Ezra 6 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Amri ya Kiro inapatikana

1Mufalme Dario alitoa amri na uchunguzi ukafanywa katika muji wa Babeli katika nyumba ya kuwekea maandiko ya zamani ya kifalme.

2Lakini kitabu kikapatikana katika muji wa Akimeta katika jimbo la Media, nacho kilikuwa na maagizo haya:

3“Katika mwaka wa kwanza wa utawala wake, mufalme Kiro alitoa amri kwamba nyumba ya Mungu ijengwe upya katika Yerusalema, na ikuwe pahali pa kutolea sadaka na sadaka za kuteketezwa kwa moto. Urefu wake kwenda juu utakuwa metre makumi mbili na saba na upana wake metre makumi mbili na saba.

4Kuta zake zitajengwa kwa mustari mumoja wa miti juu ya kila mistari tatu ya mawe makubwa. Mali itakayotumiwa kwa kazi ile itatoka katika hazina ya mufalme.

5Vilevile, vyombo vyote vya zahabu na feza ambavyo mufalme Nebukadneza alivileta Babeli kutoka katika hekalu la Yerusalema, vitarudishwa na kuwekwa kila kimoja pahali pake katika nyumba ya Mungu.”

Dario anaamuru kazi iendelee

6Halafu Dario akatuma ujumbe huu:

Kwa Tatenayi, mutawala wa jimbo la upande wa magaribi wa muto Furati, Setari-Bozenayi na wakubwa wenzako katika jimbo.

Musiende kule kwenye hekalu,

7na muache kazi ya ujenzi wa nyumba hii ya Mungu iendelee. Muache mutawala wa Yuda na viongozi wa Wayuda waijenge nyumba ya Mungu pahali pake.

8Zaidi ya hayo, ninatoa amri kwamba ninyi mutawasaidia katika kazi hiyo. Mali zao zote walizotumia zitalipwa bila kuchelewa kutoka katika hazina ya mufalme inayotokana na kodi kutoka katika jimbo la upande wa magaribi wa muto Furati.

9Kila siku, tena bila kukosa, mutawapa makuhani wa Yerusalema kila kitu watakachohitaji; ikuwe ni ngombe dume, wana-ngombe, kondoo dume au wana-kondoo wa sadaka za kuteketezwa kwa moto kwa ajili ya Mungu wa mbinguni, au ngano, chumvi, divai au mafuta.

10Haya yote yatatendeka kusudi waweze kumutolea Mungu wa mbinguni sadaka zinazomupendeza na waombee maisha yangu mimi mufalme na watoto wangu.

11Ninaamuru vilevile kwamba mutu yeyote ambaye hatatii amri hii, muti mumoja uongolewe kutoka katika nyumba yake na atundikwe juu yake. Tena, nyumba yake ifanywe kuwa yalala.

12Mungu aliyeuchagua Yerusalema kuwa pahali pake pa kuabudiwa amwangushe mufalme au taifa lolote litakalopinga amri hii au kutaka kuiharibu nyumba hii ya Mungu inayokuwa katika Yerusalema.

Ni mimi Dario niliyetoa amri hii na inapaswa kushikwa.

Hekalu linatolewa kwa Mungu

13Basi, Tatenayi, mutawala wa jimbo la upande wa magaribi wa muto Furati, Setari-Bozenayi, na wakubwa wenzao, wakafanya bidii kwa kutimiza maagizo ya mufalme.

14Viongozi wa Wayuda waliendelea vizuri sana na kazi ya ujenzi wa hekalu, wakitiwa moyo na nabii Hagai na Zakaria mwana wa Ido. Wakamaliza ujenzi wa hekalu kama walivyoamriwa na Mungu wa Israeli, na kama walivyoagizwa na mufalme Kiro, mufalme Dario na mufalme Artasasta, wa Persia. Ang. Hag 1.1; Zak 1.1

15Ujenzi wa nyumba hiyo ukamalizika katika siku ya tatu ya mwezi wa Adari, katika mwaka wa sita wa utawala wa mufalme Dario.

16Basi, watu wa Israeli, makuhani, Walawi na watu wengine waliokuwa wamerudi kutoka katika uhamisho wakaizindua nyumba ya Mungu kwa shangwe kubwa.

17Wakati wa kuizindua nyumba ya Mungu, walitoa ngombe dume mia moja, kondoo dume mia mbili, wana-kondoo mia ine na beberu kumi na wawili kwa ajili ya sadaka ya kusamehewa zambi, mbuzi mumoja kwa kila kabila la Israeli.

18Vilevile, kwa ajili ya kazi ya Mungu katika Yerusalema, waliwapanga makuhani katika makundi yao ya Walawi katika zamu zao kufuatana na maagizo yaliyoandikiwa katika kitabu cha Musa.

19Katika siku ya kumi na ine ya mwezi wa kwanza, watu waliokuwa wamerudi kutoka katika uhamisho walisherehekea Pasaka.

20Makuhani na Walawi walikuwa wamejitakasa, wote walikuwa safi kabisa. Wakachinja mwana-kondoo wa Pasaka kwa ajili ya watu wote waliorudi kutoka katika uhamisho, wandugu zao makuhani na kwa ajili yao wenyewe.

21Waliokula mwana-kondoo wa Pasaka walikuwa Waisraeli wote waliorudi kutoka katika uhamisho pamoja na watu wengine wote ambao walikuwa wameziacha njia za mataifa mengine kwa kumwabudu Yawe, Mungu wa Israeli.

22Kwa muda wa siku saba watu walisherehekea kwa furaha sikukuu ya Mikate Isiyotiwa Chachu; kwa sababu Yawe aliwajalia furaha na kumupa mufalme wa Asuria moyo wa upendo kwao, akawasaidia katika kazi za ujenzi wa nyumba ya Mungu, wa Israeli.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help