Yeremia 49 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Neno la Mungu juu ya Waamoni

1Juu ya Waamoni,

Yawe anasema hivi:

Israeli hana watoto?

Hana warizi?

Mbona basi mungu Milkomu ametwaa Gadi

na watu wake wanafanya makao yao katika miji yake?

2Kwa hiyo, siku zinakuja

ambapo nitavumisha sauti ya vita

juu ya Raba muji wa Waamoni.

–Ni ujumbe wa Yawe.–

Raba utakuwa lundo la uharibifu,

vijiji vyake vitateketezwa kwa moto.

Halafu Israeli atatwaa tena urizi wake.

Ni Yawe anayesema hivyo.

3Muomboleze, enyi watu wa Hesiboni,

maana muji Ai umeharibika!

Mulie, enyi wabinti wa Raba!

Muvae magunia, muomboleze

na kukimbia huko na huko ndani ya ukuta wenu!

Maana mungu Milkomu atapelekwa katika uhamisho,

pamoja na makuhani wake na watumishi wake.

4Mbona munajivunia mabonde yenu, enyi musiokuwa waaminifu,

ninyi watu muliotegemea mali zenu, mukisema:

Nani atasubutu kupigana nasi?

5Basi, mimi nitawaletea vitisho.

–Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe wa majeshi.–

Hivi vitisho vitatoka kwa wajirani zenu wote,

nanyi mutafukuzwa inje, kila mutu kwa njia yake,

wala hakuna mutu atakayekusanya wakimbizi.

6Lakini kisha nitawarudisha tena Waamoni katika hali yao.

–Ni ujumbe wa Yawe.

Neno la Mungu juu ya Edomu

7Juu ya Edomu,

Yawe wa majeshi anasema hivi:

Hakuna tena hekima katika muji wa Temani?

Wenye hekima wao hawana shauri tena?

Hekima imetoweka kabisa?

8Mukimbie, enyi wakaaji wa Dedani,

mugeuke na kujificha ndani ya mapango!

Maana nitawaletea maangamizi,

enyi wazao wa Esau;

wakati wa kuwaazibu umefika.

9Wachuma zabibu watakapokuja kwenu,

hawataacha hata zabibu moja.

Usiku ule wizi watakapofika,

wataharibu kila kitu mpaka watosheke.

10Lakini nimemunyanganya Esau kila kitu,

nimeyafunua maficho yake,

wala hawezi kujificha tena.

Watoto, wandugu na jirani zake wameangamizwa;

hakuna hata mumoja aliyebaki.

11Muniachie watoto wenu wayatima nami nitawatunza;

muwaache wajane wenu wanitegemee.

12Yawe anasema hivi: Ikiwa wale ambao hawakustahili kunywa kikombe cha azabu ni lazima wakikunywe, basi, wewe utaachwa bila kuazibiwa? Hapana! Hautakosa kuazibiwa; ni lazima ukunywe hicho kikombe!

13Maana nimeapa kwa nafsi yangu kwamba muji wa Bosira utakuwa kitisho na mushangao, utakuwa uharibifu na kutumiwa kama mufano wa laana; vijiji vyote vitakuwa mabomoko siku zote.

–Ni ujumbe wa Yawe.

14Nimepata habari kutoka kwa Yawe,

na mujumbe ametumwa ayatangazie mataifa:

Mujikusanye pamoja juu ya Edomu;

musimame muende kushambulia!

15Mimi Yawe nitakufanya wewe Edomu

kuwa mudogo kuliko mataifa yote.

Ulimwengu wote utakuzarau.

16Vitisho unavyotoa na kiburi chako vimekudanganya,

ewe unayekaa katika mapango ya mawe,

unayeishi juu ya kilele cha mulima!

Ingawa unaweka makao yako juu kama ya tai,

mimi nitakuporomosha kutoka huko unakokuwa.

–Ni ujumbe wa Yawe.

17Inchi ya Edomu itakuwa kitisho na kila mutu atakayepita karibu yake atashangaa, na kuizomea kwa sababu ya hasara itakayoipata.

18Kama vile Sodoma na Gomora na miji jirani yake ilivyoangamizwa, hakutakuwa mutu yeyote atakayeishi Edomu wala kufanya mashauri humo. –Ni Yawe anayesema.–

19Kama vile simba anavyochomoka kutoka ndani ya vichaka vya muto Yordani na kuingia kwenye mbuga, ndivyo nitakavyowafukuza kwa rafla Waedomu toka katika inchi yao. Nami nitamuweka huko mutawala yeyote nitakayemuchagua. Maana, ni nani anayeweza kulinganishwa nami? Nani anayeweza kunishitaki? Ni muchungaji gani anayeweza kunipinga?

