1Kisha, Musa na Haruni wakamwendea mufalme wa Misri, wakamwambia: “Yawe, Mungu wa Israeli anasema hivi: ‘Uwaache watu wangu waondoke, wanifanyie sikukuu katika jangwa.’ ”
2Lakini mufalme wa Misri akawauliza: “Ni nani yule Yawe, hata nimusikilize na kuwaacha Waisraeli waondoke? Mimi simujui yule Yawe, wala sitawaruhusu Waisraeli waondoke.”
3Musa na Haruni wakamwambia: “Mungu wa Waebrania amekutana nasi. Tunakusihi utuache tujiendee katika jangwa mwendo wa siku tatu tutoe sadaka kwa Yawe, Mungu wetu. Kama sivyo, yeye atatuua kwa ugonjwa mukali au kwa upanga.”
4Lakini mufalme wa Misri akawajibu: “Enyi Musa na Haruni, kwa nini munajaribu kuwatoa watu kwa kazi yao? Murudie kwa kazi yenu.”
5Tena mufalme akasema: “Hawa watu ni wengi nanyi munataka waache kufanya kazi!”
6Siku hiyohiyo mufalme wa Misri aliwaamuru wakubwa pamoja na wasimamizi, akasema:
7“Tangu leo musiwape watu hawa nyasi za kutengeneza matofali kama vile inavyokuwa kawaida. Wao wenyewe watakwenda kujitafutia.
8Lakini hesabu ya matofali yanayotengenezwa kila siku ikuwe ileile, wala kusipunguke hata tofali moja, kwa sababu watu hawa ni wavivu ndio maana wanapiga kelele na kusema: ‘Utuache tuende kutoa sadaka kwa Mungu wetu.’
9Muwazidishie watu hawa kazi ngumu kusudi watoke jasho na kuacha kusema maneno ya uongo.”
10Basi, wakubwa na wasimamizi wa watu wakatoka na kuwaambia watu: “Mufalme wa Misri anasema hivi: ‘Sitawapa nyasi.
11Muende ninyi wenyewe mutafute popote mutakapoweza kuzipata, na wala kazi yenu haitapunguzwa hata kidogo.’ ”
12Basi, watu wote wakatawanyika kila pahali katika inchi ya Misri wakitafuta nyasi za kutengeneza matofali.
13Nao wakubwa wakakazana wakisema: “Mutimize kazi yenu ya kila siku kama mbele mulipoletewa nyasi.”
14Wakubwa wa Wamisri wakawapiga wasimamizi wa Waisraeli waliochaguliwa kusimamia kazi wakisema: “Kwa nini hamutimizi kazi yenu na kufikisha hesabu ileile ya matofali kama mbele?”
15Halafu wasimamizi wa Waisraeli wakamwendea mufalme, wakamulilia wakisema: “Kwa nini unatutendea hivi sisi watumishi wako?
16Hatupewi tena nyasi wakati tunalazimishwa kufyatua matofali. Tena sisi watumishi wako tunapigwa, ingawa kosa ni la watu wako.”
17Lakini mufalme wa Misri akasema: “Wavivu ninyi! Ninyi ni wavivu, ndiyo maana munasema: ‘Utuache tuende kutoa sadaka kwa Yawe’.
18Muende sasa mufanye kazi; maana hamutapewa nyasi na mutafyatua hesabu ileile ya matofali.”
19Basi, wale wasimamizi wa Waisraeli sasa walijiona kuwa katika taabu, maana waliambiwa: “Hamutapunguza hata kidogo hesabu ya matofali ya kila siku.”
20Walipoondoka kwa mufalme, wakakutana na Musa na Haruni ambao walikuwa wanawangojea.
21Basi, wakawaambia Musa na Haruni: “Yawe aone jambo hili na kuwahukumu ninyi kwa sababu mumetufanya sisi kuwa chukizo kwa mufalme wa Misri na wakubwa wake. Ninyi mumewapa sababu ya kutuua.”
22Kisha Musa akamugeukia tena Yawe, akasema: “Ee Yawe, kwa nini unawatendea watu hawa uovu? Kwa nini hata ulinituma?
23Tangu nilipokwenda na kuongea na mufalme wa Misri kwa jina lako, yeye amewatendea watu hawa uovu. Wewe haujafanya lolote kwa kuwakomboa watu wako.”
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.