1Asa akatenda mambo yanayokuwa mazuri na sawa mbele ya Yawe, Mungu wake.
2Aliondoa katika inchi mazabahu za kigeni na pahali pa kuabudia miungu mingine, akabomoa minara na kukatakata sanamu za Ashera.
3Aliwaamuru watu wa Yuda wamutafute Yawe, Mungu wa babu zao, na kutii Sheria na amri.
4Vilevile aliondoa pahali pote pa kuabudia miungu mingine na meza za kufukizia ubani kutoka katika miji yote ya Yuda; halafu ufalme wake ulikuwa na amani chini ya utawala wake.
5Alijenga miji yenye kuta za kuiimarisha inchi ya Yuda wakati ule wa amani, na kwa muda wa miaka ile, hapakutokea vita kwa maana Yawe alimupa amani.
6Naye Asa akawaambia watu wa Yuda: “Tujenge miji hii na kuizungushia kuta na minara, milango yenye vifungio vya vyuma. Inchi ingali katika mikono yetu kwa maana tumetenda mapenzi ya Yawe, Mungu wetu, naye ametupatia amani pande zote.” Basi wakajenga na kufanikiwa.
7Mufalme Asa alikuwa na jeshi la waaskari elfu mia tatu kutoka Yuda, wenye ngao na mikuki, na wengine elfu mia mbili na makumi nane kutoka katika kabila la Benjamina, wenye ngao na pinde. Wote walikuwa watu mashujaa sana.
8Zera, Mwetiopia alishambulia inchi ya Yuda akiwa na jeshi la waaskari milioni moja na magari mia tatu, akasonga mbele mpaka Maresa.
9Asa alitoka akaenda kupigana naye. Pande zote mbili zilijipanga katika Bonde la Sefata karibu na Maresa.
10Hapo Asa akamulilia Yawe, Mungu wake, akisema: “Ee Yawe, hakuna mwingine kama wewe, mwenye uwezo wa kusaidia jeshi likuwe zaifu au lenye nguvu. Utusaidie, ee Yawe, Mungu wetu, kwa sababu sisi tunakutegemea wewe, na kwa jina lako tumekuja kupigana vita na jeshi hili kubwa ajabu. Ee Yawe, wewe ndiwe Mungu wetu; usimuruhusu mwanadamu yeyote ashindane nawe.”
11Yawe akawashinda Waetiopia mbele ya Asa na jeshi lake la watu wa Yuda. Waetiopia wakakimbia.
12Asa pamoja na waaskari wake wakawafuatilia mpaka Gerari, wakawaua Waetiopia wengi sana, hapakubaki hata mumoja, maana walikuwa wamekwisha kushindwa na Yawe pamoja na jeshi lake. Jeshi la Yuda likateka vitu vingi sana.
13Likaharibu miji yote iliyokuwa kandokando ya Gerari, kwa kuwa watu waliokuwa katika miji ile, walipatwa na hofu ya Yawe. Likabeba mali nyingi kutoka katika miji ile, kwa sababu kulikuwa mali mengi sana.
14Likashambulia vilevile wachungaji, likachukua kondoo wengi na ngamia. Kisha likarudia Yerusalema.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.