2 Wafalme 5 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Namani anaponyeshwa

1Namani, jemadari wa waaskari wa mufalme wa Aramu, alikuwa mutu mukubwa aliyeheshimiwa sana na bwana wake, maana kwa njia yake Yawe aliiletea inchi ya Waaramu ushindi. Alikuwa askari hodari, lakini alikuwa na ugonjwa wa ukoma.

2Katika vita walivyokuwa wakipigana na Waisraeli, Waaramu walikuwa wamemukamata binti mumoja mudogo kutoka Israeli kuwa mufungwa, naye akakuwa anamutumikia muke wa Namani.

3Siku moja akamwambia bibi yake, muke wa Namani: “Ingekuwa heri bwana wangu angekwenda na kumwona yule nabii anayekuwa Samaria! Angemuponyesha ugonjwa wake.”

4Namani alipopata habari hii, akaenda kwa mufalme na kumwelezea habari za mutoto yule.

5Mufalme wa Aramu akamwambia: “Twaa barua hii umupelekee mufalme wa Israeli.”

Hivyo Namani akaondoka, akipeleka vikoroti elfu makumi tatu vya feza, vikoroti elfu sita vya zahabu na nguo kumi za sikukuu.

6Barua yenyewe iliandikwa hivi:

“Ninakutumia jemadari wangu Namani pamoja na barua hii, kusudi upate kumuponyesha ugonjwa wake.”

7Mufalme wa Israeli aliposoma barua hii alipasua nguo yake na kusema: “Sababu gani mufalme wa Aramu anataka nimuponyeshe mutu huyu ukoma wake? Anafikiri kwamba mimi ni Mungu anayekuwa na uwezo wa kuua au kufufua? Mufahamu basi, muone kwamba mutu huyu anataka kuniletea ugomvi!”

8Elisha, nabii wa Mungu, alipopata habari kwamba mufalme wa Israeli amepasua nguo zake, alituma ujumbe kwa mufalme, akamwuliza: “Kwa sababu gani umepasua nguo zako? Umutume mutu huyo kwangu, kusudi apate kujua kwamba kuna nabii katika Israeli!”

9Namani akaenda na farasi wake na gari lake mpaka kwenye mulango wa Elisha.

10Elisha akamutuma mutumishi wake amwambie: “Kwenda uoge mara saba katika muto Yordani, nawe utapona kabisa.”

11Lakini Namani alikasirika sana, akaenda zake akisema: “Nilizani kwamba hakika atanifikia na kumwomba Yawe, Mungu wake, apitishe mikono yake juu ya pahali ninapogonjwa na kuniponyesha!

12Zaidi ya ile, mito Abana na Farpari ya kule Damasiki si bora kuliko mito yote ya Israeli? Nisingeweza kuoga mule na kupona?” Akaondoka na kurudi kwake, naye alikasirika sana.

13Watumishi wake wakamwendea na kumwambia: “Baba yetu, kama nabii angekuambia ufanye jambo fulani gumu, haungelifanya? Sasa, aliyokuambia tu ni: ‘Ujioshe, kusudi upone!’ ”

14Basi, Namani akateremuka kwenye muto Yordani akajitumbukiza mule mara saba, kama alivyoagizwa na Elisha mutu wa Mungu, naye akapona kabisa. Ngozi yake ikakuwa laini na yenye afya kama ya mutoto mudogo.

15Halafu akarudi kwa mutu wa Mungu pamoja na watu wake, akasema: “Sasa ninajua kwamba hakuna Mungu yeyote katika dunia lakini tu Mungu wa Israeli; kwa hiyo, tafazali sasa upokee zawadi ya mutumishi wako.”

16Elisha akamujibu: “Kama vile Yawe, yule ambaye mimi ninamutumikia, anavyoishi, sitapokea zawadi yoyote.”

Namani akamusihi, lakini Elisha akakataa kabisa.

17Namani akasema: “Ikiwa hautapokea zawadi zangu, basi tafazali umupatie mutumishi wako udongo unaoweza kubebwa na nyumbu wawili, maana tokea leo mimi mutumishi wako sitatoa sadaka za kuteketezwa wala sadaka kwa miungu mingine lakini tu kwa Yawe.

18Naye Yawe anisamehe ninapofuatana na mufalme wangu kwenda kuabudu katika hekalu la Rimoni mungu wa Waaramu. Ninapaswa kuinama pamoja naye kwa sababu anaegemea kwenye mukono wangu. Ninaomba Yawe anisamehe!”

19Elisha akamwambia: “Kwenda kwa amani.” Namani akaenda zake.

Alipokuwa bado hajafika mbali,

20Gehazi, mutumishi wa Elisha mutu wa Mungu, akasema: “Bwana wangu amemwachilia Namani wa Aramu aende bila kupokea chochote alicholeta. Kama vile Yawe anavyoishi, nitamufuata kusudi nipate kitu kutoka kwake.”

21Hapo akaondoka na kumufuata Namani. Namani alipoangalia na kuona mutu anamufuata mbio, akashuka ndani ya gari lake, akaenda kukutana naye. Basi, akamwuliza: “Kuna usalama?”

22Gehazi akajibu: “Mambo yote ni sawa lakini tu bwana wangu amenituma nikuambie kwamba sasa hivi amepokea watu wawili wa kundi la manabii katika inchi ya milima ya Efuraimu, naye angependa uwape vikoroti elfu tatu vya feza na nguo mbili ya sikukuu.”

23Namani akasema: “Tafazali twaa vikoroti elfu sita vya feza.” Akamusihi, kisha akamufungia mafungu mawili na kumupa nguo mbili ya sikukuu, akawapa watumishi wake wawili na kuwaagiza wafuatane na Gehazi.

24Walipofika juu ya mulima pahali Elisha alipoishi, Gehazi akatwaa mafungu ya feza kutoka kwa watumishi wa Namani na kuyapeleka ndani ya nyumba yake. Kisha akawaruhusu wale watumishi waende zao, nao wakaondoka.

25Halafu Gehazi akaingia kwa Elisha na kuanza kumutumikia. Elisha akamwuliza: “Unatoka wapi?”

Gehazi akajibu: “Sikuenda nafasi yoyote.”

26Lakini Elisha akamwambia: “Unafikiri roho yangu haikukuwa pamoja nawe wakati mutu yule alipotoka ndani ya gari lake na kuja kukutana nawe? Huu ndio wakati wa kupokea feza na nguo, mashamba ya mizeituni na mizabibu, kondoo na ngombe au watumishi na wajakazi?

27Kwa hiyo ukoma wa Namani utakushika wewe, na wazao wako milele.”

Basi, Gehazi aliondoka akiwa ameshikwa na ukoma, na ngozi yake ilikuwa nyeupe kama teluji.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help