Yeremia 2 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Mungu anawalinda Waisraeli

1Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi:

2Kwenda uwatangazie waziwazi wakaaji wote wa Yerusalema na kusema hivi:

Yawe anasema hivi:

Ninakumbuka wema wako ulipokuwa kijana,

jinsi ulivyonipenda kama muchumba wako.

Ulinifuata katika jangwa

kwenye inchi ambayo haikupandwa kitu.

3Israeli, ulikuwa wangu wa pekee,

kama malimbuko ya shamba langu.

Wote waliokukula walibeba hukumu,

wakipatwa na hasara.

–Ni ujumbe wa Yawe.

Zambi ya babu za Waisraeli

4Musikilize neno la Yawe, enyi wazao wa Yakobo.

Musikilize, enyi jamaa zote za wazao wa Israeli.

5Yawe anasema hivi:

Babu zenu waliona kosa gani kwangu

hata wakanigeuka na kuniacha,

wakakimbilia miungu ya bure,

hata nao wakakuwa watu bure?

6Hawakujiuliza hivi:

Yuko wapi Yawe aliyetuondoa katika inchi ya Misri,

aliyetuongoza katika mbuga,

katika inchi ya jangwa na mashimo,

inchi inayokauka na yenye giza kubwa,

inchi isiyopitiwa na mutu yeyote,

wala kukaliwa na mwanadamu?

7Niliwaleta katika inchi yenye mboleo,

muyafurahie mazao yake na mema yake mengine.

Lakini mulipofika tu, muliichafua inchi yangu;

inchi niliyowapa ikuwe yenu, mukaifanya chukizo.

8Nao makuhani hawakujiuliza hivi: Yuko wapi Yawe?

Wafundi wa sheria hawakunijua,

viongozi wa watu waliniasi;

manabii nao walitabiri kwa jina la Bali

na kuabudu sanamu zisizokuwa na faida yoyote.

Mashitaki ya Yawe juu ya watu wake

9Kwa hiyo, mimi nitawashitaki ninyi,

na nitawashitaki wazao wenu.

–Ni ujumbe wa Yawe.–

10Basi muvuke bahari mpaka Kipuro, muone,

au mutume watu huko Kedari wachunguze,

kama jambo kama hili limekwisha kutokea.

11Kuna taifa ambalo limekwisha kubadilisha miungu yao

ingawa miungu hiyo si miungu?

Lakini watu wangu wameniacha mimi, utukufu wao,

wakafuata miungu isiyokuwa na faida yoyote.

12Kwa hiyo mushangae, enyi mbingu,

muogope na kufazaika kabisa.

–Ni ujumbe wa Yawe.–

13Watu wangu wametenda maovu mawili;

wameniacha mimi ninayekuwa chemichemi ya maji ya uzima,

wakajichimbia visima vyao wenyewe,

visima vyenye nyufa, visivyoweza kuchunga maji.

Matokeo ya kukosewa uaminifu kwa Waisraeli

14Israeli ni mutumwa,

au amezaliwa mutumwa?

Hapana! Kwa nini basi amekuwa kama nyama anayewindwa?

15Simba wananguruma kwa ajili yake,

wananguruma kwa sauti kubwa.

Wameiharibu kabisa inchi yake,

miji yake imebaki mabomoko pasipo watu.

16Hata watu wa Nofi na Tahapanesi,

wamenyoa nywele ya kichwa chake.

17Israeli, si wewe mwenyewe uliyejiletea hayo yote,

kwa kuniacha mimi Yawe, Mungu wako,

niliyekuwa ninakuongoza katika njia?

18Na sasa itakufalia nini kwenda Misri

kunywa maji ya muto Nili?

Au itakufalia nini kwenda Asuria

kunywa maji ya muto Furati?

19Uovu wako utakuazibu;

na uasi wako utakuhukumu.

Ujue na kutambua kwamba ni vibaya sana

kuacha Bwana wako Yawe, Mungu wako,

na kutokuwa na woga wangu ndani yako.

–Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe wa majeshi.–

Israeli anakataa kumwabudu Yawe

20Yawe anasema: Tangu zamani wewe ulivunja nira yako,

ulikata minyororo yako,

ukasema: “Sitakutumikia”.

Juu ya kila kilima kirefu

na chini ya kila muti wa majani mabichi,

ukalala machali kama kahaba.

21Lakini mimi nilikupanda kama mizabibu uliochaguliwa,

muzabibu wenye afya na wa mbegu safi.

Mbona basi umeharibika,

umegeuka kuwa muzabibu wa bure wa pori?

22Hata ukijisafisha kwa dawa ya kutosha taka

na kutumia sabuni nyingi,

madoa ya uovu wako yatabaki mbele yangu.

–Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.

23Namna gani basi unaweza kusema:

Mimi sikujichafua

wala sikufuata miungu Bali.

Ukumbuke vile ulivyotenda zambi kule katika bonde;

utambue yale uliyofanya huko!

Wewe ni kama mwana wa ngamia,

anayetangatanga huko na huko;

24kama punda dike wa pori aliyezoea jangwa.

Katika tamaa yake ananusanusa upepo;

nani anayeweza kumuzuiza katika hamu yake?

Dume anayemutamani hahitaji kujisumbua;

wakati wake unapofika watamupata tu.

25Israeli, usiichubue miguu yako

wala usilikaushe koo lako.

Lakini wewe unasema: Hakuna tumaini lolote.

Ninapenda miungu ya kigeni,

hiyo ndiyo nitakayoifuata.

26Kama vile mwizi anavyofezeheka anaponaswa,

ndivyo Waisraeli watakavyofezeheka;

wao wenyewe, wafalme wao, wakubwa wao,

makuhani wao na manabii wao.

27Wao wanauambia muti: “Wewe ni baba yetu”,

nalo jiwe: “Wewe ndiwe uliyetuzaa”;

kwa maana unanigeuzia mugongo,

wala hawakunielekezea uso.

Lakini wakati wa shida wanasema: Simama utuokoe!

28Lakini iko wapi ile miungu yenu muliyojifanyia?

Basi kama inaweza, isimame iwasaidie,

wakati munapokuwa katika shida.

Ee ninyi watu wa Yuda, hesabu ya miungu yenu

ni sawa na hesabu ya miji yenu!

29Kwa nini basi munanilalamikia?

Ninyi wote mumeniasi.

–Ni ujumbe wa Yawe.–

30Niliwaazibu ninyi lakini ilikuwa bure,

ninyi munakataa maonyo.

Muliwateketeza manabii wenu kwa upanga

kama simba mwenye uchu.

31Enyi watu! Musikilize vile mimi Yawe ninavyosema:

Nimekuwa kama vile jangwa

au inchi yenye giza kubwa?

Kwa nini basi watu wangu wanasema:

Sisi tuko watu huru;

hatutakurudilia!

32Kijana binti anaweza kusahau mapambo yake,

au bibi arusi nguo yake?

Lakini watu wangu wamenisahau

kwa muda wa siku zisizohesabika.

33Kweli wewe ni bingwa wa kutafuta wapenzi!

Hata wanawake waovu unawafundisha njia zako.

34Juu ya nguo zako kuna damu ya wamasikini wasiokuwa na kosa,

ijapokuwa haukuwakuta wakivunja nyumba yako.

Na zaidi ya hayo yote,

35wewe unasema: Mimi sina kosa;

hakika hasira yake imegeuka mbali nami.

Lakini mimi nitakuhukumu

kwa sababu unasema kwamba haukutenda zambi.

36Kwa nini unaniachilia hivi,

ukibadilishabadilisha mwenendo wako?

Utafezeheshwa na Misri

kama ulivyofezeheshwa na Asuria.

37Na huko vilevile utatoka na haya,

mikono ikiwa juu ya kichwa.

Mimi Yawe nimewakataa wale uliowategemea,

wala hautafanikiwa kwa musaada wao.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help