1Hezekia alianza kutawala Yuda akiwa na umri wa miaka makumi mbili na mitano, akatawala kule Yerusalema kwa muda wa miaka makumi mbili na tisa. Mama yake aliitwa Abiya binti ya Zakaria.
2Alitenda kwa usawa mbele ya Yawe, kama vile babu yake Daudi alivyotenda.
3Katika mwezi wa kwanza wa mwaka wa kwanza wa utawala wake, mufalme Hezekia akafungua tena milango ya hekalu, akaitengeneza.
4Akawaingiza makuhani na Walawi, kisha akawakusanya katika kiwanja upande wa mashariki,
5akawaambia: “Munisikilize, enyi Walawi! Mujitakase na mutakase nyumba ya Yawe, Mungu wa babu zenu. Mutoshe uchafu wote unaokuwa katika Pahali Patakatifu.
6Kwa maana babu zetu waliasi na kutenda maovu mbele ya Yawe, Mungu wetu. Wamemwacha na kugeuzia mbali nyuso zao na makao ya Yawe.
7Tena, wamefunga milango ya baraza, wakazimisha taa, na hawajafukiza ubani wala kutoa sadaka za kuteketeza kwa moto katika Pahali Patakatifu pa Mungu wa Israeli.
8Kwa sababu hii, Yawe akakasirikia sana inchi ya Yuda na Yerusalema, na yale aliyowatendea yalikuwa ya kushangaza, ya kuogopesha na ya kuchekelewa. Haya yote mumeyaona wenyewe kwa macho yenu.
9Baba zetu waliuawa katika vita, na wana wetu na wabinti zetu na wake zetu ni wafungwa kwa sababu hii.
10Sasa, nimeamua ndani ya moyo wangu kufanya agano na Yawe, Mungu wa Israeli, kusudi asitukasirikie zaidi.
11Basi wana wangu, musikuwe wavivu. Yawe amewachagua ninyi kusudi mumutumikie, muwaongoze watu wake katika ibada, na kumufukizia ubani.”
12-14Walawi hawa wakaanza kazi:
wa ukoo wa Kohati: Mahati mwana wa Amasai na Yoeli mwana wa Azaria;
wa ukoo wa Merari: Kisi mwana wa Abudi na Azaria mwana wa Yehaleli;
wa ukoo wa Gersoni: Yoa mwana wa Zima, na Edeni mwana wa Yoa;
wa ukoo wa Elisafani: Simori na Yeneli;
wa ukoo wa Hemani: Zakaria na Matania;
wa ukoo wa Yedutuni: Semaya na Uzieli.
15Hawa wakawakusanya Walawi wenzao, wakajitakasa. Kisha wakaingia kama walivyotakiwa kufanya na mufalme, wakaanza kusafisha nyumba ya Yawe kama vile Yawe alivyoagiza.
16Makuhani wakaingia katika sehemu ya ndani ya nyumba ya Yawe, wakatosha uchafu wote uliokuwa mule, wakauweka katika kiwanja. Kutoka pale, Walawi walitwaa uchafu ule mpaka inje kwenye Bonde la Kidroni.
17Walianza kazi ya kutakasa hekalu siku ya kwanza ya mwezi wa kwanza, na kufikia siku ya nane, wakakuwa wamekwisha kumaliza kazi yote, hata na baraza. Kisha, wakafanya kazi kwa muda wa siku nane zaidi mpaka siku ya kumi na sita ya mwezi ule, kila kitu kikakamilika.
Hekalu linatakaswa tena18Kisha, Walawi wakamwendea mufalme Hezekia wakamwambia: “Tumekwisha kutakasa hekalu lote pamoja na mazabahu ya sadaka za kuteketeza kwa moto na vyombo vyake vyote, na meza ya mikate inayotolewa kwa Mungu na vyombo vyake vyote.
19Tena, tumerudisha na kutakasa vyombo vyote ambavyo mufalme Ahazi alivyotupa wakati wa utawala wake, pale alipoasi. Vyote vipo mbele ya mazabahu ya Yawe.”
20Bila kupoteza wakati, mufalme Hezekia akawakusanya wakubwa wa muji, akaenda nao katika nyumba ya Yawe.
