1Solomono alianza kujenga nyumba ya Yawe katika mwaka wa mia ine na makumi nane kisha Waisraeli kutoka Misri. Huo ulikuwa mwaka wa ine wa utawala wa Solomono juu ya Israeli, katika mwezi wa Zivu, ni kusema mwezi wa pili.
2Nyumba hiyo ambayo mufalme Solomono alimujengea Yawe ilikuwa na urefu wa metre makumi mbili na saba, upana metre kenda, na metre kumi na tatu na nusu urefu wa kwenda juu.
3Uwanja wa baraza ya nyumba ulikuwa na upana wa metre ine na nusu toka upande mumoja wa nyumba mpaka upande mwingine. Na kina chake mbele ya hiyo nyumba kilikuwa metre tisa.
4Aliiwekea nyumba hiyo madirisha mapana kwa ndani na membamba kwa inje.
5Tena aliongeza kujenga nguzo kuzunguka, kwa kutegemeza ukuta wa inje. Akatengeneza vyumba vya pembeni kila upande.
6Vyumba vya chini, katika hivyo vyumba vya nyongezo, vilikuwa na upana wa metre mbili na sentimetre makumi mbili na tano, na gorofi iliyofuata ilikuwa na upana wa metre mbili na sentimetre makumi ine na tano, na gorofi ya juu kabisa ilikuwa na upana wa metre tatu. Gorofi hizo zilikuwa zimetofautiana kwa upana, kwa sababu Solomono alikuwa amepunguza kipimo cha ukuta wa inje kuzunguka nyumba, kusudi miti ya kutegemeza jengo isishikamane na kuta.
7Wakati nyumba ilipokuwa inajengwa, hakukusikilika ndani ya nyumba mulio wa nyundo, wala wa chombo chochote cha chuma, maana ilijengwa kwa mawe yaliyokuwa yamechongwa na kutayarishwa kabisa kule walikoyachimba.
8Mulango wa kuingilia sehemu ya chini ya jengo lililoongezwa kwenye ubavu wa nyumba, ulikuwa upande wa kusini. Ndani, mulikuwa ngazi ambayo watu waliweza kupandia kwa kwenda kwenye gorofi ya katikati na ya mwisho.
9Hivyo, Solomono aliijenga nyumba, ikamalizika. Dari ya nyumba alikuwa ameitengeneza kwa boriti na mbao za mierezi.
10Kuuzunguka ukuta wa inje wa nyumba hiyo, alijenga vyumba kila gorofi ikiwa na urefu wa kwenda juu metre mbili na sentimetre makumi mbili na tano; navyo vilikuwa vimeunganishwa na nyumba kwa boriti za mierezi.
11Wakati ule, neno la Yawe lilimufikia Solomono kusema hivi:
12“Juu ya nyumba hii unayoijenga, kama ukifuata masharti yangu, ukiyatii maagizo yangu na amri zangu zote, nitakutimizia mambo yote niliyomwahidi baba yako Daudi.
13Mimi nitakaa kati ya wazao wa Waisraeli, na sitawaacha hata kidogo watu wangu, Waisraeli.”
14Hivyo, Solomono akaijenga nyumba na kuimaliza.
Mapambo ya ndani ya hekalu(2 Sik 3.8-14)15Upande wa ndani wa kuta za nyumba aliufunika kwa mbao za mierezi, kutokea kwenye sakafu mpaka kwenye boriti za dari; na sakafu akaitandikia mbao za miberoshi.
16Chumba cha ndani, kilichoitwa Pahali Patakatifu Sana, kilijengwa katika sehemu ya nyuma ya nyumba. Kilikuwa kimejengwa kwa mbao za mierezi kutokea kwenye sakafu mpaka kwenye dari, na urefu wake ulikuwa metre tisa.
17Nyumba ile iliyokuwa mbele ya Pahali Patakatifu Sana, ilikuwa na urefu wa metre kumi na nane.
18Mbao za mierezi zilizofunika ukuta wa nyumba kwa ndani zilikuwa zimepambwa kwa michoro ya maboga na maua yaliyochanua. Kila sehemu ilikuwa imefunikwa kwa mbao za mierezi, wala hakuna jiwe lililoonekana.
19Katika sehemu ya ndani kabisa ya jengo hilo, Solomono alitayarisha chumba cha pekee ambamo Sanduku la Agano la Yawe liliwekwa.
20Chumba hicho kilikuwa na metre tisa urefu, metre tisa upana, na metre tisa kwenda juu; nacho kilipambwa kwa zahabu safi. Vilevile, alitengeneza mazabahu kwa mbao za mierezi.
21Solomono aliipamba kwa zahabu safi sehemu ya ndani ya nyumba, na mbele ya hicho chumba cha ndani akaweka minyororo ya zahabu kutoka upande mumoja mpaka upande wa pili, aliipamba kwa zahabu.
22Nyumba yote aliipamba kwa zahabu, na mazabahu yote iliyokuwa katika chumba cha ndani kabisa.
23Alitengeneza kwa mbao za mizeituni sanamu za makerubi wawili, kila sanamu ikiwa na metre ine na nusu kwenda juu, akaziweka katika chumba cha ndani kabisa.
24Kila bawa lilikuwa na urefu wa metre mbili na sentimetre makumi mbili na tano; kwa hiyo urefu kutoka incha ya bawa moja mpaka incha ya bawa lingine ulikuwa metre ine na nusu.
25Kerubi mwingine alikuwa na urefu wa metre ine na nusu; makerubi wote wawili walikuwa na vipimo vilevile na umbo lilelile.
26Urefu wa kerubi mumoja ulikuwa metre ine na nusu; vilevile urefu wa kerubi mwingine ulikuwa uleule.
27Sanamu hizo zilielekeana, zikiwa na mabawa yaliyokunjuliwa: bawa la mumoja likigusa ukuta mumoja, na bawa la mwingine likigusa ukuta wa pili, na yale mengine yaligusana katikati ya chumba.
28Nazo sanamu hizo alizipamba kwa zahabu.
29Kuta za kila chumba alizipamba kwa kuchongwa michoro ya makerubi, miti ya ngazi na michoro ya maua yaliyochanua.
30Aliipakaa zahabu kwenye sakafu ya vyumba vya ndani na vya inje.
31Kwa kuingilia katika chumba cha ndani kabisa alitengeneza milango kwa mbao za mizeituni. Vizingiti na miimo ya milango vilifanya umbo la pembe tano.
32Katika milango hiyo miwili ya mizeituni, alichora makerubi, miti ya ngazi na maua yaliyochanua; akaipamba michoro hiyo kwa zahabu.
33Vilevile, alitengeneza mulango wa muraba wa kuingilia katika baraza. Miimo ya mulango huo ilikuwa ya mizeituni,
34na mbao zake mbili zilikuwa za miberoshi; kila ubao uliweza kukunjwa mara moja.
35Juu ya mbao hizo za mulango, kulichorwa makerubi, miti ya ngazi na maua yaliyochanua; akaipamba vizuri michoro hiyo kwa zahabu.
36Alijenga uwanja wa ndani ambao kuta zake zilikuwa za mistari tatu ya mawe yaliyochongwa, na mustari moja wa boriti za mwerezi.
37Musingi wa nyumba ya Yawe ulijengwa katika mwezi wa Zivu, katika mwaka wa ine.
38Na katika mwezi wa Buli, ni kusema mwezi wa nane, katika mwaka wa kumi na mumoja, ujenzi wa nyumba ulimalizika, na kazi ilikuwa imekamilika kama ilivyopangwa. Solomono alitumia miaka saba kwa kujenga.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.