Matendo ya Mitume 13 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Barnaba na Saulo wanasimikwa kwa kazi

1Katika kanisa la Antiokia kulikuwa manabii na walimu wamoja. Kati yao kulikuwa Barnaba, Simoni aliyeitwa vilevile Nigeri; Lukio wa Kurene, Saulo na Manaeni, aliyekomaa pamoja na mufalme Herode.

2Siku moja walipokuwa wakifanya ibada, wakiwa wamefunga kula chakula, Roho Mutakatifu akasema: “Muwasimike Barnaba na Saulo kwa kazi ile niliyowachagulia.”

3Basi wakafunga tena kula chakula na kuomba. Kisha wakaweka mikono juu yao na kuwatuma waende safari.

Saulo na Barnaba katika Kipuro

4Halafu Barnaba na Saulo wakaenda kwenye kivuko cha Seleukia kwa uongozi wa Roho Mutakatifu. Kule wakaingia ndani ya chombo na kwenda mpaka katika kisanga cha Kipuro.

5Nao walipofika katika muji Salami, wakahubiri Neno la Mungu katika nyumba za kuabudia za Wayuda. Yoane alikuwa pamoja nao, akiwasaidia kwa kufanya kazi.

6Walipokwisha kupita katika kisanga chote, wakafika katika muji Pafo. Kule wakakutana na Muyuda mumoja aliyekuwa muchawi na nabii wa uongo, jina lake Bara-Yesu.

7Huyo alitumika pamoja na liwali mumoja mwenye akili, aliyeitwa Sergio Paulo. Liwali huyo akawaita Barnaba na Saulo wafike kwake kwa sababu alitaka kusikia Neno la Mungu.

8Lakini yule muchawi Elema, (kufuatana na maana ya jina lake katika Kigriki), akapingana nao, akitaka kumugeuza yule liwali kusudi asiamini Neno la Mungu.

9Halafu Saulo, anayeitwa vilevile Paulo, akiwa amejazwa na Roho Mutakatifu, akamukazia macho

10na kusema: “Wewe mutoto wa Shetani unayejaa udanganyifu na ukorofi wa kila namna! Wewe usiyependa kuona jambo la haki! Wewe hauchoki na kugeuza maneno ya ukweli ya Bwana!

11Basi, sasa Bwana atakuazibu, nawe utakuwa kipofu, wala hautaweza hata kidogo kuona mwangaza kwa muda.”

Mara moja macho ya Elema yakaingiwa na giza hata yakapofuka, naye akaanza kupapasapapasa akitafuta mutu wa kumwongoza.

12Yule liwali alipoona mambo yale yaliyotokea, akashangaa na mafundisho ya Bwana hata akapata kumwamini.

Barnaba na Saulo katika muji Antiokia wa Pisidia

13Kisha Paulo na wenzake wakaingia ndani ya chombo, wakaondoka katika muji Pafo na kwenda katika muji Perga katika jimbo la Pamfilia. Walipofika kule Yoane aliyeitwa vilevile Marko akaachana nao na kurudi Yerusalema.

14Kutoka kule wakaendelea na safari yao na kufika mpaka katika muji Antiokia wa jimbo la Pisidia. Siku ya Sabato ilipotimia, wakaingia ndani ya nyumba ya kuabudia na kuikaa mule.

15Na nyuma ya kusoma katika vitabu vya Sheria na vya manabii, wakubwa wa ile nyumba ya kuabudia wakatuma mutu kwa kuwaambia: “Wandugu, ikiwa muko na maneno ya kuwatia watu moyo, muyaseme.”

16Basi Paulo akasimama, akainua mukono kwa kuwaalika wanyamaze. Akasema: “Munisikilize ninyi wanainchi wenzangu Waisraeli, nanyi watu wa mataifa mengine munaomwogopa Mungu!

17Mungu wa taifa hili la Waisraeli aliwachagua babu zetu, naye akawafanya kuwa taifa kubwa walipokuwa wakikaa kama wageni katika inchi ya Misri. Kisha akawaondosha kule kwa uwezo wake mukubwa

18na kuwavumilia katika jangwa kwa muda wa miaka makumi ine.

19Naye alipokwisha kuteketeza mataifa saba yaliyokaa katika inchi ya Kanana, akatoa inchi ile kwa lile taifa lake kuwa urizi wao.

20Mambo haya yote yalitendeka kwa muda wa miaka yapata mia ine makumi tano.

“Kisha akawapa waamuzi kwa kuwaongoza mpaka katika siku za nabii Samweli.

21Na kisha wakaomba wapewe mufalme. Kwa hiyo Mungu akawawekea Saulo, mwana wa Kisi, wa kabila la Benjamina kwa kuwatawala kwa muda wa miaka makumi ine.

22Kisha kumwondosha Saulo, Mungu akasimika Daudi kuwa mufalme wao. Na yeye mwenyewe alimushuhudia akisema: ‘Nimejichagulia Daudi mwana wa Yese, kwa maana ni mutu mwenye kunipendeza. Huyu ndiye atakayefanya mambo yote ninayotaka.’

23Na toka katika uzao wa mutu huyo Mungu akawaletea Waisraeli Mwokozi, ndiye Kristo, kama vile alivyokuwa amewaahidia.