21Wakaleta ngombe dume saba, kondoo dume saba, wana-kondoo saba na mbuzi dume saba, kuwa sadaka ya maondoleo ya zambi, kwa ajili ya jamaa ya kifalme, ya Pahali Patakatifu na ya watu wa Yuda. Kwa hiyo, mufalme akawaambia makuhani waliokuwa wazao wa Haruni wawateketeze juu ya mazabahu ya Yawe.
22Makuhani walichinja ngombe dume kwanza, kisha kondoo dume, halafu wana-kondoo na kila mara walitwaa damu ya nyama wale na kuinyunyiza juu ya mazabahu.
23Kisha, wakawaleta wale mbuzi dume wa sadaka ya maandoleo ya zambi karibu na mufalme na watu wote waliokuwa mule, nao wakaweka mikono yao juu ya mbuzi dume wale.
24Basi, wale makuhani wakawachinja, na kunyunyiza damu yao juu ya mazabahu kusudi ikuwe sadaka ya upatanisho kwa Waisraeli wote, kwa maana mufalme Hezekia alikuwa ameagiza sadaka ya kuteketeza kwa moto na sadaka ya maondoleo itolewe kwa ajili ya Waisraeli wote.
25Mufalme Hezekia alifuata maagizo ambayo Yawe alikuwa amemupa mufalme Daudi kwa njia ya Gadi, nabii wa mufalme na nabii Natani. Hivyo basi, akaweka Walawi katika nyumba ya Yawe, wamoja wao wakiwa na matoazi, wengine vinanda na wengine vinubi. Hiyo ilikuwa amri ya Yawe kwa njia ya manabii wake.
26Walawi walisimama na vyombo vya muziki vya Daudi, vilevile makuhani walisimama wakiwa na baragumu zao.
27Basi, Hezekia akaamuru sadaka ya kuteketeza kwa moto itolewe juu ya mazabahu. Mara tu sadaka hiyo ilipoanza kutolewa, watu wakaanza kumusifu Yawe kwa nyimbo zilizofuatana na mulio wa baragumu na vyombo vya muziki vya Daudi, mufalme wa Israeli.
28Watu wote waliokuwa mule wakashiriki katika ibada. Waimbaji wakaendelea na kuimba, na baragumu zikaendelea kupigwa mpaka wakati shuguli za utoaji wa sadaka hiyo ya kuteketeza kwa moto ilipokamilika.
29Kisha, mufalme Hezekia pamoja na watu wote waliokuwa pale wakainama, kwa kumwabudu Yawe.
30Kisha mufalme Hezekia na viongozi wakawaambia Walawi wamusifu Yawe kwa nyimbo ambazo mufalme Daudi na nabii Asafu walizotunga. Basi, watu wote wakamutukuza Mungu kwa furaha, na kuinama uso mpaka chini.
31Halafu Hezekia akawaambia watu: “Sasa mumekwisha kujitakasa, mukaribie, mulete sadaka na matoleo ya shukrani katika nyumba ya Yawe.” Basi, watu wakaleta sadaka zao na matoleo yao ya shukrani, na za kuteketeza.
32Sadaka za kuteketeza walizoleta kwa jumla zilikuwa ngombe dume makumi saba, kondoo dume mia moja na wana-kondoo mia mbili. Zote hizo zilikuwa sadaka za kuteketeza kwa ajili ya Yawe.
33Matoleo matakatifu yalikuwa ngombe dume mia sita na kondoo elfu tatu.
34Kwa vile ambavyo hesabu ya makuhani ilikuwa ndogo, hawakuweza kuchuna nyama wale wote. Kwa hiyo, wandugu zao Walawi wakawasaidia mpaka walipomaliza kazi hiyo. Wakati ule, makuhani wengine zaidi walikuwa wamekwisha kujitakasa. (Walawi walijiweka katika hali ya usafi zaidi kuliko makuhani.)
35Mbali na wingi wa sadaka za kuteketeza, kulikuwa vilevile mafuta ya sadaka ya amani, hata kulikuwa sadaka ya kinywaji kwa ajili ya kila sadaka za kuteketeza. Hivyo basi, kazi za ibada zikaanzishwa tena katika hekalu.
36Mufalme Hezekia na watu wote wakajazwa na furaha tele kwa sababu ya yote Mungu aliyowatendea watu; maana tukio hili lilitokea kwa rafla.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.