Mezali 25 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Mezali zingine za Solomono

1Hizi nazo ni mezali nyingine za mufalme Solomono zilizoandikwa na watu wa Hezekia, mufalme wa Yuda.

2Mungu anatukuzwa kwa kuficha mambo, lakini wafalme wanatukuzwa kwa kuchunguza mambo.

3Kama vile mbingu zinavyokuwa mbali juu na dunia mbali chini, ndivyo inavyokuwa vigumu kuelewa akili za mufalme.

4Toa takataka katika feza, na mufuaji wa vyuma atakutengenezea chombo kizuri.

5Uwaondoe waovu mbele ya mufalme, na utawala wake utaimarika katika haki.

6Usijipendekeze kwa mufalme, wala usijifanye mutu mukubwa,

7maana ni heri kuambiwa: “Kuja huku mbele”, kuliko kuporomoshwa mbele ya mukubwa.

8Mambo uliyoona kwa macho yako, usiharakishe kuyapeleka katika tribinali; maana utafanya nini kwa mwisho, kama jirani yako anakupatisha haya?

9Utengeneze ugomvi na mwenzako peke yake, na kila mumoja wenu asitoe siri ya mwenzake;

10watu wanaokusikia wasikuzarau, nawe usijiharibishie heshima kwa siku zote.

11Neno linalosemwa kwa wakati unaofaa, ni kama michoro ya zahabu juu ya feza.

12Onyo la mwenye hekima kwa mutu musikilivu ni bora kuliko pete au ushanga wa zahabu safi.

13Mujumbe mwaminifu anamufurahia yule aliyemutuma, kama maji ya baridi wakati wa joto la mavuno.

14Kama vile mawingu na upepo bila mvua, ndivyo anavyokuwa mutu anayeahidi zawadi na haitoi.

15Kwa uvumilivu mutawala anaweza kusadikishwa; ulimi laini unavunja mifupa.

16Unapopata asali, kula sehemu ya kukutoshelea, kusudi usishibe na kuitapika.

17Usimutembelee jirani yako mara kwa mara, kusudi asichoke nawe na kukuchukia.

18Mutu anayetoa ushuhuda wa uongo juu ya mwenzake, ni hatari kama nyundo, upanga au mushale mukali.

19Kumutegemea mutu asiyeaminiwa wakati wa taabu, ni kama kutegemea jino zaifu au muguu ulioteguka.

20Kumwimbia mutu mwenye huzuni ni kama kumuvua nguo wakati wa baridi, au kutia siki katika kidonda.

21Adui yako akiwa na njaa, umupe chakula; akiwa na kiu, umupe maji ya kunywa.

22Hivyo utamufezehesha, kama vile kumwanga makaa ya moto juu ya kichwa chake. Yawe atakupa zawadi.

23Upepo wa kaskazini unaleta mvua; vilevile mwenye kusingiziana analeta chuki.

24Afazali kuishi pembeni juu ya paa, kuliko kuishi ndani ya nyumba pamoja na mwanamuke mugomvi.

25Kama vile maji baridi kwa mwenye kiu, ndivyo habari njema kutoka mbali inavyokuwa.

26Mwenye haki anayekubali kufuata mambo ya mwovu ni chemichemi iliyochafuliwa au kisima kinachotofuliwa.

27Si vizuri kula asali nyingi sana; vilevile haifai kujipendekeza sana.

28Mutu asiyeweza kuzuia hasira yake ni kama muji usiokuwa na ulinzi unaposhambuliwa.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help