Zaburi 68 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Wimbo wa ushindi

1Kwa mukubwa wa waimbaji. Zaburi ya Daudi.

2Mungu asimame sasa, na waadui zake watawanyike!

Wanaomuchukia wakimbie mbali naye!

3Kama moshi unavyopeperushwa na upepo,

ndivyo nao wanavyopeperushwa;

kama inta inavyoyeyuka karibu na moto,

ndivyo waovu wanavyoangamia mbele ya Mungu!

4Lakini watu wa haki wanafurahi Mungu anapokuja,

wanashangilia na kuimba kwa furaha.

5Mumwimbie Mungu, musifu jina lake;

mumutengenezee njia yeye anayetembea juu ya mawingu.

Jina lake ni Yawe; mufurahi mbele yake.

6Mungu anayekaa pahali pake patakatifu,

ni Baba ya wayatima na mulinzi wa wajane.

7Mungu anawapatia wenye ukiwa jamaa,

anawafungua wafungwa na kuwapa uheri.

Lakini waasi wataishi katika inchi yenye kukauka.

8Ee Mungu, ulipowaongoza watu wako,

uliposafiri kule katika jangwa,

9dunia ilitetemeka, mbingu zilitiririsha mvua;

mbele yako, Mungu wa Sinai,

mbele yako, Mungu wa Israeli!

10Ee Mungu, ulinyeshea inchi mvua nyingi,

ulitia tena inchi yako nguvu ilipokuwa imechakaa.

11Watu wako wakapata makao ndani yake,

uliyotayarishia wamasikini kwa uzuri wako.

12Bwana alitoa amri,

nao wanawake wengi wakatangaza habari:

13“Wafalme na majeshi yao wanakimbia ovyo!”

Wanawake waliobaki ndani ya nyumba

waligawanya vitu vilivyonyanganywa,

14ingawa walibaki ndani ya mazizi:

sanamu za njiwa zilizotengenezwa na feza,

na mabawa yao yanayoangaa zahabu.

15Mungu Mukubwa alipowatawanya wafalme,

teluji ilianguka juu ya mulima Salmoni.

16Ewe mulima wa Basani,

murefu na wenye vichwa vingi,

17mbona unauonea kijicho

mulima Mungu aliouchagua akae juu yake?

Yawe atakaa huko milele!

18Bwana anakuja kwenye pahali pake patakatifu kutoka Sinai,

akikuwa na kundi kubwa,

na maelfu na maelfu ya magari ya kukokotwa.

19Anapanda juu akichukua wafungwa,

anapokea zawadi kutoka kwa watu,

hata kutoka kwa watu walioasi,

Yawe apate kukaa huko.

20Yawe asifiwe siku kwa siku!

Yeye anatubebea mizigo yetu,

yeye ndiye Mungu mwokozi wetu.

21Mungu wetu ni Mungu mwenye kutuokoa;

Bwana wetu Yawe pekee ndiye anayeokoa katika kifo.

22Mungu ataviponda vichwa vya waadui zake,

ndivyo vichwa vya wanaoendelea katika njia mbaya.

23Bwana wetu alisema: “Nitawarudisha waadui kutoka Basani;

nitawarudisha kutoka shimo la bahari,

24usafishe miguu katika damu ya waadui zako,

nao imbwa wako wapate posho yao.”

25Ee Mungu, maandamano yako ya ushindi yanaonekana;

maandamano ya Mungu wangu, mufalme wangu,

katika pahali patakatifu!

26Mbele waimbaji, nyuma wanamuziki,

katikati wabinti wanavumisha ngoma.

27“Mumusifu Mungu katika mukutano.

Mumusifu Yawe, enyi wazao wa Israeli!”

28Kwanza ni Benjamina, mudogo wa wote;

kisha waongozi wa Yuda na kundi lao,

halafu wakubwa wa Zebuluni na Nafutali.

29Onyesha, ee Mungu, nguvu yako kubwa;

nguvu yako uliyotumia kwa ajili yetu.

30Kutoka katika hekalu lako, Yerusalema,

ambapo wafalme watakufikia na zawadi zao,

31uwakaripie wale nyama wanaokaa katika matete,

kundi la mabeberu na ngombe dume,

mpaka mataifa hayo yakupe heshima na kodi.

Uwatawanye hao watu wenye kupenda vita!

32Wajumbe watakuja kutoka Misri,

Waetiopia watamuletea Mungu mali zao.

33Enyi falme za dunia, mumwimbie Mungu,

mumwimbie Bwana wetu nyimbo za sifa,

34mumwimbie yeye anayepita katika mbingu,

mbingu za tangu zamani.

Mumusikilize akinguruma kwa kishindo.

35Mutambue nguvu za Mungu;

yeye anatawala juu ya Israeli,

mamlaka yake yanafika katika mbingu.

36Mungu ni wa kutisha tangia pahali pake patakatifu,

yeye ni Mungu wa Israeli!

Anawapa watu wake nguvu na uwezo.

Mungu asifiwe!

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help