24Mbele Yesu hajajionyesha, Yoane alihubiri kwa Waisraeli wote kwamba wageuke toka zambi zao na kubatizwa.

25Na Yoane alipokaribia kwa mwisho wa kazi yake, alisema: ‘Munafikiri mimi ni nani? Mimi siko yule munayengojea. Lakini angalia, nyuma yangu kutakuja mutu ambaye mimi sistahili hata kufungua kamba za viatu vyake.’

26“Wandugu zangu, ninyi wazao wa Abrahamu na ninyi watu wa mataifa mengine munaokuwa hapa kwa kumwabudu Mungu, habari hii ya wokovu imetumwa kwetu!

27Wakaaji wa Yerusalema na wakubwa wao hawakumutambua Yesu wala maandiko ya manabii yaliyosomwa kila siku ya Sabato. Lakini ingawa hivi wakatimiza maandiko yale kwa njia ya kumuhukumu kufa.

28Ijapokuwa hawakupata sababu ya kumuhukumu kufa, wakamwomba Pilato awape ruhusa ya kumwua.

29Na wakati walipokwisha kutimiza yote yaliyoandikwa juu yake, wakamushusha toka juu ya musalaba na kumuzika.

30Lakini Mungu akamufufua.

31Na kwa siku nyingi akaonekana kwa waliosafiri pamoja naye toka Galilaya kwenda Yerusalema. Na wale ndio sasa wanaomushuhudia mbele ya watu.

32Na sasa sisi tunahubiri Habari Njema kwenu kwamba, ile Mungu aliyoitoa kwa babu zetu

33ameitimiza kwa ajili yetu sisi wazao wao. Amefanya hivi kwa kumufufua Yesu kwa kuhakikisha maandiko haya ya Zaburi ya pili yanayosema:

‘Wewe ni mwana wangu,

mimi leo ninakuwa baba yako.’

34Na juu ya ufufuko wa Yesu, kusudi asipate kuoza, Mungu alisema:

‘Nitakupa baraka takatifu zinazokuwa za hakika,

nilizomwahidia Daudi.’

35Na kwa hiyo inasemwa tena katika maandiko mengine:

‘Hautakubali mutumishi wako mutakatifu aoze.’

36Lakini Daudi alipokwisha kutumika sawasawa na kusudi la Mungu katika maisha yake, akakufa na kwenda kukutana na babu zake waliomutangulia, naye akaoza.

37Lakini yule Mungu aliyemufufua hakuoza.

38-39“Basi wandugu zangu, mujue hakika kwamba kwa njia ya huyo, habari ya kusamehewa zambi inahubiriwa kwenu. Na zaidi ya hii, hakuna mutu anayeweza kuhesabiwa haki katika mambo yote kwa njia ya kushika Sheria ya Musa. Lakini kila mutu anayemwamini anahesabiwa haki katika mambo yale.

40Basi mujiangalie vizuri kusudi maneno haya ya manabii yasiwapate ninyi:

41‘Muangalie, ninyi wenye kuzarau,

mupigwe na mushangao na mutoweke!

Maana katika siku hizi nitafanya jambo ambalo ninyi musingeweza kusadikia hata wangewaelezea.’ ”

42Paulo na Barnaba walipotoka ndani ya ile nyumba ya kuabudia, watu wakawasihi warudie tena kuwaelezea maneno yale yale kwa siku ya Sabato iliyofuata.

43Nyuma ya mukutano, Wayuda wengi na watu wa mataifa mengine waliogeuka kufuata dini ya Kiyuda, waliomwogopa Mungu, wakawafuata Paulo na Barnaba. Nao wawili wakasema na watu hao na kuwatia moyo kusudi waendelee kutegemea neema ya Mungu.

44Siku ya Sabato iliyofuata, karibu watu wote wa muji wakakusanyika kwa kusikia neno la Bwana.

45Wayuda walipoona lile kundi la watu, wakajaa na wivu sana, nao wakapinga maneno Paulo aliyosema na kumutukana.

46Halafu Paulo na Barnaba wakawaambia bila woga: “Ilitupasa kwanza kuhubiri Neno la Mungu kwenu. Lakini kwa kuona mumelikataa na kujihesabu ninyi wenyewe kwamba uzima wa milele haufai kwenu, basi tunashugulika na watu wa mataifa mengine.

47Kwa maana Bwana ametuagiza hivi:

‘Nimekuweka kuwa mwangaza wa mataifa,

kusudi watu wapate kuokolewa katika dunia yote.’ ”

48Wakati watu wa mataifa mengine waliposikia maneno haya wakafurahi, wakatukuza neno la Bwana. Nao wote waliokuwa wamechaguliwa kwa kupata uzima wa milele, wakaamini.

49Neno la Bwana likaenea katika inchi ile yote.

50Lakini Wayuda wakawashawishi wakubwa wa muji pamoja na wanawake wamoja wenye heshima, walioabudu Mungu. Wakawatesa Paulo na Barnaba hata wakawafukuza toka katika inchi yao.

51Halafu hawa mitume wakawakungutia mavumbi toka juu ya miguu yao, na kwenda katika muji Ikonio.

52Nao wanafunzi wa Antiokia walijazwa na furaha na Roho Mutakatifu.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help