2 Mambo ya Siku 18 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Nabii Mikaya anamwonya Ahabu(1 Fal 22.1-28)

1Wakati mufalme Yosafati wa Yuda alipokuwa amekwisha kuwa mutu tajiri na mwenye heshima, alifanya mupango wa ndoa kati ya jamaa yake, na jamaa ya mufalme Ahabu wa Israeli.

2Nyuma ya miaka fulani Yosafati akakwenda Samaria kumutembelea mufalme Ahabu. Ahabu akamuchinjia Yosafati kondoo na ngombe wengi, kwa heshima yake pamoja na watu waliokuwa pamoja naye, kisha akamushawishi aende pamoja naye kwa kushambulia muji wa Ramoti-Gileadi.

3Ahabu mufalme wa Israeli akamwambia Yosafati mufalme wa Yuda: “Utakwenda pamoja nami kwa kushambulia muji wa Ramoti-Gileadi?” Naye akajibu: “Mimi niko kama wewe, na watu wangu ni kama watu wako. Tutakuwa pamoja nawe katika vita.”

4Kisha Yosafati akaendelea kumwambia mufalme wa Israeli: “Lakini ninakusihi uombe kwanza shauri la Yawe.”

5Basi Ahabu akakusanya manabii mia ine, akawauliza: “Twende kushambulia muji wa Ramoti-Gileadi, au nisiende?” Wakamujibu: “Kwenda! Mungu atakupatia ushindi!”

6Lakini, Yosafati akauliza: “Hapa hakuna nabii mwingine wa Yawe ambaye tunaweza kumwuliza shauri?”

7Naye mufalme wa Israeli akamujibu Yosafati: “Kungali mumoja, Mikaya mwana wa Imula. Yeye tunaweza kumwuliza shauri la Yawe. Lakini ninamuchukia sana kwa sababu yeye hatabiri jambo jema juu yangu hata kidogo, lakini mabaya tu.” Yosafati akamwambia: “Si vizuri kwa mufalme kusema hivyo.”

8Basi, Ahabu, mufalme wa Israeli akamwita mukubwa mumoja na kumwamuru: “Haraka, kwenda umulete Mikaya mwana wa Imula.”

9Wakati ule, mufalme wa Israeli pamoja na Yosafati, mufalme wa Yuda, walikuwa wameikaa katika viti vyao vya kifalme kwenye kiwanja cha kupepetea ngano kwenye mulango wa kuingilia muji wa Samaria nao walikuwa wakivaa nguo zao za kifalme. Wakati ule manabii wote walikuwa wakitoa unabii wao mbele yao.

10Kisha mumoja wa manabii wale, Zedekia mwana wa Kenana, akajitengenezea pembe za chuma na kusema: “Yawe anasema hivi: ‘Kwa pembe hizi, utawarudisha nyuma Wasuria hata kuwaangamiza.’ ”

11Na wale manabii wengine wakatabiri vile vile wakasema: “Kwenda kushambulia muji wa Ramoti-Gileadi na kufanikiwa. Yawe atautia katika mikono yako.”

12Wakati ule, yule mutumishi aliyetumwa kwa Mikaya akamwambia: “Manabii wengine wote kwa pamoja wamemutabiria mufalme ushindi; tafazali nawe vilevile ufanye kama wao umutabirie mazuri.”

13Lakini Mikaya akamujibu: “Kama vile Yawe anavyoishi, kile Mungu wangu atakachoniambia, ndicho nitakachosema.”

14Basi Mikaya alipofika mbele ya mufalme, mufalme akamwuliza: “Twende kupigana vita kule Ramoti-Gileadi au nisiende?” Mikaya akajibu: “Kwenda na ufanikiwe, naye Yawe atawatia katika mikono yako.”

15Lakini mufalme akamwambia: “Nitakuapisha mara ngapi kwamba kila mara unaposema nami kwa jina la Yawe, unapaswa kuniambia ukweli?”

