1Barua hii inatoka kwangu mimi Yuda, mutumishi wa Yesu Kristo na ndugu wa Yakobo.
Ninawaandikia ninyi mulioitwa na Mungu Baba na munaoishi katika upendo wake na kulindwa kwa ajili ya Yesu Kristo.
2Ninawatakia huruma, amani na upendo kwa uwingi.
Walimu wa uongo(2 Pet 2.1-17)3Wapendwa wangu, wakati nilipokuwa nikifanya bidii sana ya kuwaandikia juu ya wokovu tunaoshiriki wote pamoja, nikaona sherti niwaandikie na kuwaonya mupate kutetea imani ile Mungu aliyotoa mara moja tu kwa watu wake.
4Maana kuna watu wasiomuheshimu Mungu waliojiingiza kwa siri kati yetu. Watu hawa wanapotosha ujumbe wa neema ya Mungu wetu kusudi wapate kufanya uasherati na kumukana Yesu Kristo, anayekuwa peke yake Kiongozi na Bwana wetu. Tangia zamani Maandiko Matakatifu yamejulisha hukumu ile itakayowapata watu hawa.
5Ijapokuwa mumekwisha kujua kabisa mambo haya yote, ninataka kuwakumbusha namna Bwana alivyowaokoa Waisraeli kutoka katika inchi ya Misri, lakini kisha, akawaangamiza wale waliokataa kuamini.
6Mukumbuke vilevile wamalaika wale waliokosa kulinda vema cheo chao, lakini wakaacha makao yao: Mungu akawaweka katika nafasi ya giza, wakifungwa minyororo ya milele kwa kungojea Siku ile ya hukumu.
7Mukumbuke vilevile watu wa Sodoma na Gomora na wa miji iliyokuwa kandokando wanaokuwa sawasawa na wamalaika hawa. Walifanya uasherati na mambo ya kimwili yasiyokuwa ya kawaida ya asili. Watu hawa wanapokea hukumu ya moto wa milele kuwa mufano wazi kwa watu wote.
8Hata hivi, watu hawa vilevile wanafanana nao; maono yao yanawasukuma kuchafua miili yao na kuzarau mamlaka ya Mungu na kutukana viumbe vitukufu vya mbinguni.
9Hata Mikaeli, malaika mukubwa, aliposhindana na kubishana na Shetani juu ya maiti ya Musa, hakusubutu kumuhukumu kwa matusi, lakini alisema: “Bwana mwenyewe akukaripie.”
10Lakini watu hawa wanasema vibaya juu ya mambo wasiyoyafahamu; na mambo wanayoyajua kwa tabia yao kama nyama wasiokuwa na akili, ndiyo yale yanayowaangamiza.
11Ole kwao! Maana wamefuata njia ya Kaina. Kwa ajili ya kupata mali wameanguka katika kosa Balama alilofanya. Wameangamia kwa sababu wameasi kama vile Kora alivyoasi.Ang. Mwa 4.3-8; Hes 22.1-35; 16.1-35
12Kufika kwao kunaleta machafuko katika karamu zenu za upendo. Wanakula na kushiba pamoja nanyi pasipo haya yoyote. Wao ni kama mawingu yanayopeperushwa na upepo pasipo kuleta mvua. Wao ni kama miti isiyozaa matunda hata wakati wa mavuno; ni miti iliyoongolewa na kufa kabisa.
13Wanafanana na zoruba kubwa ya bahari na matendo yao ya haya yanaonekana kama pofu ya zoruba. Wanafanana vilevile na nyota zinazotangatanga; Mungu amekwisha kuwawekea nafasi katika giza kubwa kwa milele.
14Ni Enoki, mutu wa kizazi cha saba tangu Adamu, ndiye aliyetabiri zamani juu yao, akisema: “Musikilize, Bwana atakuja pamoja na maelfu na maelfu ya wamalaika zake watakatifu.
15Atakuja kuwahukumu wote na kuwaazibu watu wabaya wasiomwogopa Mungu, kwa ajili ya matendo yao yote mabaya waliyotenda, na kwa ajili ya maneno yote mabaya wenye zambi hawa waliyosema juu yake.”
16Watu hawa wanaendelea kunungunika na kuteta wengine. Wanaishi kufuatana na tamaa zao mbaya. Wanasema maneno ya majivuno na kujipendekeza kwa watu kusudi wapate faida toka kwao.
Maonyo na mapendekezo17Lakini ninyi wapendwa wangu, mukumbuke maneno yaliyosemwa zamani na mitume wa Bwana wetu Yesu Kristo.
18Wao waliwaambia: “Katika siku za mwisho, kutakuja watu watakaowachekelea, wakiishi kwa kufuata tamaa zao mbaya.”
19Watu hawa ndio wanaoleta matengano; wanatawaliwa na tabia za kimwili nao hawana Roho wa Mungu.
20Lakini ninyi wapendwa wangu, muendelee kusimama imara katika imani yenu inayokuwa takatifu sana, mukiomba kwa uwezo wa Roho Mutakatifu.
21Mudumu katika upendo wa Mungu, mukimungojea Bwana wetu Yesu Kristo, atakayewapa ninyi uzima wa milele kwa huruma yake.
22Mukuwe na moyo wa huruma kwa wale wanaokuwa na mashaka:
23muwaokoe, mukiwaopoa toka katika moto. Muwasikilie vilevile wengine huruma, lakini kwa woga, mukichukia hata nguo zao zilizochafuliwa na tamaa zao mbaya.
Sifa na baraka24Basi yeye anayeweza kuwalinda kusudi musianguke, na kuwasimamisha ninyi mbele ya utukufu wake pasipo kilema na kwa furaha kubwa,
25yeye anayekuwa Mungu peke yake, Mwokozi wetu, asifiwe na kuwa na ukubwa, uwezo na mamlaka, kwa njia ya Yesu Kristo Bwana wetu, tangia zamani za kale, sasa na hata milele! Amina.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.