Isaya 42 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Mutumishi wa Mungu

1Muangalie mutumishi wangu ninayemusaidia;

muchaguliwa wangu ambaye moyo wangu umependezwa naye.

Nimeiweka roho yangu juu yake,

naye ataimarisha sheria yangu katika mataifa.

2Hatalalamika wala hatapiga kelele,

wala hatasema kwa sauti kubwa katika barabara.

3Hatavunja tete lililokunjama,

hatazimisha utambi unaotoa moshi;

ataimarisha sheria yangu kwa uaminifu.

4Yeye hataregea wala kuchoka,

mpaka atakapoimarisha sheria yangu katika dunia.

Watu wa mbali wanangojea mafundisho yake.

Mwangaza wa mataifa

5Hivi ndivyo anavyosema Yawe

aliyeumba mbingu na kuzitandika kama hema,

aliyeifanya dunia na vyote vinavyokuwa ndani yake,

anayewapa watu wanaokaa ndani yake uzima,

na kuwajalia uzima wote wanaoishi ndani yake:

6Mimi Yawe nimekuita kutenda haki,

nimekushika mukono na kukulinda.

Kwa njia yako nitafanya ahadi na watu wote,

wewe utakuwa mwangaza wa mataifa.

7Utayafungua macho ya vipofu,

utawafungua wafungwa toka katika kifungo,

utawaweka huru wale waliofungwa katika giza.

8Jina langu mimi ni Yawe;

sitamupa mwingine utukufu wangu,

wala sifa zangu sanamu za miungu.

9Mambo niliyotabiri yametukia;

na sasa ninatangaza mambo mapya,

ninakuelezea hayo mbele hayajatukia.

10Mumwimbie Yawe wimbo mupya!

Dunia yote iimbe sifa zake:

bahari na vyote vinavyokuwa ndani yake,

inchi za mbali na wakaaji wake;

11jangwa na miji yake yote vipige kelele,

vijiji vya wakaaji wa Kedari vimusifu,

wakaaji wa Sela waimbe kwa shangwe;

wapige kelele kutoka juu kwenye mulima.

12Wote wanaokaa katika inchi za mbali,

wamutukuze na kumusifu Yawe.

13Yawe anajitokeza kama shujaa;

kama vile askari katika vita anatatanua kupigana.

Anapiga kelele kubwa la vita

na kujionyesha mwenye nguvu juu ya waadui zake.

Mungu anaahidi kuwasaidia watu wake

14Yawe anasema hivi:

Kwa muda murefu sasa nimenyamaza,

nimekaa kimya na kujizuiza;

lakini sasa nitalia kama mwanamuke wakati wa kuzaa,

anayeugua pamoja na kupumua kwa nguvu.

15Nitaharibu milima na vilima,

na majani yote nitayakausha.

Mito ya maji nitaigeuza kuwa inchi kavu,

na visima vya maji nitavikausha.

16Nitawaongoza vipofu katika njia wasiyoifahamu,

nitawaongoza katika njia ambazo hawazijui.

Mbele yao nitaligeuza giza kuwa mwangaza,

na pahali penye kuharibika patakuwa laini.

Huo ndio mupango wangu wa kufanya,

nami nitautimiza.

17Wote wanaotegemea sanamu za miungu,

wote wanaoziambia “Ninyi ni miungu yetu”

watakomeshwa na kupata haya.

Waisraeli ni viziwi na vipofu

18Musikilize enyi viziwi!

Muangalie, enyi vipofu, mupate kuona!

19Nani anayekuwa kipofu isipokuwa mutumishi wangu?

Nani anayekuwa kiziwi kama mujumbe ninayemutuma?

Ni nani anayekuwa kipofu kama huyu niliyemutakasa,

au kipofu kama mutumishi wa Yawe?

20Ninyi mumeona mambo mengi,

lakini hamuelewi kitu.

Masikio yenu yako wazi,

lakini hamusikii kitu!

21Kwa ajili ya uaminifu wake, Yawe,

alipenda kutukuza sheria yake na kuiheshimisha.

22Lakini hawa ni watu walioibwa mali yao na kunyanganywa!

Wote wamenaswa katika mashimo,

wamefungwa katika kifungo.

Wamenyanganywa bila mutu wa kuwaokoa,

wamekamatwa mateka na hakuna anayesema: Muwarudishe!

23Mutatega masikio kwa kusikia kitu hiki?

Nani kati yenu atakayesikiliza vizuri yatakayotukia?

24Ni nani aliyewatia Waisraeli katika mikono ya waadui zao?

Nani aliyewaacha wanyanganywe mali zao?

Ni Yawe ambaye tumemukosea!

Wazee wetu walikataa kuzifuata njia zake,

wala hawakuzitii amri zake.

25Kwa hiyo aliwamwangia kasirani yake kali,

akawaacha kupatwa na vita kali.

Hasira yake iliwawakia kila upande,

lakini wao hawakuelewa chochote;

iliwachoma, lakini hawakufikiri juu ya jambo hilo.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help