2 Samweli 17 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Husayi anamupotosha Abusaloma

1Zaidi ya hayo, Ahitofeli alimwambia Abusaloma: “Uniruhusu nichague watu elfu kumi na mbili, niondoke na kumufuatia Daudi leo usiku.

2Nitamushambulia akiwa amechoka na amevunjika moyo, nami nitamutia hofu kubwa. Watu wote wanaokuwa pamoja naye watakimbia. Nitamwua mufalme peke yake,

3na kuwarudisha watu wengine wote kwako kama bibi arusi anavyorudi katika nyumba ya mume wake. Wewe unayatafuta maisha ya mutu mumoja tu na watu wengine watakuwa na amani.”

4Shauri hilo la Ahitofeli lilimupendeza Abusaloma na wazee wote wa Israeli.

5Kisha, Abusaloma akasema: “Mumwite Husayi vilevile, yule mutu wa inchi ya Arki, tusikie neno analotaka kusema.”

6Husayi alipofika kwa Abusaloma, Abusaloma alimwuliza: “Hivyo ndivyo Ahitofeli alivyosema. Tufanye kama vile alivyotushauria? Kama sivyo, basi, utuambie shauri lako.”

7Husayi akamwambia Abusaloma: “Wakati huu, shauri Ahitofeli alilolitoa si jema.”

8Zaidi ya hayo, Husayi akamwambia: “Wewe unajua kwamba baba yako na watu wake ni mashujaa na kwamba wamekasirikishwa kama dubu dike aliyenyanganywa watoto wake katika mbuga. Zaidi ya hayo, unajua kwamba baba yako ni bingwa wa vita. Yeye hatakaa usiku kucha pamoja na watu wake.

9Hata sasa amekwisha kujificha katika pango moja au nafasi ingine. Ikiwa tu katika mashambulizi ya mwanzo kunakufa watu kati yetu, habari itasambaa kwamba wafuasi wa Abusaloma wameshindwa vibaya.

10Watu wako watakaposikia hivyo, hata wale ambao ni hodari, wenye mioyo kama ya simba, watavunjika kabisa moyo kwa woga. Maana, Waisraeli wote wanajua kwamba baba yako ni shujaa na wote wanaokuwa pamoja naye ni watu hodari.

11Shauri langu ni kwamba uwakusanye kwako watu wote wa Israeli tangia Dani mpaka Beri-Seba wakuwe wengi kama muchanga wa bahari, na wewe mwenyewe peke yako uende kwa vita.

12Nasi tutamwendea Daudi pahali popote anapoweza kupatikana na tutamwangukia sawa vile umande unavyoanguka juu ya udongo. Basi, hakuna atakayebakia hata kama ni yeye mwenyewe au watu wake wote wanaokuwa pamoja naye.

13Ikiwa atakimbilia katika muji fulani, basi, watu wote wa Israeli wataleta kamba na kukokotea mawe ya majengo yake mpaka katika bonde, na hakutabaki kitu chochote hata jiwe dogo la muji ule.”

14Abusaloma pamoja na watu wote wa Israeli wakasema: “Shauri la Husayi ni bora kuliko shauri la Ahitofeli.” Wakakataa shauri la Ahitofeli kwa sababu Yawe alikuwa amepanga kulishinda shauri jema la Ahitofeli kusudi aweze kumuletea Abusaloma hasara.

Daudi anaonywa na kutoroka

15Kisha Husayi akawaambia makuhani Zadoki na Abiatari jinsi Ahitofeli na yeye mwenyewe walivyomushauria Abusaloma na wazee wa Israeli.

16Kisha akasema, “Mupelekee Daudi habari upesi kwamba asilale usiku kwenye vivuko katika jangwa, lakini lazima avuke muto Yordani kusudi asikamatwe na kuuawa, yeye pamoja na watu wake wote.”

17Wakati ule, Yonatani na Ahimasi walikuwa wakimungojea karibu na Eni-Rogeli, kusudi wasionekane na mutu yeyote wakiingia katika muji. Kila mara mujakazi fulani alikuwa akiwapelekea habari nao wakaipeleka kwa mufalme Daudi.

18Lakini wakati huu, walionekana na kijana mumoja ambaye alikwenda na kumupasha Abusaloma habari. Kwa hiyo, Yonatani na Ahimasi waliondoka haraka, wakaenda Bahurimu katika nyumba ya mutu fulani aliyekuwa na kisima katika kiwanja chake. Wakaingia ndani ya kisima na kujificha.

19Mwanamuke mwenye nyumba hiyo akatwaa kifuniko na kukifunika kisima hicho, halafu akaanika ngano juu ya kifuniko. Habari hizo hazikujulikana.

20Watumishi wa Abusaloma walipofika kwa yule mwanamuke, wakamwambia: “Ahimasi na Yonatani wako wapi?”

Yule mwanamuke akawaambia: “Wamekwenda ngambo ya kijito.”

Walipowatafuta na kuwakosa, wakarudi Yerusalema.

21Nyuma ya watumishi wa Abusaloma kuondoka, Yonatani na Ahimasi walitoka ndani ya kisima, wakaenda kwa mufalme Daudi na kumupasha habari. Wakamwambia: “Ondoka, uende ngambo ya muto, kwa sababu Ahitofeli amemushauria Abusaloma juu yako.”

22Kwa hiyo, Daudi akaondoka na watu wote waliokuwa pamoja naye, wakavuka muto Yordani. Ilipofika asubui hakuna mutu aliyebaki nyuma bila kuvuka muto Yordani.

Ahitofeli anajitundika

23Ahitofeli alipoona kwamba shauri lake halikufuatwa, alitandika punda wake, akaenda kwake, kwenye muji wake. Alipofika kule, alipanga vizuri mambo ya nyumba yake, akajitundika. Akakufa na kuzikwa kwenye kaburi la baba yake.

24Basi, Daudi akaenda Mahanaimu. Abusaloma akavuka muto Yordani na watu wote wa Israeli.

25Wakati ule, Abusaloma alikuwa amemuweka Amasa kuwa jemadari wa waaskari pahali pa Yoabu. Amasa alikuwa mwana wa Itira, Mwisimaeli. Mama yake aliitwa Abigaili binti wa Nahasi, aliyekuwa dada ya Zeruya mama ya Yoabu.

26Abusaloma pamoja na watu wa Israeli walipiga kambi yao katika inchi ya Gileadi.

27-29Daudi alipofika Mahanaimu, alikutwa na Sobi mwana wa Nahasi wa muji wa Raba katika inchi ya Amoni, Makiri mwana wa Amieli wa muji wa Lodebari, pamoja na Barzilayi wa muji wa Rogelimu katika inchi ya Gileadi. Hawa watu waliona kwamba Daudi na watu wake walikuwa na njaa, walikuwa wanachoka na walikuwa na kiu kwa sababu ya kusafiri katika jangwa. Basi, waliwapelekea vitanda, mabeseni, vyombo vya udongo, ngano, shayiri, unga, mihindi yenye kukaangwa, kunde na manjegere, asali, siagi, kondoo na maziwa kutoka nyama wao wa kufugwa.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help