Isaya 59 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Nabii analaani zambi za watu

1Musifikiri kwamba mukono wa Mungu ni mufupi,

hata asiweze kuwaokoa,

au kwamba masikio yake yamefungana,

hata asiweze kuwasikiliza ninyi.

2Zambi zenu ndizo zinazowatenga na Mungu wenu,

zambi zenu zimemufanya ajifiche mbali nanyi

hata asiweze kuwasikiliza ninyi.

3Maana mikono yenu imechafuka kwa damu,

na vidole vyenu kwa matendo maovu.

Midomo yenu imesema uongo,

na ndimi zenu zinasema uovu.

4Hakuna anayemushitaki mwenzake kwa haki,

wala anayejitetea kwa ukweli.

Munategemea mambo ya bure; munasema uongo.

Munafanya mipango ya kuleta hasara na kuzaa uovu.

5Munatoa mayai ya nyoka yenye sumu,

munafuma wavu wa buibui.

Anayekula mayai yenu anakufa,

na yakipasuliwa, nyoka anatokea ndani yake.

6Wavu wenu haufai kama nguo,

watu hawawezi kujifunikia munachofuma.

Kazi zenu ni kazi za uovu,

matendo yenu yote ni mateso makali.

7Muko mbio kutenda maovu,

muko wepesi kumwanga damu isiyokuwa na kosa.

Mawazo yenu ni mawazo ya uovu,

popote munapokwenda munaacha ukiwa na uharibifu.

8Njia ya amani hamuijui hata kidogo;

hamufuati sheria ya Mungu.

Mumejifanyia njia potovu,

yeyote anayepitia humo hapati amani.

Watu wanatambua zambi yao

9Kwa hiyo, kufuata sheria ya Mungu kuko mbali nasi,

haki haifiki kwetu.

Tulitazamia kupata mwangaza, kumbe ni giza tupu;

tulingojea mwangaza, lakini tunatembea katika giza.

10Kama vipofu tunapapasapapasa ukuta;

tunasitasita kama watu wasiokuwa na macho.

Tunajikwaa muchana kati, sawa vile ni usiku;

kati ya wenye afya, sisi ni kama wafu.

11Tunanguruma kama dubu,

tunaomboleza kama njiwa.

Tunatazamia watu wanaofuata sheria ya Mungu, lakini hakuna,

tunatazamia wokovu, lakini uko mbali nasi.

12Makosa yetu mbele yako ni mengi sana,

zambi zetu zinashuhudia juu yetu.

Kweli, makosa yetu yanaandamana nasi,

tunayajua maovu yetu.

13Tumekuasi na kukukana, ee Yawe,

tumekataa kukufuata, ewe Mungu wetu.

Tunasema maneno ya kutesa na uasi,

katika mioyo yetu tunatunga na kutoa maneno ya uongo.

14Sheria ya Mungu imewekwa pembeni,

haki iko mbali;

ukweli unakanyagwa katika tribinali,

usawa hauwezi kuingia humo.

15Ukweli umekosekana,

naye anayeacha uovu ananyanganywa.

Mungu anajitayarisha kuwakomboa watu wake

Mungu aliona mambo hayo.

Alichukizwa kwamba watu hawafuati sheria yake.

16Aliona kwamba hakuna mutu aliyejali,

akashangaa kwamba hakuna aliyeingilia kati.

Basi akaamua kunyoosha mukono wake mwenyewe,

haki yake ikamusaidia.

17Alivaa haki kama vile nguo ya kujikinga kifua,

na wokovu kama kofia ya chuma juu ya kichwa.

Alivaa nguo ya kulipiza kisasi,

na kujifunika na kanzu ya wivu.

18Atawaazibu waadui kadiri ya matendo yao,

kasirani yake na kisasi vitawapata waadui zake;

atawaazibu hata wakaaji wa inchi za mbali.

19Toka magaribi mpaka mashariki,

kila mutu atamwogopa Yawe

na kutambua utukufu wake.

Maana atakuja kama muto wenye kuporomoka mbio,

muto unaosukumwa kwa upepo wa Yawe.

20Naye atakuja katika Sayuni kama Mukombozi,

Mukombozi wa wazao wa Yakobo

ambao wataachana na makosa yao.

–Ni ujumbe wa Yawe.

21Yawe anasema:

Mimi ninafanya nanyi agano hili:

Roho wangu anayekuwa juu yenu,

maneno niliyoyaweka katika kinywa chenu,

hayataondoka kwenu hata kidogo,

wala kwa watoto na wajukuu wenu,

tangu sasa na hata milele.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help