Hesabu 7 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Matoleo ya viongozi

1Siku Musa alipomaliza kusimamisha hema takatifu, akalimiminia mafuta na kulitakasa pamoja na vyombo vyake vyote. Akamiminia mazabahu mafuta na kuitakasa pamoja na vyombo vyake vyote.

2Viongozi wa Israeli na wakubwa wa ukoo na viongozi wa makabila ambao walisimamia watu wale waliohesabiwa,

3wakamuletea Yawe matoleo yao: magari sita yaliyofunikwa na ngombe dume kumi na wawili, gari moja kwa kila viongozi wawili na ngombe dume mumoja kwa kila kiongozi. Kisha kuvitoa mbele ya hema takatifu,

4Yawe akamwambia Musa:

5Pokea matoleo haya kusudi yatumiwe katika kazi itakayofanywa kwa ajili ya hema la mukutano, uwape Walawi, kila mumoja kwa kadiri ya kazi yake.

6Basi, Musa akatwaa magari na ngombe dume akawapa Walawi.

7Wagersoni wakapewa magari mawili na ngombe dume wane, kwa kadiri ya kazi yao,

8na Wamerari wakapewa magari mane na ngombe dume wanane kwa kuwasaidia katika kazi zao zote chini ya uongozi wa Itamari mwana wa kuhani Haruni.

9Lakini Musa hakuwapa Wakohati kitu chochote kwa sababu wao walikuwa na utumishi wa kutunza vitu vitakatifu ambavyo vilipaswa kubebwa juu ya mabega.

10Viongozi hao wakatoa sadaka kwa ajili ya kuitakasa mazabahu siku ile ilipopakwa mafuta; walitoa sadaka zao mbele ya mazabahu.

11Yawe akamwambia Musa: Kila siku kiongozi mumoja atatoa sadaka yake kwa ajili ya kutakasa mazabahu.

12-83Wale waliotoa sadaka ni hawa:

Siku ya kwanza: Nasoni mwana wa Aminadabu, wa kabila la Yuda;

Siku ya pili: Netaneli mwana wa Suari, wa kabila la Isakari;

Siku ya tatu: Eliabu mwana wa Heloni, wa kabila la Zebuluni;

Siku ya ine: Elisuri mwana wa Sedeuri, wa kabila la Rubeni:

Siku ya tano: Selumieli mwana wa Suri-Shadai, wa kabila la Simeoni;

Siku ya sita: Eliasafu mwana wa Deueli, wa kabila la Gadi;

Siku ya saba: Elisama mwana wa Amihudi, wa kabila la Efuraimu;

Siku ya nane: Gamalieli mwana wa Pedasuri, wa kabila la Manase;

Siku ya tisa: Abidani mwana wa Gideoni, wa kabila la Benjamina;

Siku ya kumi: Ahiezeri mwana wa Amishadai, wa kabila la Dani;

Siku ya kumi na moja: Pagieli mwana wa Okrani, wa kabila la Aseri;

Siku ya kumi na mbili: Ahira mwana wa Enani, wa kabila la Nafutali.

Hii ni sadaka iliyotolewa na kila mumoja:

sahani moja ya feza yenye uzito wa kilo moja na nusu na beseni moja la feza lenye uzito wa grama mia nane kulingana na vipimo vya hema takatifu; sahani na beseni hilo vikiwa vimejazwa unga laini uliochanganywa na mafuta kwa ajili ya sadaka ya vyakula;

kisahani kimoja cha zahabu chenye uzito wa grama mia moja na kumi kikiwa kimejazwa ubani;

mwana-ngombe dume mumoja, kondoo dume mumoja, na mwana-kondoo dume mumoja wa mwaka mumoja, kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa;

beberu mumoja kwa ajili ya sadaka ya zambi;

ngombe dume wawili, kondoo dume watano, beberu watano na wana-kondoo dume watano wa mwaka mumoja kwa ajili ya sadaka za amani.

84Jumla ya matoleo ya sadaka za viongozi wa Israeli kwa ajili ya mazabahu siku ilipotakaswa ilikuwa: sahani za feza kumi na mbili, beseni za feza kumi na mbili, na visahani vya zahabu kumi na viwili.

85Kila sahani ya feza, ilikuwa yenye uzito wa kilo moja na nusu na kila kisahani kilikuwa chenye uzito wa grama mia nane. Hivyo vyombo vyote vilikuwa na uzito wa kilo makumi mbili na saba na grama mia sita kadiri ya vipimo vya hema takatifu.

86Vile visahani vya zahabu kumi na viwili vyenye kujaa ubani, kila kimoja kikiwa na uzito wa grama mia moja na kumi kadiri ya vipimo vya hema takatifu vilikuwa na jumla ya uzito wa kilo moja na grama mia tatu makumi mbili.

87Jumla ya nyama wote wa sadaka ya kuteketezwa ilikuwa ngombe dume kumi na wawili, kondoo dume kumi na wawili, na wana-kondoo dume wa mwaka mumoja kumi na wawili, pamoja na sadaka ya vyakula na beberu kumi na wawili kwa ajili ya sadaka ya zambi,

88na kwa ajili ya sadaka ya amani, jumla ya nyama waliotolewa ilikuwa ngombe dume makumi mbili na wane, kondoo dume makumi sita, beberu makumi sita, na wana-kondoo dume wa mwaka mumoja makumi sita. Hiyo ndiyo iliyokuwa sadaka iliyotolewa kwa ajili ya mazabahu, kisha mazabahu hayo kupakwa mafuta.

89Wakati Musa alipoingia ndani ya hema la mukutano kwa kuongea na Yawe, akasikia sauti kutoka upande wa juu wa kiti cha rehema, kilichokuwa juu ya Sanduku la Agano, kutoka kati ya wale makerubi.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help