20Kwa hiyo, musikilize mupango ambao mimi Yawe nimepanga juu ya Edomu pamoja na mambo niliyokusudia kuwafanyia wakaaji wa Temani: Hakika, watoto wao wadogo watakokotwa na kukamatwa; kweli kutakuwa mushangao mukubwa katika makao yao!

21Kwa kishindo cha kuanguka kwao, dunia itatetemeka, na kilio chao kitasikilika mpaka kwenye bahari Nyekundu.

22Adui atapanda juu na kuruka kama tai na kutandaza mabawa yake juu ya Bosira. Siku hiyo moyo wa mashujaa wa Edomu utakuwa kama vile moyo wa mwanamuke anayezaa.

Neno la Mungu juu ya Damasiki

23Hii ni juu ya Damasiki:

Miji ya Hamati na Arpadi, imejaa wasiwasi

kwa kufikiwa na habari mbaya;

mioyo ya watu wake inayeyuka kwa hofu,

imefazaika kama bahari isiyoweza kutulia.

24Watu wa Damasiki wamevunjika moyo;

wamegeuka kusudi wapate kukimbia;

hofu kubwa imewashika,

uchungu na huzuni vimewapata,

kama mwanamuke anayezaa.

25Namna gani muji wenye sifa umeachwa,

muji uliokuwa umejaa furaha!

26Basi vijana wake wataanguka katika viwanja vyake,

waaskari wake wote wataangamizwa siku hiyo.

–Ni ujumbe wa Yawe wa majeshi.

27Nitawasha moto katika kuta za Damasiki,

nao utateketeza nyumba nzuri za mufalme Beni-Hadadi.

Neno la Mungu juu ya makabila ya Kedari na Hazori

28Juu ya Kedari na falme za Hazori ambazo Nebukadneza mufalme wa Babeli alizishambulia na kuzishinda, Yawe anasema hivi:

Simama uende kulishambulia kabila la Kedari!

Uwaangamize watu wa mashariki!

29Hema zao na kondoo wao vitakamatwa,

vilevile na mapazia yao na mali yao yote;

watanyanganywa ngamia wao,

na kilio kitasikilika: Kitisho kila upande!

30Mukimbie, muende mbali, mukae ndani ya mashimo.

Enyi wakaaji wa Hazori,

mukimbie, mutangetange na kujificha mbali!

–Ni ujumbe wa Yawe.–

Maana Nebukadneza mufalme wa Babeli,

amefanya mupango juu yenu,

amekusudia kuja kuwashambulia.

31Simama uende kulishambulia taifa linalostarehe,

taifa linaloishi kwa usalama.

–Ni ujumbe wa Yawe.–

Taifa hilo halina milango wala vifungio vya chuma;

ni taifa ambalo liko peke yake.

32Ngamia wao watatekwa,

makundi yao ya nyama yatanyanganywa.

Nitawasambaza kila upande,

watu wale wanaonyoa nywele zote za pembenipembeni ya kichwa.

Nitawaletea hasara kutoka kila upande.

–Ni ujumbe wa Yawe.

33Muji wa Hazori utakuwa makao ya mbweha,

utakuwa jangwa siku zote;

hakuna mutu atakayekaa humo,

wala atakayeishi humo.

Neno la Mungu juu ya Elamu

34Yawe akamutolea nabii Yeremia ujumbe huu juu ya Elamu, kwa mwanzo wa utawala wa Zedekia, mufalme wa Yuda.

35Yawe wa majeshi anasema hivi: Nitavunja upinde wa watu wa Elamu unaokuwa musingi wa nguvu zao.

36Nitaleta upepo kutoka pande zote za mbingu; nitawatawanya kila pahali, wala hakutakuwa taifa lolote ambalo halitakuwa na wakimbizi wa Elamu.

37Nitawafazaisha watu wa Elamu mbele ya waadui zao na mbele ya wale wanaotaka kuyaangamiza maisha yao. Nitawaletea hasara na hasira yangu kali.

–Ni ujumbe wa Yawe.–

Nitawashambulia kwa upanga mpaka niwaangamize kabisa.

38Nitaweka kiti changu cha kifalme huko Elamu na kumwangamiza mufalme wao pamoja na wakubwa wao.

–Ni ujumbe wa Yawe!

39Lakini katika siku za mwisho, nitaurudishia muji wa Elamu hali yake.

–Ni ujumbe wa Yawe!

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help