1Wakaendelea na safari yao, wakapita katika muji wa Amfipoli na wa Apolonia, na wakafika Tesalonika. Kule kulikuwa nyumba ya kuabudia ya Wayuda.
2Na sawa ilivyokuwa desturi, Paulo akaingia katika nyumba ile. Kwa muda wa siku tatu za Sabato zilizofuatana juma kwa juma, akabishana na watu waliokuwa mule, akitumia Maandiko Matakatifu.
3Aliwaelezea na kuwaonyesha wazi kwamba Kristo alipaswa kuteswa na kufufuka. Akawaambia: “Huyu Yesu ninayemuhubiri kwenu ndiye Kristo.”
4Wamoja kati ya Wayuda wakasadiki na kujiunga pamoja na Paulo na Sila. Vilevile kundi kubwa la Wagriki walioogopa Mungu pamoja na wanawake wengi wenye heshima wakasadiki.
5Lakini Wayuda wakajaa na wivu, hata wakakusanya watu wamoja wa ovyo ovyo waliowakuta kwenye nafasi za makutano, na kufanya kikundi. Kisha wakafanya fujo katika muji wote. Wakashambulia nyumba ya Yasoni, wakiwatafuta Paulo na Sila kusudi wawapeleke mbele ya watu.
6Kwa kuwa hawakuwapata, wakamupeleka Yasoni pamoja na wandugu waamini wengine mbele ya wakubwa wa muji. Wakalalamika wakisema: “Watu hawa walifanya fujo fasi zote na sasa wamefika huku.
7Naye Yasoni amewakaribisha kwake! Hawa wote wanatembea kinyume cha amri za Mufalme wa Roma wakisema kwamba kuna mufalme mwingine anayeitwa Yesu.”
8Maneno haya yakafazahisha kundi la watu pamoja na wakubwa wa muji.
9Wakubwa wa muji walipokwisha kumulipisha Yasoni na wenzake feza, wakawaachilia kwenda.
Paulo na Sila katika muji Beroya10Mara moja ilipokuwa usiku, wanafunzi wakawasindikiza Paulo na Sila waende Beroya. Nao walipofika kule, pale pale wakaingia katika nyumba ya kuabudia ya Wayuda.
11Watu hao walikuwa wenye nia nzuri zaidi kuliko watu wa Tesalonika; nao walipokea Neno la Mungu kwa hamu kubwa. Kila siku walichunguza Maandiko Matakatifu wapate kujua kwamba maneno Paulo aliyosema yalikuwa ya haki.
12Basi Wayuda wengi kati yao wakaamini pamoja na wanawake wengi Wagriki wenye heshima, na hesabu yenye kutosha ya wanaume vilevile.
13Lakini Wayuda wa muji wa Tesalonika wakapata habari kwamba Paulo anahubiri Neno la Mungu vilevile katika muji Beroya. Kwa hiyo wakaenda kule, wakaanza kufanya fujo kati ya makundi ya watu na kuwachochea.
14Halafu pale pale, wandugu waamini wakamusindikiza Paulo mpaka kwenye kivuko, lakini Sila na Timoteo wakabaki Beroya.
15Nao wale waliomwongoza Paulo wakamufikisha mpaka katika muji wa Atene. Kisha wakarudi Beroya wakiwa wameagizwa na Paulo kwamba wawaambie Timoteo na Sila wamufuate upesi.
Paulo katika muji Atene16Paulo alipokuwa akingojea Sila na Timoteo kule Atene, moyo wake ukavunjika sana kuona namna muji ule ulivyojaa sanamu za miungu.
17Alikuwa akibishana na Wayuda katika nyumba ya kuabudia pamoja na watu wa mataifa mengine walioogopa Mungu. Vilevile alibishana kila siku na watu aliowakuta kwenye nafasi ya makutano.
18Walimu wamoja wa kikundi cha Waepikurio na cha Wastoiko, wakaanza kubishana na Paulo. Wamoja wao wakauliza: “Huyu katetea anataka kusema nini?” Wengine wakasema: “Anaonekana kuwa muhubiri wa miungu ya kigeni.” Walisema hivi kwa sababu Paulo alikuwa akihubiri juu ya Yesu na jinsi alivyofufuka.
19Halafu wakamukamata Paulo, na kumupeleka mbele ya Baraza Kubwa inayoitwa “Areopago,” wakamwuliza: “Unaweza kutujulisha maana ya mafundisho haya mapya unayotoa?
20Kwa maana unatuelezea mambo ya kigeni. Basi tunataka kujua maana yake.”
21(Haya yote ni kwa kuwa wazaliwa wa Atene pamoja na wageni walioishi kati yao, wanapitisha wakati wao wote kwa kueleza na kusikiliza habari mupya mupya.)
22Halafu Paulo akasimama mbele ya Areopago na kusema: “Ninyi wakaaji wa Atene, ninaona kwamba ninyi ni watu munaopenda sana mambo yote ya dini.
23Kwa maana nilipokuwa nikipitapita katika muji wenu nilichunguza nafasi zenu za kuabudia, nikaona hata mazabahu mamoja ambako waliyochora maandiko haya: ‘Kwa ajili ya mungu asiyejulikana.’ Basi yule munayemwabudu pasipo kumujua ndiye mimi ninayemuhubiri kwenu sasa.
24Mungu aliyeumba ulimwengu na vitu vyote vinavyokuwa ndani yake, yeye anayekuwa Bwana wa mbingu na dunia, hakai ndani ya hekalu zilizojengwa na watu.
25Yeye hahitaji kushugulikiwa na watu, kama vile angekuwa na lazima ya musaada fulani. Kwa maana yeye ndiye anayewapa watu wote pumzi ya uzima, pamoja na vitu vyote wanavyohitaji.
26Kutokana na mutu mumoja, yeye aliumba watu wa mataifa yote kusudi waishi katika dunia yote. Aliwapangia nyakati na kukata mipaka ya inchi wanayopaswa kukaa ndani yake.
27Mungu alitaka watafute kumujua, na kama ikiwezekana wamutambue hata ikiwa kama kwa njia ya kupapasa. Na kweli yeye hayuko mbali na kila mumoja wetu,
28maana
‘kwa uwezo wake tunaishi, tunatenda na kuendelea kuwa.’
Ni sawa na maneno ya watunga mashairi wamoja wa kwenu waliosema:
‘Sisi vilevile tuko watoto wake.’
29Basi kwa kuwa sisi tuko watoto wa Mungu, tusiwaze kwamba anafanana na sanamu ya zahabu au ya feza au ya jiwe, iliyochorwa kwa ufundi na akili ya watu.
30Mungu hahesabu tena nyakati zile watu walipokuwa katika ujinga, lakini sasa anatangaza kwa watu wote, na nafasi zote kwamba wageuke toka zambi zao.
31Kwa maana amekwisha kupanga siku atakapohukumu dunia kwa haki, kwa njia ya mutu mumoja, yule aliyemuweka kwa kazi ile. Naye amehakikisha mambo hayo kwa kumufufua mutu yule.”
32Nao waliposikia Paulo akisema juu ya ufufuko, wamoja wakamuchekelea na wengine wakasema: “Tutakusikiliza tena ukisema juu ya habari hii siku ingine.”
33Ni vile Paulo alivyoachana nao.
34Ingawa vile watu wamoja walijiunga naye na kuamini. Kati yao kulikuwa Dionisio, mumoja wa Baraza Kubwa inayoitwa Areopago, pamoja na mwanamuke mumoja aliyeitwa Damari na watu wengine vilevile.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.