Amosi 9 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Azabu ya Mungu

1Nilimwona Yawe akisimama pembeni ya mazabahu,

naye akaniamuru:

Piga zile nguzo za hekalu

mpaka misingi yake itikisike.

Uvunje zile nguzo ziwaangukie watu juu ya vichwa.

Wale watakaobaki nitawaua kwa upanga;

hakuna hata mumoja wao atakayeponyoka,

hakuna atakayetoroka.

2Hata wakijichimbia njia ya kwenda kuzimu,

nitawakamata kule kwa mukono wangu;

hata wakipanda juu mbinguni,

nitawaporomosha chini.

3Hata wakijificha juu ya mulima Karmeli,

huko nitawatafuta na kuwakamata;

hata wakijificha mbali nami katika vilindi vya bahari,

mule nitaiamuru nyoka kubwa ya bahari iwaume.

4Hata wakikamatwa mateka na waadui zao,

nitatoa amri kule wauawe kwa upanga.

Nitawachunga kwa uangalifu sana

nipate kuwatendea mabaya na si mema.

5Bwana wetu Yawe wa majeshi,

anaigusa dunia nayo inatetemeka,

na wakaaji wake wanaomboleza;

dunia nzima inapanda na kushuka

kama vile muto Nili wa Misri unavyojaa na kupunguka.

6Yawe amejenga makao yake mbinguni,

nayo dunia akaifunika kwa anga;

anayaita maji ya bahari,

na kuyamwanga juu ya inchi kavu.

Yawe, ndilo jina lake!

Kutengeneza kisha uharibifu

7Kwangu mimi, ninyi Waisraeli,

muko sawasawa na watu wa Kushi!

–Ni ujumbe wa Yawe.–

Niliwatoa Wafilistini kutoka Krete,

na Waaramu kutoka Kiri,

kama nilivyowatoa ninyi kutoka Misri.

8Ninauangalia ufalme wenye zambi,

na nitauangamiza kabisa kutoka katika dunia.

Lakini sitawaangamiza wazao wote wa Yakobo.

–Ni ujumbe wa Yawe.

9Nitatoa amri,

na kuwapepeta Waisraeli kati ya mataifa

kama mutu anavyopepeta ngano

kusudi niwatoshe wote wasiofaa.

10Wenye zambi kati ya watu wangu,

watakufa katika vita.

Hao ndio wanaosema:

Hasara haitatufikia wala kutupata!

11Siku inakuja nitakapoisimika nyumba ya Daudi iliyoanguka;

nitazitengeneza kuta zake,

na kusimika upya mabomoko yake.

Nitaijenga upya kama ilivyokuwa tangu zamani.

12Nao Waisraeli watarizi mabaki ya inchi ya Edomu

na mataifa yote yaliyokuwa yangu.

–Ni ujumbe wa Yawe, yule anayefanya hivyo.

13Siku zinakuja ambapo

wakati wa kuvuna utafuata mbio

wakati wa kulima,

wakati wa kukamua zabibu utafuata mbio

wakati wa kupanda mizabibu.

–Ni ujumbe wa Yawe.–

Milima itabubujika divai mupya,

navyo vilima vitatiririka divai.

14Nitarudisha hali ya mbele ya watu wangu Waisraeli.

Watajenga miji yao iliyoharibiwa na kuishi ndani yake;

watapanda mizabibu na kunywa divai yake;

watalima mashamba na kula mazao yake.

15Nitawasimika katika inchi yao,

wala hawataongolewa tena

kutoka katika inchi niliyowapa.

–Ni Yawe anayesema hivyo.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help