1Yawe akamwambia Musa: “Kwenda kwa mufalme wa Misri. Mimi nimefanya moyo wake kuwa mugumu na wa wakubwa wake kusudi nipate kuonyesha vitambulisho hivi kati yao,
2na ninyi mupate kuwaelezea watoto wenu na wajukuu wenu jinsi nilivyowachekelea Wamisri kwa kuonyesha vitambulisho vile kati yao. Hivyo mutatambua kwamba mimi ni Yawe.”
3Basi, Musa na Haruni wakamwendea mufalme wa Misri na kumwambia: “Yawe, Mungu wa Waebrania, anasema hivi: ‘Mpaka wakati gani utakataa kujinyenyekeza mbele yangu? Uwaache watu wangu waondoke kusudi wanitumikie.
4Ukikataa kuwaacha watu wangu waondoke, basi, kesho nitaleta nzige washambulie inchi yako.
5Inchi yote ya Misri itakuwa giza kwa sababu ya nzige wale. Watakula kila kitu kilichobaki nyuma ya ile mvua ya mawe. Vilevile hawataacha chochote juu ya miti inayoota katika mashamba.
6Nzige wale watajaa katika nyumba zako, nyumba za wakubwa wako na za Wamisri wote. Watakuwa wengi kiasi ambacho hata wazee wenu hawajapata kuona tangu walipozaliwa, mpaka leo.’ ” Basi, Musa akatoka kwa mufalme wa Misri.
7Viongozi wa mufalme wakamwuliza: “Mutu huyu atatusumbua mpaka wakati gani? Uwaache watu hawa wajiendee wamutumikie Yawe, Mungu wao. Haujali kwamba inchi ya Misri inaangamia?”
8Hapo, Musa na Haruni wakaitwa warudi kwa mufalme wa Misri, naye akawaambia: “Muende mumutumikie Yawe, Mungu wenu. Lakini, ninauliza, ni nani watakaokwenda pamoja nanyi?”
9Musa akamujibu: “Kila mutu, vijana na wazee, tutaondoka na watoto wetu wanaume na wanawake, kondoo na mbuzi wetu na ngombe. Kwa maana tunapaswa kumufanyia Yawe sikukuu.”
10Mufalme wa Misri akawaambia: “Basi, Yawe akuwe pamoja nanyi kama nitawaruhusu mujiendee na watoto wenu. Ni wazi kwamba muko na nia mbaya ndani ya moyo wenu.
11Haitakuwa vile! Ni wanaume tu watakaokwenda kumutumikia Yawe, maana hilo ndilo munalotaka.” Halafu Musa na Haruni wakafukuzwa toka mbele ya mufalme.
12Yawe akamwambia Musa: “Nyoosha mukono wako juu ya inchi ya Misri, nzige watokee kusudi waingie na kula mimea yote katika inchi na vyote vilivyoachwa na ile mvua ya mawe.”
13Basi, Musa akainua fimbo yake juu ya inchi ya Misri. Yawe akaleta upepo toka upande wa mashariki, ukavuma juu ya inchi muchana kutwa na usiku kucha. Kulipokucha, ule upepo ukaleta nzige.
14Wale nzige wakaenea kila pahali katika inchi ya Misri, wakatua juu ya inchi yote. Nzige wale walikuwa kundi kubwa sana, kiasi ambacho hakijapata kutokea wala hakitatokea tena. Ang. Ufu 9.2-3
15Walifunika inchi yote ya Misri, hata inchi ikaonekana kuwa giza. Walikula mimea yote na matunda yote yaliyobaki wakati wa ile mvua ya mawe. Hakuna hata jani moja lililobakia katika inchi. Hakuna jani lolote lililobakia juu ya miti wala mimea popote katika inchi yote ya Misri.
16Hapo mufalme wa Misri akaita Musa na Haruni kwa haraka, akawaambia: “Nimetenda zambi mbele ya Yawe, Mungu wenu, na mbele yenu.
17Kwa hiyo sasa ninawasihi munisamehe zambi yangu mara hii, muniombee kwa Yawe, Mungu wenu, aniondolee kifo hiki.”
18Basi, Musa akaondoka kwa mufalme, akaenda kumwomba Yawe.
19Naye Yawe akaleta upepo mukali toka upande wa magaribi, ukawainua wale nzige na kuwasukumia kwenye bahari Nyekundu. Hakuna hata nzige mumoja aliyebaki katika inchi nzima ya Misri.
20Lakini Yawe akafanya moyo wa mufalme kuwa mugumu, naye hakuwaachilia Waisraeli waondoke.
Pigo la tisa: Giza21Yawe akamwambia Musa: “Nyoosha mukono wako juu mbinguni kusudi giza nzito litokee katika inchi ya Misri, giza nzito sana ambalo mutu ataweza kulipapasa.”
22Basi, Musa akanyoosha mukono wake juu mbinguni, kukakuwa giza nzito katika inchi yote ya Misri kwa muda wa siku tatu. Ang. Zab 105.28; Ufu 16.10
23Watu hawakuweza kuonana wala kuondoka pahali walipokuwa kwa muda ule wa siku tatu. Lakini Waisraeli wote walikuwa na mwangaza kule Goseni walikokuwa wanakaa.
24Kisha, mufalme wa Misri akamwita Musa, akamwambia: “Mwende mumutumikie Yawe. Watoto wenu vilevile wanaweza kwenda pamoja nanyi. Lakini kondoo na mbuzi, na ngombe wenu wabaki.”
25Lakini Musa akamwambia: “Unapaswa kuturuhusu kutwaa nyama wa matoleo na sadaka za kuteketezwa kwa kumutolea Yawe, Mungu wetu.
26Ngombe wetu tunapaswa vilevile kuwapeleka wala hakuna hata nyama mumoja atakayebaki nyuma. Kwa sababu kutoka katika mifugo yetu wenyewe, tutamutumikia Yawe, Mungu wetu, wala sisi hatujui ni nyama gani tutakayemutolea Yawe sadaka mpaka tutakapofika kule.”
27Lakini Yawe akaufanya moyo wa mufalme wa Misri kuwa mugumu, akakataa kuwaachilia Waisraeli waondoke.
28Mufalme akamwambia Musa: “Toka mbele yangu! Ufanye angalisho sana! Usikuje kuniona tena, maana siku utakapokuja tena mbele yangu, utakufa!”
29Musa naye akamwambia: “Sawa! Kama vile ulivyosema sitakuja kukuona tena.”
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.