1Mutu wa haki akikufa,
hakuna mutu anayejali;
mutu mwema akihamishwa toka dunia,
hakuna mutu anayefikiri na kusema:
Mutu huyo mwema amehamishwa kusudi asipatwe na hasara,
2kusudi apate kuingia kwenye amani.
Watu wenye mwenendo sawa,
watakuwa na amani na kupumzika.
3Lakini Yawe anasema:
Mukuje hapa ninyi wana wa wake wachawi;
ninyi wazao wa wachawi, wazinzi na makahaba.
4Ni nani munayemuchekelea?
Munamuzomea nani na kumutoshea ulimi inje?
Ninyi wenyewe ni waasi tangu mwanzo,
ninyi ni kizazi kidanganyifu.
5Ninyi munawaka tamaa kwenye miti ya mialo,
na chini ya kila muti wenye kuwa na majani mabichi.
Munawachinja watoto wenu
na kuwatambikia katika mabonde na ndani ya nyufa za mawe.
6Munachagua mawe laini katika mabonde,
na kuyafanya kuwa mungu wenu.
Munayamwangia sadaka ya kinywaji
na kuyapelekea sadaka ya unga!
Mimi nitatulizwa kwa vitu hivyo?
7Mumeweka vitanda vyenu juu ya milima mirefu,
na kwenda kule kwa kutambikia.
8Nyuma ya milango na miimo
mumetundika sanamu yenu.
Ninyi munaniacha mimi.
Mumevua nguo zenu na kupanda juu ya vitanda vyenu vipana.
Mumelipa wapenzi wenu ambao munataka kulala nao.
Halafu munatimiza tamaa zenu mbaya.
9Munajipakaa marasi na mafuta kwa wingi
kisha munakwenda kumwabudu Moleki.
Munawatuma wajumbe wenu huko na huko,
kujitafutia miungu ya kuabudu;
hata kuzimu walifika.
10Mulichoka na safari zenu ndefu,
hata hivyo hamukukata tamaa;
mulijipatia nguvu mupya,
ndiyo maana hamukuzimia.
11Mulimwogopa na kutishwa na nani
hata mukasema uongo,
mukaacha kunikumbuka mimi
na kuacha kabisa kufikiri juu yangu?
Mimi sikuwaambia kitu kwa muda murefu;
ndiyo maana labda mukaacha kuniheshimu!
12Munafikiri kwamba munafanya sawa,
lakini nitayafichua matendo yenu,
nayo miungu yenu haitawafalia kitu.
13Mutakapolia kwa kuomba musaada,
basi ile lundo ya sanamu zenu iwaokoe!
Upepo utavipeperushia mbali;
pumzi itavitupilia mbali.
Lakini watakaotafuta kimbilio kwangu,
watarizi inchi,
mulima wangu mutakatifu utakuwa mali yao.
Huruma ya Mungu14Yawe anasema hivi:
Mujenge! Mujenge! Mutayarishe njia!
Muondoe vikwazo vyote katika njia ya watu wangu!
15Hivi ndivyo anavyosema Mungu anayekuwa juu kabisa,
anayeishi milele na ambaye jina lake ni Mutakatifu:
Mimi ninakaa kule juu, Pahali Patakatifu,
ninakaa vilevile na wenye majuto na wanyenyekevu.
Mimi nitawatia moyo wanaokuwa wanyenyekevu
na kuwapa nguvu wenye majuto.
16Maana sitaendelea kugombana
wala kuwakasirikia siku zote,
maana hao niliowaumba watazimia mbele yangu,
nami ndiye niliyewapa pumzi yangu ya uzima.
17Niliwakasirikia kwa sababu ya uovu na tamaa zao;
niliwaazibu, nikauficha uso wangu na kukasirika.
Lakini wao waliendelea kufuata njia zao wenyewe.
18Niliona mwenendo wao, lakini nitawaponyesha;
nitawaongoza na kuwapa faraja,
nitawatuliza hao wanaoomboleza.
19Mimi nitawapa amani,
amani kwa wanaokuwa mbali na wanaokuwa karibu!
–Ni Yawe anayesema hivyo.–
Mimi nitawaponyesha.
20Lakini waovu ni kama bahari iliyochafuka,
ambayo haiwezi kutulia;
maji yake yanatupa matope na takataka.
21Mungu wangu anasema hivi:
Hakuna amani kwa watu waovu.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.