Waebrania 6 - Swahili Congo Revised Bible 2002

1-3Basi kwa sababu hii, tuache mafundisho ya mwanzo juu ya Kristo. Tusijenge tena musingi mupya wa mambo haya: kugeuka toka katika matendo yasiyofaa, kumwamini Mungu, namna mbalimbali za ubatizo, kuwawekea watu mikono, ufufuko na hukumu ya milele. Tuendelee katika mafundisho makamilifu. Tutafanya hivi, Mungu akitaka.

4Maana watu wanapokwisha kuangaziwa na ukweli wa Mungu na kuonja zawadi ya mbinguni, na kuishi katika ushirika na Roho Mutakatifu,

5wanapokwisha kuonja wema wa Neno la Mungu na nguvu za ulimwengu utakaokuja,

6kisha wakianguka, haiwezekani kuwarudisha hata wapate kugeuka mara ingine toka katika matendo yao mabaya. Kwa sababu wamemutundika wao wenyewe Mwana wa Mungu mara ya pili na kumupatisha haya mbele ya watu.

7Udongo unaonyeshewa na mvua mara kwa mara na kutoa mimea inayofaa kwa walimaji, unabarikiwa na Mungu.

8Lakini kama ukitoa miiba na magugu, udongo ule haufai kitu nao uko karibu ya kulaaniwa na Mungu, tena mwisho wake ni kuteketezwa.

9Lakini wapendwa wangu, ijapokuwa tunasema hivi, hatuna mashaka juu yenu, tukijua kwamba munafuata njia nzuri zaidi, ile ya wokovu wenu.

10Kwa maana Mungu ni mwenye haki. Yeye hatasahau kazi yenu na upendo mulioonyesha kwa ajili yake kwa namna mulivyowasaidia watu wake na munavyoendelea kuwasaidia.

11Lakini tunatamani sana kwamba kila mumoja kati yenu aendelee kuonyesha bidii ile mpaka mwisho, kusudi mambo yale munayotumainia yapate kutimizwa.

12Basi musigeuke kuwa wavivu, lakini mufuate mufano wa wale wanaoamini na kuvumilia. Kwa njia hiyo wanapokea yale Mungu aliyoahidi kuwapa.

Ahadi ya Mungu

13Wakati Mungu alipomupa Abrahamu ahadi, alifanya vilevile kiapo. Kwa sababu hakuna mutu mwingine mukubwa kuliko yeye kusudi ataje jina lake, akaapa kwa jina lake mwenyewe.

14Akasema: “Hakika nitakubariki sana na nitaongeza wazao wako.”

15Hivi kisha kungojea kwa uvumilivu, Abrahamu akapokea yale Mungu aliyomwahidi.

16Kwa maana watu wanapofanya kiapo, wanaapa kwa jina la mutu anayekuwa mukubwa kuliko wao wenyewe, nao uhakikisho wa kiapo kile unakomesha mabishano yote kati yao.

17Naye Mungu, kwa sababu alitaka kuonyesha wazi kwa wale watakaopokea ahadi kwamba yeye hawezi kubadilisha shauri lake hata kidogo, akaihakikisha kwa kiapo.

18Basi kuna mambo mawili, ahadi na kiapo, yasiyoweza kubadilika, na kuelekea hayo, Mungu hawezi kusema uongo. Kwa hivi, sisi tuliomukimbilia tunatiwa moyo sana na kushika kwa nguvu tumaini tulilowekewa.

19Tumaini hili linasimamisha imara na kulinda mioyo yetu kama vile nanga inavyosimamisha mashua imara. Nalo linapita katika pazia na kuingia katika Pahali Patakatifu Sana.

20Yesu alitangulia kuingia pahali pale kwa ajili yetu. Amekuwa Kuhani Mukubwa hata milele, kwa mufano wa Melkisedeki.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help