe na vitambulisho vya ajabu munavyoviona katika mbingu;

muyaache mataifa mengine yashangazwe navyo.

3Maana, desturi za dini za watu hao ni za uongo.

Kwa maana mutu anakata muti katika pori,

naye fundi anachonga sanamu ya mungu kwa shoka.

4Kisha watu wanaipamba kwa feza na zahabu

wakiipigilia misumari na nyundo

kusudi isianguke.

5Sanamu zao ni kama sanamu za kutishia ndege

katika shamba la maboga,

hazina uwezo wa kuongea;

ni lazima zibebwe

maana haziwezi kutembea.

Musiziogope sanamu hizo,

maana haziwezi kuzuru,

wala haziwezi kutenda jambo lolote jema.

6Ee Yawe, hakuna anayekuwa kama wewe;

wewe ni mukubwa na nguvu yako inajulikana.

7Nani asiyekuogopa wewe, ee mufalme wa mataifa?

Wewe unastahili kuheshimiwa:

kwa maana kati ya wenye hekima wote wa mataifa,

na katika falme zao zote,

hakuna hata mumoja anayekuwa kama wewe.

8Wote ni wajinga na wapumbafu,

fundisho la sanamu hizi ni mazarau matupu!

9Sanamu hizo zinapambwa kwa feza kutoka Tarsisi,

na zahabu kutoka Ofiri;

zilitengenezwa na wafundi na wafua zahabu.

Zimevalishwa nguo nzuri za rangi ya samawi na nyekundu-nyeusi,

zilizofumwa na wafundi wa kufuma.

10Lakini Yawe ni Mungu wa kweli,

Mungu Mwenye Uzima, mufalme wa milele.

Akikasirika, dunia inatetemeka,

mataifa hayawezi kuvumilia hasira yake.

11Basi, utawaambia hivi: Miungu hiyo ambayo haikuumba mbingu na dunia itaangamia. Itatoweka kabisa toka katika dunia, hapa chini ya mbingu.

Wimbo wa kumusifu Mungu

12Yawe aliiumba dunia kwa nguvu zake;

kwa hekima yake alisimamisha ulimwengu imara,

kwa akili yake alizitandika mbingu juu.

13Anapotoa sauti, maji yananguruma katika mbingu,

anapandisha mawingu toka kwa miisho ya dunia.

Anaufanya umeme upige wakati wa mvua,

na kuuvumisha upepo katika gala zake.

14Mwanadamu ni mujinga na mupumbafu;

kila mufua zahabu anafezeheshwa na sanamu zake.

Sanamu hizo ni uongo mutupu,

hazina uzima wowote ndani yao.

15Hazina faida, ni udanganyifu mutupu;

wakati zitakapoazibiwa zote zitaangamia.

16Lakini Mungu wa Yakobo si kama sanamu hizo,

maana, yeye ndiye aliyeumba vitu vyote,

na Israeli ni taifa linalokuwa mali yake;

Yawe wa majeshi, ndilo jina lake.

Uhamisho unakaribia

17Mufunge vitu vyenu, enyi watu muliozungukwa kwa vita.

18Maana Yawe anasema hivi:

Mara hii nitawatupa inje wakaaji wa inchi hii,

nitawataabisha hata kusibaki mutu yeyote.

19Ole wangu mimi Yerusalema, maana nimeumizwa sana!

Kidonda changu ni kikubwa sana!

Mimi nilikuwa nikijisemesha hivi: Hakika haya ni magumu tu,

nami ninapaswa kuyavumilia.

20Lakini hema yangu imebomolewa,

kamba zake zote zimekatika;

watoto wangu wameniacha, na kujiendea,

wala hawako tena;

hakuna wa kunisimikia tena hema yangu,

wala wa kunitundikia mapazia yangu.

21Nami Yeremia nikasema:

Wachungaji wamekuwa wajinga,

hawakuuliza shauri kwa Yawe;

kwa sababu hiyo, hawakufanikiwa,

na kondoo wao wote wamesambaa.

22Musikilize ile fujo!

Angalia inakuja.

Kunatokea shindo kubwa upande wa kaskazini.

Taifa kutoka kaskazini linakuja

kuifanya miji ya Yuda kuwa jangwa,

wataigeuza mapango ya mbweha!

23Ninajua, ee Yawe,

mwanadamu hana uwezo juu ya maisha yake;

hakuna mutu anayeweza kuongoza maisha yake.

24Utuonye, ee Yawe, lakini si kwa kasirani,

wala kwa hasira yako, kusudi tusiangamie.

25Umwange hasira yako juu ya mataifa yasiyokuabudu,

na juu ya watu ambao hawakutambui.

Maana, wamewaua wazao wa Yakobo;

wamewaua na kuwaangamiza kabisa,

na inchi yao wameiacha mabomoko.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help