1Mashairi ya Etani, Mwezra.
2Ee Yawe, nitayaimba mema yako kwa milele;
nitatangaza uaminifu wako kwa vizazi vyote.
3Nitasema kwamba wema wako unadumu kwa milele,
uaminifu wako ni imara kama mbingu.
4Wewe umesema: “Nimefanya agano na muchaguliwa wangu,
nimemwapia mutumishi wangu Daudi hivi:
5‘Siku zote nitamuweka mumoja wa wazao wako kuwa mufalme,
tena nitaudumisha ufalme wako milele.’ ”
6Ee Yawe, mbingu zinasifia maajabu yako,
uaminifu wako unasifiwa katika kusanyiko la watakatifu.
7Nani katika mbingu anayeweza kulinganishwa nawe, ee Yawe?
Nani anayekuwa sawa nawe kati ya miungu?
8Wewe unatisha katika baraza la watakatifu;
wote wanaokusanyika mbele yako wanakuheshimu na kukuogopa.
9Ee Yawe, Mungu wa majeshi,
ni nani mwenye nguvu kama wewe?
Ee Yawe, uaminifu umekuzunguka pande zote.
10Wewe unaamuru machafuko ya bahari;
mawimbi yake yakiinuka, unayatuliza.
11Ulimuponda nyama mukubwa Rahaba na kumwua;
uliwatawanya waadui zako kwa nguvu yako.
12Mbingu ni zako na dunia ni yako pia;
ni wewe uliyeumba ulimwengu na vyote vinavyokuwa ndani yake.
13Wewe uliumba kaskazini na kusini;
milima Tabori na Hermoni inakushangilia.
14Mukono wako unajaa nguvu,
mukono wako una nguvu na umeshinda!
15Haki na sheria ndio musingi wa utawala wako;
wema na uaminifu vinakutangulia!
16Heri watu wanaojua kukushangilia,
wanaoishi katika mwangaza wa wema wako, ee Yawe.
17Wanafurahi muchana kutwa kwa sababu yako,
na kukusifu kwa ajili ya haki yako.
18Wewe ndiwe utukufu na nguvu yao;
kwa upendo wako tunapata ushindi.
19Ee Yawe, ngao yetu ni chini ya ulinzi wako.
Mufalme wetu ametoka kwako, ewe Mutakatifu wa Israeli.
Ahadi ya Mungu kwa Daudi20Zamani ulisema katika maono,
ukawaambia watumishi wako waaminifu:
“Nimemupa nguvu shujaa mumoja,
nimemwinua huyo niliyemuchagua kati ya watu.
21Nimemupata mutumishi wangu Daudi;
nimemuchagua kwa kumupakaa mafuta yangu matakatifu.
22Mukono wangu wa nguvu utakuwa naye siku zote;
mukono wangu mimi mwenyewe utamwimarisha.
23Waadui hawataweza kumushinda,
wala waovu hawatamwonea.
24Mimi nitawaponda wapinzani wake;
nitawaangamiza wote wanaomuchukia.
25Nitakuwa mwaminifu na mwema kwake.
Kwa jina langu atapata ushindi mukubwa.
26Nitaongeza nguvu na utawala wake,
kutoka bahari ya Mediteranea mpaka muto Furati.
27Yeye atasema, ‘Wewe ni
baba yangu,
Mungu wangu,
mulima wa wokovu wangu.’
28Nami nitamufanya kuwa muzaliwa wangu wa kwanza,
mukubwa kuliko wafalme wote wa dunia.
29Nitamwonyesha wema wangu kwa milele,
na agano langu kwake litadumu siku zote.
30Nitaudumisha ukoo wake wa kifalme siku zote,
nao ufalme wake kama mbingu.
31“Lakini wazao wake wakiiacha sheria yangu,
wasipoishi kufuatana na maagizo yangu,
32kama wakivunja masharti yangu,
na kuacha kutii amri zangu,
33hapo nitayaazibu makosa yao;
nitawapiga kwa sababu ya maovu yao.
34Lakini sitaacha kumutendea mema Daudi,
wala sitavunja uaminifu wangu kwake.
35Sitavunja agano langu naye,
wala kugeuza neno nililosema kwa mudomo wangu.
36“Nimeapa mara moja tu kwa utakatifu wangu;
nami sitamwambia Daudi uongo.
37Ukoo wake utadumu milele,
nao ufalme wake kama jua.
38Utadumu milele kama mwezi
unaokuwa mushuhuda mwaminifu asiyetoka katika anga.”
Masikitiko ya sasa39Lakini sasa, ee Mungu, umemutupa na kumukataa,
umejaa kasirani juu ya huyo uliyemuchagua.
40Umefuta agano ulilofanya na mutumishi wako;
umeitupa taji yake ya kifalme ndani ya mavumbi.
41Umebomoa kuta zote za muji wake;
umezivunjavunja nafasi zake za kukimbilia.
42Wote wanaopita wanaiba mali zake;
wajirani zake wanamuzarau.
43Umewapatia waadui ushindi;
umewafurahisha waadui zake wote.
44Umepoteza ukali wa silaha zake;
ukamwachilia ashindwe katika vita.
45Umemuvua madaraka yake ya kifalme,
ukauangusha utawala wake chini.
46Umezipunguza siku za ujana wake,
ukamufunika haya tele.
Kuomba usalama47Ee Yawe, utajificha hata milele?
Mpaka wakati gani hasira yako itawaka kama moto?
48Unikumbuke, ee Bwana. Maisha ni mafupi!
Umewaumba wanadamu wote kwa bure?
49Ni mutu gani anayeweza kuishi pasipo kufa?
Nani anayeweza kujiepusha na kifo?
50Ee Bwana, yako wapi yale mema yako ya zamani
uliyomwahidi Daudi kwa uaminifu wako?
51Ee Bwana, ukumbuke matusi ya mutumishi wako,
jinsi ninavyovumilia mazarau ya mataifa.
52Ee Yawe, ona jinsi wanavyomuzomea muchaguliwa wako.
Wanamuzomea kila fasi anapokwenda.
53Yawe asifiwe milele!
Amina! Amina!
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.