1Mainzi waliokufa wanaharibu na kunukisha marasi;
upumbafu kidogo unapoteza hekima na heshima.
2Moyo wa mwenye hekima unamwongoza kutenda mambo yanayokuwa sawa;
lakini mutu mupumbafu anapotoshwa na moyo wake.
3Hata anapopita katika njia, anakosa akili,
anamwambia kila mutu kwamba yeye ni mupumbafu.
4Mutawala akikukasirikia, usiache kazi;
makosa makubwa yanaweza kufutwa ukiwa munyenyekevu.
5Kuna uovu niliotambua hapa chini ya jua, uovu unaosababishwa na watawala:
6wapumbafu wanapewa kazi za madaraka ya juu, na watajiri wanakamata nafasi za mwisho.
7Nimeona watumwa wanapanda juu ya farasi, na wakubwa wanatembea kwa miguu kama watumwa.
8Yeye anayechimba shimo anatumbukia ndani yake mwenyewe,
anayebomoa ukuta anaumwa na nyoka.
9Muchonga mawe anaumizwa nayo,
mukata kuni anapatwa na hatari.
10Nguvu nyingi zaidi zinahitajika
kwa mutumiaji wa shoka lisilonolewa,
lakini kutumia hekima kunamufanya mutu afanikiwe.
11Nyoka ya muchawi ikiuma mbele haijachochewa,
hakuna faida tena kwa muchawi.
12Maneno ya mwenye hekima yanamupa upendeleo;
lakini maneno ya mupumbafu yanamwangamiza.
13Mupumbafu anaanza kusema kwa maneno ya kijinga,
na kumaliza masemi yake kwa wazimu wa hatari.
14Mupumbafu anasema maneno mengi.
Mwanadamu hajui yatakayokuwa,
wala yale yatakayotukia nyuma yake.
15Mupumbafu anachokeshwa kwa kutoa jasho,
hata hajui njia ya kwenda katika muji.
16Ole wako, ewe inchi, mutawala wako akiwa kijana,
na viongozi wako wakifanya karamu asubui.
17Heri yako, ewe inchi, mutawala wako akiwa mutu wa heshima,
na viongozi wako wakifanya karamu wakati unaofaa,
kwa kujipatia nguvu na si kujilewesha.
18Kutokana na uvivu wa mutu, paa ya nyumba inaanguka;
kwa sababu ya uregevu, nyumba inavuja.
19Chakula ni kwa ajili ya kujifurahisha,
divai inachangamusha maisha,
na feza inasababisha hayo yote.
20Usimutukane mutawala hata ndani ya moyo wako,
wala usimutukane tajiri hata ndani ya chumba chako cha kulala,
maana ndege atapeleka sauti yako,
kiumbe kinachoruka kitatangaza maneno yako.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.