Kumbukumbu la Sheria 30 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Matumaini mema kwa siku zinazokuja

1Musa akaendelea kusema: “Baraka na laana hizi zote zitatimizwa. Mutafikiri juu ya mambo hayo wakati Yawe, Mungu wenu, atakuwa amewatawanya kati ya mataifa.

2Mukimurudilia Yawe, Mungu wenu, ninyi na watoto wenu, mukitii kwa moyo wote na roho yote neno lake ninalowaamuru leo,

3hapo Yawe, Mungu wenu, atawarudishia mema yenu na kuwahurumia na kuwakusanya tena kutoka katika mataifa ambamo atakuwa amewatawanya.

4Na hata kama mumetawanywa katika sehemu mbali kabisa katika dunia, Yawe, Mungu wenu, atawakusanya na kuwarudisha,

5kwa kurizi tena inchi ambamo wazee wenu waliishi. Naye atawafanya mufanikiwe zaidi na kuwa wengi kuliko wazee wenu.

6Yawe, Mungu wenu, atawafanya ninyi na wazao wenu mukuwe na moyo wa utii kusudi mumupende yeye kwa moyo wenu wote na roho yenu, mupate kuishi.

7Yawe, Mungu wenu, atafanya laana hizi zote ziwapate waadui zenu ambao waliwatesa.

8Nanyi mutatii sauti ya Yawe na kushika amri zake zote ninazowapa leo.

9Yawe, Mungu wenu, atawafanya mufanikiwe katika kila mutakalofanya; mutakuwa na watoto wengi na ngombe wengi na mashamba yenu yatatoa mazao. Maana atapenda tena kuwafanya mufanikiwe kama vile alivyopenda kuwafanikisha wazee wenu,

10ikiwa mutatii sauti yake na kushika amri na masharti yake yaliyoandikwa katika kitabu hiki cha sheria na kumurudilia Yawe, Mungu wenu, kwa moyo wote na roho yote.

11“Amri ninazowapa leo si ngumu sana kwenu, wala haziko mbali nanyi.

12Haziko mbinguni hata museme: ‘Nani atakayepanda juu mbinguni kutuletea kusudi tupate kuzisikia na kuzitii?’

13Wala haziko ngambo ya bahari, hata museme: ‘Nani atakayevuka bahari atuletee kusudi tuzisikie na kuzitii.’

14Sivyo, lakini neno hili liko karibu nanyi, ndani ya vinywa vyenu na ndani ya mioyo yenu, mupate kulitimiza.

15“Leo hii ninawapa uchaguzi kati ya mema na mabaya, kati ya uzima na kifo.

16Kama mukitii amri za Yawe, Mungu wenu, ambazo ninawapa leo, mukimupenda Yawe, Mungu wenu, na kufuata njia zake na kushika amri, masharti na maagizo yake, basi, mutaishi na kuongezeka; naye Yawe, Mungu wenu, atawabariki katika inchi ambayo munakwenda kuirizi.

17Lakini mukipotoshwa na kukataa kumusikiliza, mukivutwa kuabudu miungu mingine na kuitumikia,

18mimi ninawatangazia leo hii kwamba mutaangamia. Hamutaishi kwa muda murefu katika inchi munayokwenda kurizi, ngambo ya muto Yordani.

19Ninaita mbingu na inchi zishuhudie juu yenu leo hii, kwamba nimewapa uchaguzi kati ya uzima na kifo, kati ya baraka na laana. Basi, muchague uzima ninyi na wazao wenu mupate kuishi.

20Mumupende Yawe, Mungu wenu. Muitii sauti yake na kuambatana naye. Kama munafanya hivyo, mutapata maisha marefu na kuishi katika inchi ambayo Yawe aliwaahidi wazee wenu, Abrahamu, Isaka na Yakobo, kwamba atawapa.”

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help