16Naye Mikaya akasema: “Niliwaona watu wote wa Israeli wakitawanyika juu ya milima kama kondoo wasiokuwa na muchungaji. Naye Yawe akasema: ‘Watu hawa hawana kiongozi; uwaache warudi kila mutu kwake kwa amani.’ ”

17Halafu mufalme wa Israeli akamwambia Yosafati: “Sikukuambia kwamba hatatabiri jema juu yangu, lakini mabaya tu?”

18Kisha Mikaya akasema: “Basi sikia neno la Yawe: Nilimwona Yawe akikaa katika kiti chake cha kifalme na jeshi lake lote la mbinguni likisimama upande wake wa kuume na wa kushoto.

19Halafu Yawe akauliza: ‘Ni nani atakayemushawishi Ahabu mufalme wa Israeli aende aangamie kule Ramoti-Gileadi?’ Kila mumoja akajibu sawa alivyofikiri.

20Kisha, pepo mumoja akajitokeza mbele ya Yawe, akasema: ‘Mimi nitamushawishi.’ Yawe akamwuliza: ‘Kwa njia gani?’

21Naye akajibu: ‘Nitakwenda na kuwasukuma manabii wake wote waseme uongo.’ Yawe akamwambia: ‘Wewe utamushawishi na utashinda; kwenda kufanya hivyo.’

22“Basi sasa angalia: Yawe ametia pepo wa uongo katika vinywa vya manabii wako. Lakini Yawe amesema mabaya juu yako!”

23Kisha nabii Zedekia mwana wa Kenana akamukaribia Mikaya, akamupiga kofi kwenye shavu na kumwuliza: “Kwa njia gani Roho wa Yawe ameniacha na akakuja kusema nawe?”

24Mikaya akamujibu: “Utatambua mambo haya siku ile utakapoingia katika chumba cha ndani kwa kujificha.”

25Naye mufalme wa Israeli akatoa amri: “Mumukamate Mikaya mumurudishe kwa Amoni, liwali wa muji, na kwa Yoasi, mwana wa mufalme,

26na kusema: ‘Mufalme anasema hivi: Mumuweke mutu huyu katika kifungo na kumulisha kwa mukate kidogo na maji kidogo, mpaka nitakaporudi salama.’ ”

27Mikaya akasema: “Ukirudi salama, basi, utajua kwamba Yawe hakusema nami.” Kisha akaendelea kusema: “Musikie, enyi watu wote!”

Kifo cha Ahabu(1 Fal 22.29-35)

28Basi, mufalme wa Israeli akaenda pamoja na Yosafati mufalme wa Yuda kwa kuushambulia muji wa Ramoti-Gileadi.

29Mufalme wa Israeli akamwambia Yosafati: “Mimi nitavaa nguo zisizokuwa za kifalme kwa kuingia katika vita, lakini wewe utavaa nguo yako ya kifalme.” Hivyo mufalme wa Israeli akaenda kwa vita bila kuvaa nguo za kifalme.

30Mufalme wa Suria alikuwa amewaamuru wakubwa wa waaskari wake waliosimamia magari yake ya vita akisema: “Musipigane na mutu ye yote mukubwa au mudogo, lakini tu na mufalme wa Israeli.”

31Halafu wakubwa wale walipomwona Yosafati, wakasema: “Huyu ndiye mufalme wa Israeli.” Kwa hiyo, wakamwelekea kwa kumushambulia; lakini Yosafati akapiga kelele, na Yawe akamwokoa. Mungu akawaondoa wale waliokuwa karibu kumushambulia.

32Wakubwa wa waaskari walipotambua kwamba hakukuwa mufalme wa Israeli, wakaacha kumushambulia, wakarudi.

33Lakini askari mumoja wa Suria akauvuta upinde wake, kwa kubahatisha, akamupiga mufalme wa Israeli mushale katika nafasi ya maunganio ya nguo yake ya chuma ya kujikinga kifua. Hapo Ahabu akamwambia mwongozi wa gari lake la vita: “Geuza gari uniondoe katika vita nimeumizwa.”

34Nayo mapigano siku ile, yakazidi kuwa makali wakati mufalme wa Israeli amejiegemeza mwenyewe ndani ya gari akiwaelekea Wasuria mpaka magaribi. Halafu wakati jua liliposhuka, akakufa.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help