Amosi 7 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Maono ya kwanza: Nzige

1Bwana wetu Yawe alinionyesha hivi: Yawe alikuwa anaumba nzige kundi zima, nyuma ya watu kumaliza kukata majani kwa ajili ya nyama wa mufalme. Wakati ule, majani yalikuwa ndio yanaanza kuchipuka tena.

2Niliwaona nzige hao wakikula na kumaliza kila jani katika inchi. Halafu nikasema:

Ee Bwana wetu Yawe, ninakusihi utuhurumie!

Wazao wa Yakobo wataweza kuishi namna gani?

Wao ni wadogo sana!

3Basi, Bwana wetu Yawe akabadilisha nia yake,

akasema: Halitatukia!

Maono ya pili: Moto

4Bwana wetu Yawe alinionyesha tena maono mengine: Bwana wetu Yawe akiuita moto wa hukumu wa kuwaazibu watu. Moto ule uliunguza vilindi vikubwa vya bahari, ukaanza kuiteketeza inchi kavu.

5Halafu nikasema:

Ee Bwana wetu Yawe, ninakusihi uache kuazibu!

Wazao wa Yakobo wataweza kuishi namna gani?

Wao ni wadogo sana!

6Basi, Yawe akabadilisha nia yake,

akasema: Hili vilevile halitatukia.

Maono ya tatu: Timazi

7Yawe alinionyesha tena maono mengine: Yawe alikuwa anasimama karibu na ukuta, akishika katika mukono wake uzi wenye timazi.

8Naye akaniuliza: Amosi, unaona nini? Nikamujibu: Ninaona timazi. Kisha Yawe akasema:

Ninaweka timazi kati ya watu wangu Waisraeli.

Sitavumilia tena maovu yao.

9Kule kwenye vilima ambapo wazao wa Isaka wanatambikia,

kutafanywa kuwa uharibifu mutupu

na mahekalu ya Waisraeli yatakuwa mabomoko.

Nitaushambulia kwa vita ukoo wa mufalme Yeroboamu.

Amosi na Amazia

10Basi, Amazia kuhani wa muji wa Beteli, akamupelekea mufalme Yeroboamu wa Israeli habari hii: Amosi analeta fitina juu yako katika ufalme wa Israeli. Hotuba zake ni hatari kwa inchi hii.

11Anachosema ni hiki:

Yeroboamu atakufa kwa upanga

nao Waisraeli watapelekwa katika uhamisho,

mbali kabisa na inchi yao.

12Kisha Amazia akamwambia Amosi: Sasa tumechoka nawe, ewe nabii! Uende! Urudie katika inchi ya Yuda, utoe unabii kule upate na chakula chako kulekule.

13Usitoe tena unabii hapa katika Beteli, kwa sababu hapa ni pahali ya ibada ya mufalme; ni hekalu la utawala huu.

14Amosi akamujibu Amazia: Mimi si nabii wa mushahara, wala si mumoja wa kikundi cha manabii. Mimi ni muchungaji na mulimaji wa miti ya mikuyu.

15Yawe alinitosha katika kazi yangu hiyo ya uchungaji, akaniamuru nikuje kuwaambia watu wake wa Israeli unabii.

16Nawe basi, ewe Amazia,

sikiliza neno la Yawe:

Wewe unaniambia nisitoe unabii juu ya Waisraeli,

wala nisiseme neno lolote juu ya wazao wa Isaka.

17Kwa hiyo, Yawe anasema hivi:

Muke wako atakuwa kahaba katika muji,

na wana wako na wabinti zako watauawa katika vita.

Inchi yako itagawanywa na kupewa wengine,

nawe mwenyewe utakufia katika inchi inayohesabiwa kuwa chafu;

nao Waisraeli hakika watapelekwa katika uhamisho,

mbali kabisa na inchi yao.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help