Zaburi 40 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Mashairi ya sifa

1Kwa mukubwa wa waimbaji. Zaburi ya Daudi.

2Nilimungojea Yawe kwa uvumilivu,

akanielekea na kusikia kilio changu.

3Aliniondoa katika shimo la hatari,

alinitoa katika matope mengi,

akanisimamisha salama juu ya mulima,

na kuziimarisha hatua zangu.

4Alinifundisha wimbo mupya,

wimbo wa sifa kwa Mungu wetu.

Wengi wataona, wataogopa,

na kisha watamutumainia Yawe.

5Heri mutu anayemutumainia Yawe,

mutu asiyejiunga na watu wenye majivuno,

watu waliopotoka kwa kuabudu miungu ya uongo.

6Ee Yawe, Mungu wangu, umetufanyia maajabu mengi,

na mipango yako juu yetu haihesabiki;

hakuna yeyote anayekuwa kama wewe.

Kama ningeweza kusimulia hayo yote,

hesabu yake ingenishinda.

7Wewe hautaki sadaka za kuteketezwa kwa moto wala matoleo,

sadaka za nyama za kuteketezwa wala za kusamehewa zambi,

lakini umenipa masikio nikusikie.

8Halafu nikasema: “Ninakuja.

Katika kitabu imeandikwa juu yangu.

9Ninataka kutimiza mapenzi yako, ee Mungu wangu;

sheria yako ninaishika kwa moyo wangu wote!”

10Nimesimulia habari njema ya ukombozi,

mbele ya kusanyiko kubwa la watu.

Kama unavyojua, ee Yawe,

mimi sikujizuia kuitangaza.

11Sikuficha katika moyo wangu ukombozi ulionijalia.

Nimetangaza siku zote kwamba wewe ni mwokozi mwaminifu.

Sikuficha kusanyiko kubwa la watu

wema wako na uaminifu wako.

Kuomba musaada

12Ee Yawe, usikose kunirehemu!

Wema na uaminifu wako vinilinde.

13Hatari zisizohesabika zinanizunguka,

maovu yangu yananisonga hata siwezi kuona;

ni mengi kuliko nywele zangu,

nami nimevunjika moyo.

14Upendezwe, ee Yawe, kuniokoa;

ee Yawe, ukuje haraka kunisaidia.

15Wote wanaokusudia kuniangamiza,

wafezeheke pamoja!

Hao wanaotamani niumie,

warudi nyuma na kuzarauliwa!

16Hao wanaonisimanga,

wafezeheke kwa kushindwa kwao!

17Lakini wanaokutafuta wafurahi na kushangilia.

Wanaopenda uwaokoe waseme siku zote:

“Yawe ni mukubwa!”

18Mimi ni masikini na mukosefu, ee Bwana;

lakini wewe haukunisahau.

Wewe ni musaada wangu na mwokozi wangu;

ukuje, ee Mungu wangu, usikawie!

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help