Yobu 37 - Swahili Congo Revised Bible 2002

1Kutokana na hayo, moyo wangu unatetemeka,

na kuruka kutoka pahali pake.

2Musikilize ngurumo ya sauti ya Mungu,

na muvumo wa sauti kutoka ndani ya kinywa chake.

3Anafanya uenee chini ya mbingu yote,

anaeneza umeme wake katika pembe zote za dunia.

4Halafu sauti yake inanguruma,

sauti ya Mungu inanguruma kwa utukufu;

yeye hazuizi umeme wakati inaposikilika.

5Mungu anapiga radi ya ajabu kwa sauti yake,

anafanya mambo makubwa tusiyoweza kuyaelewa.

6Anaiambia teluji: “Anguka juu ya inchi!”

na manyunyu na mvua: “Nyesha kwa nguvu.”

7Anafunga shuguli za kila mutu

kusudi watu wote watambue kazi yake.

8Nyama wa pori wanarudi katika maficho yao

na kubaki katika mapango yao.

9Zoruba inavuma kutoka chumba chake,

na baridi kali kutoka katika gala yake.

10Kwa pumzi ya Mungu barafu inatokea,

uso wa maji unaganda kwa haraka.

11Mungu analijaza wingu manyunyu mazito;

mawingu yanasambaza umeme wake.

12Kwa amri yake vyote vinazunguka huku na kule,

kutimiza kila kitu anachoviamuru,

kufanya katika ulimwengu wa viumbe.

13Mungu anatimiza mapenzi yake katika dunia,

ikuwe ni kwa ajili ya kuwaazibu watu,

au kwa ajili ya kuonyesha wema wake.

14Unapaswa kusikiliza Yobu!

Nyamaza, usikilize maajabu ya Mungu.

15Unajua jinsi Mungu anavyovipa amri yake,

na kuyafanya umeme wa mawingu yake uangae?

16Unajua jinsi mawingu yanavyoelea katika anga?

Ndizo kazi za ajabu za yule anayekuwa mukamilifu wa maarifa!

17Wewe unajiona umevaa nguo za joto sana,

wakati upepo wa kusini unapovuma juu ya inchi.

18Unaweza kuzitandaza mbingu kama yeye

hata zikuwe ngumu kama kioo cha shaba?

19Utufundishe tutakachomwambia Mungu;

maana masemi yetu si wazi, tuko katika giza.

20Yeye anahitaji kujulishwa kwamba ninataka kusema?

Au mutu anaweza kujitakia kuangamizwa?

21Kwa rafla mutu hawezi tena kuona waziwazi:

Jua limefichwa nyuma ya mawingu,

na upepo umesafisha anga!

22Mwangaza muzuri unatokea upande wa kaskazini;

Mungu amezungukwa na utukufu wa kutisha.

23Mungu Mwenye Uwezo asiyeweza kufikiwa na mutu,

uwezo na haki yake ni mukubwa.

Amejaa haki wala hapotoshi sheria hata kidogo.

24Kwa hiyo, watu wote wanamwogopa.

Yeye hawajali watu wanaojiona kuwa wenye hekima.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help