Wagalatia 6 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Kusaidiana kwa kubeba mizigo

1Wandugu zangu, kama mutu akipatikana na kosa fulani, ninyi munaoongozwa na Roho wa Mungu mumwonye mutu yule kwa roho ya upole. Na kila mumoja wenu ajiangalie mwenyewe, kusudi asijaribiwe vilevile.

2Musaidiane ninyi kubeba mizigo yenu, na hivi mutatimiza sheria ya Kristo.

3Kama mutu akijizania kwamba yeye ni kitu, ijapokuwa yeye si kitu, anajidanganya yeye mwenyewe.

4Kila mutu achunguze mwenendo wake mwenyewe. Basi akiwa na sababu ya kujivuna, ajivune kufuatana na mwenendo wake mwenyewe pasipo kujilinganisha na mutu mwingine.

5Kwa maana kila mutu anapaswa kubeba muzigo wake mwenyewe.

6Mwenye kufundishwa Habari Njema anapaswa kushirikiana mapato yake na yule anayemufundisha.

7Musidanganyike: Mungu hachekelewi. Chochote mutu atakachopanda, ndicho atakachovuna.

8Anayepanda kwa kupendeza hali yake ya kimwili, atavuna matunda yanayotokana na hali ile, nayo ni lufu. Lakini anayepanda kwa kupendeza Roho Mutakatifu, atavuna matunda yanayotokana na Roho yule, nayo ni uzima wa milele.

9Tusichoke kutenda mema; kwa maana siku zitakapotimia tutavuna kama tusiporegea.

10Basi, tunapokuwa bado na wakati, tufanye mema kwa watu wote, na zaidi kwa wandugu zetu katika imani.

Maonyo ya mwisho na kutakiana heri

11Mujionee wenyewe ni kwa herufi kubwa gani nimewaandikia ninyi kwa mukono wangu mwenyewe!

12Wale watu wanaowalazimisha ninyi kutahiriwa, ndio wanaotaka kujionyesha katika mambo yanayoelekea mwili. Lakini wanafanya vile tu kusudi wasiteswe kwa ajili ya kuhubiri habari za musalaba wa Kristo.

13Watu hao wanaotahiriwa, hawashiki Sheria lakini wanataka mutahiriwe kusudi wapate kujivuna kwamba wanawashurutisha kuwa na kitambulisho kile juu ya mwili wenu.

14Na mimi kwa ngambo yangu sitaki kujivuna, isipokuwa tu kwa ajili ya musalaba wa Bwana wetu Yesu Kristo. Maana kwa njia ya musalaba huo, ninahesabu dunia kama vile imekwisha kufa na mbele ya dunia mimi ninahesabiwa kama vile mufu.

15Kutahiriwa au kutokutahiriwa hakufai kitu; kitu cha lazima ni kuwa kiumbe kipya.

16Na wote wanaofuata kanuni hii katika maisha yao pamoja na watu wa Mungu wanaohesabiwa kama Waisraeli wa kweli, ninawatakia amani na wema.

17Basi sasa, mutu asinisumbue tena kwa maana niko na makovu juu ya mwili wangu niliyopata kwa ajili ya Yesu.

18Wandugu, ninawatakia ninyi wote neema kutoka kwa Bwana wetu Yesu Kristo. Amina.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help