1 Mambo ya Siku 16 - Swahili Congo Revised Bible 2002

1Kisha wakaingiza Sanduku la Agano, na kuliweka ndani ya hema ambayo Daudi alikuwa ametayarisha. Halafu wakatoa sadaka za kuteketezwa kwa moto na za amani mbele ya Mungu.

2Daudi alipomaliza kutoa sadaka hizo za kuteketezwa na za amani, akawabariki watu katika jina la Yawe,

3na akawagawanyia Waisraeli wote, wanaume na wanawake, kila mumoja akapewa mukate, kipande cha nyama na mukate wa zabibu.

4Zaidi ya hayo, Daudi akaweka Walawi wamoja kwa kazi mbele ya Sanduku la Agano la Yawe, wamutukuze, wamutolee shukrani na wamusifu Yawe, Mungu wa Israeli.

5Akamuchagua Asafu kuwa kiongozi wao, akisaidiwa na Zekaria. Yeieli, Semiramoti, Yehieli, Metitia, Eliabu, Benaya, Obedi-Edomu na Yehieli, akawachagua wakuwe wapiga vinanda na vinubi. Asafu alipiga matoazi,

6nao makuhani Benania na Yaharieli, wakachaguliwa wakuwe wakipiga baragumu kwa mufululizo mbele ya Sanduku la Agano la Mungu.

7Basi, hiyo ikakuwa siku ambayo kwa mara ya kwanza, Daudi alimupa Asafu na wandugu zake Walawi kazi ya kumwimbia Yawe nyimbo za shukrani.

Wimbo wa Sifa(Zab 105.1-15; 96.1-13; 106.1,47-48)

8Mutangaze ukubwa wa Yawe,

mujulishe mataifa mambo aliyoyatenda!

9Mushangilie, mumwimbie Mungu sifa;

mueleze matendo yake ya ajabu!

10Mujisifu kwa ajili ya jina lake takatifu;

wanaomutafuta Yawe wafurahi.

11Mumutafute Yawe mwenye nguvu;

mumutafute Yawe siku zote.

12Mukumbuke matendo ya ajabu aliyotenda,

maajabu yake na hukumu alizotoa,

13enyi wazao wa Abrahamu, mutumishi wake,

enyi wazao wa Yakobo, wachaguliwa wake.

14Yeye Yawe, ndiye Mungu wetu;

hukumu zake zina nguvu katika dunia yote.

15Yeye anashika agano lake milele,

anatimiza ahadi zake kwa vizazi elfu.

16Anashika agano alilofanya na Abrahamu,

na ahadi aliyomwapia Isaka.

17Alimusimamishia Yakobo ahadi yake,

akamuhakikishia agano hilo la milele.

18Alisema: “Nitawapa inchi ya Kanana,

nayo itakuwa mali yenu wenyewe.”

19Hesabu yenu ilikuwa ndogo,

mulikuwa wachache na wageni katika inchi ya Kanana,

20mukitangatanga toka taifa hata taifa,

kutoka inchi moja hata inchi ingine.

21Mungu hakumuruhusu mutu yeyote awatese;

kwa ajili yao aliwaonya wafalme:

22“Musiwaguse wachaguliwa wangu;

musiwazuru manabii wangu!”

23Mumwimbie Yawe, ulimwengu wote.

Mutangaze kila siku matendo yake ya wokovu.

24Mutangazie mataifa utukufu wake,

muwaelezee watu wote matendo yake ya ajabu.

25Maana Yawe ni mukubwa, anasifika sana

anastahili kuheshimiwa kuliko miungu yote.

26Miungu yote ya mataifa mengine si kitu;

lakini Yawe ndiye aliyeumba mbingu.

27Utukufu na sifa vinamuzunguka,

nguvu na furaha vinajaza pahali pake.

28Mumupe Yawe heshima, enyi jamii zote za watu,

mutangaze utukufu na nguvu yake.

29Mumupe Yawe heshima ya utukufu wa jina lake;

mulete sadaka na kuingia katika nyumba yake.

Mumwabudu Yawe katika Pahali Patakatifu pake.

30Ee dunia yote; tetemeka mbele yake!

Ameweka ulimwengu imara, hautatikisika.

31Mufurahi enyi mbingu na dunia!

Muambie mataifa: “Yawe anatawala!”

32Bahari ivume, pamoja na vyote vinavyokuwa mule!

Mufurahi enyi mashamba na vyote vinavyokuwa mule!

33Halafu miti yote katika pori

itaimba kwa furaha

mbele ya Yawe anayekuja

kuihukumu dunia.

34Mumushukuru Yawe!

Yeye ni muzuri,

wema wake unadumu milele!

35Mumwambie Yawe:

utuokoe, ee Mungu wa wokovu wetu,

utukusanye pamoja na kutuokoa kutoka kwa mataifa,

tupate kulisifu jina lako takatifu,

kuona utukufu juu ya sifa zako.

36Asifiwe Yawe, Mungu wa Israeli,

tangu milele na hata milele!

Kisha watu wote wakasema: “Amina!” Wakamusifu Yawe vilevile.

Ibada kule Yerusalema na Gibeoni

37Halafu, mufalme Daudi akawaacha Asafu na wandugu zake Walawi pahali walipoliweka Sanduku la Agano la Yawe, kwa ajili ya kazi zinazotakiwa mbele ya sanduku kila siku.

38Obedi-Edomu mwana wa Yedutuni, pamoja na wenzake makumi sita na wanane waliwasaidia. Obedi-Edomu mwana wa Yedutuni na Hosa walikuwa walinzi wa milango.

39Mufalme Daudi akawaweka kuhani Zadoki na makuhani wenzake kuwa watumishi wa hema ya Yawe iliyokuwa pahali pa kuabudia kule Gibeoni

40kwa kutolea Yawe sadaka za kuteketezwa kwa moto juu ya mazabahu ya sadaka za kuteketezwa kwa moto siku zote asubui na magaribi, kulingana na yote yaliyoandikwa katika sheria ambayo Yawe aliyowaamuru Waisraeli.

41Pamoja nao kulikuwa Hemani na Yedutuni na wale wote waliochaguliwa, waliotajwa majina yao, kwa kumushukuru Yawe kwa sababu wema wake unadumu milele.

42Hemani na Yedutuni walikuwa na baragumu na matoazi kwa ajili ya muziki na ala za muziki kwa ajili ya nyimbo takatifu. Wana wa Yedutuni walichaguliwa kwa kulinda milango.

43Kisha, kila mutu akaondoka kwenda kwake; naye Daudi akaenda kwake kwa kuibariki jamaa yake.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help