Yoshua 4 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Mawe ya ukumbusho kumi na mawili

1Taifa zima lilipokwisha kuvuka muto Yordani, Yawe akamwambia Yoshua:

2“Chagua watu kumi na wawili kati ya hao Waisraeli, ni kusema mutu mumoja kutoka kila kabila,

3uwaagize hivi: ‘Mutwae mawe kumi na mawili kutoka hapa katikati ya muto Yordani, kutoka hapa miguu ya makuhani ilipokuwa, mutwae mawe hayo, muyaweke pahali pale ambapo mutalala leo hii.’ ”

4Yoshua akawaita hao watu kumi na wawili ambao alikuwa amewachagua kati ya Waisraeli, kila kabila mutu mumoja,

5akawaambia: “Mulitangulie Sanduku la Agano la Yawe, Mungu wenu, mpaka katikati ya muto Yordani. Kila mumoja wenu abebe jiwe kwenye bega lake, jiwe moja kwa ajili ya kila kabila la Israeli.

6Jambo hilo litakuwa kitambulisho kati yenu; na watoto wenu watakapowauliza kwa siku zinazokuja: ‘Mawe haya yana maana gani kwenu?’

7Ninyi mutawaambia: ‘Sanduku la Agano la Yawe lilipopitishwa katika muto Yordani, maji ya muto huo yalizuiliwa yasitiririke!’ Kwa hiyo mawe haya yatakuwa ukumbusho kwa Waisraeli milele.”

8Wale wanaume wakafanya kama vile walivyoamriwa na Yoshua, wakatwaa mawe kumi na mawili kutoka katikati ya muto Yordani, jiwe moja kwa ajili ya kila kabila la Israeli, kama Yawe alivyomwambia Yoshua, wakaenda nayo mpaka pahali pale walipolala, wakayaweka kule.

9Yoshua akasimika vilevile mawe kumi na mawili katikati ya muto Yordani, pahali pale miguu ya makuhani waliobeba lile Sanduku la Agano iliposimama. Mawe hayo yako kule mpaka hivi leo.

10Wale makuhani waliobeba Sanduku la Agano, walisimama katikati ya muto Yordani mpaka watu walipomaliza kutimiza kila kitu ambacho Yawe alimwamuru Yoshua awaambie watu; Yoshua alifanya yote ambayo Musa alikuwa amemwamuru. Watu wakaharakisha kuvuka muto,

11na watu wote walipokwisha kuvuka, wale makuhani wakawatangulia na lile Sanduku la Agano la Yawe.

12Wanaume wa kabila la Rubeni na la Gadi na nusu ya kabila la Manase waliwatangulia Waisraeli wakiwa na silaha zao, kama vile walivyoagizwa na Musa.

13Watu yapata elfu makumi ine wakiwa na silaha tayari kwa vita walipita mbele ya Yawe wakielekea bonde la muji wa Yeriko.

14Katika siku hiyo Yawe akamutukuza Yoshua mbele ya Waisraeli wote, nao wakamuheshimu Yoshua maisha yake yote kama walivyomuheshimu Musa katika maisha yake.

15Kisha Yawe akamwambia Yoshua:

16“Uamuru makuhani wanaobeba sanduku la agano, watoke katika muto Yordani.”

17Basi, Yoshua akawaamuru wale makuhani: “Mutoke katika muto Yordani.”

18Hao makuhani waliokuwa wanabeba lile Sanduku la Agano la Yawe walipotoka katikati ya muto Yordani, na kukanyaga ukingo wa muto, maji ya muto Yordani yakaanza kutiririka tena, na kufurika kama mbele.

19Waisraeli walivuka muto Yordani katika siku ya kumi ya mwezi wa kwanza, wakapiga kambi kule katika muji wa Gilgali, upande wa mashariki wa Yeriko.

20Yoshua akayasimika yale mawe kumi na mawili ambayo waliyatwaa kutoka muto Yordani, kule Gilgali.

21Kisha Yoshua akawaambia Waisraeli: “Watoto wenu watakapowauliza kwa siku zinazokuja: ‘Mawe haya yana maana gani?’

22Mutawaambia hivi: ‘Taifa la Israeli lilivuka muto huu wa Yordani pahali pakavu.’

23Mutawaambia kwamba Yawe, Mungu wenu, aliyakausha maji ya muto Yordani kwa ajili yenu mpaka mukavuka, kama vile alivyofanya kwa bahari Nyekundu. Akaikausha mbele yetu mpaka tulipovuka

24kusudi watu wote wa dunia wajue kwamba mukono wa Yawe una nguvu; nanyi mupate kumwogopa Yawe, Mungu wenu, milele.”

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help